Je! Unatafuta Hekima ya Kimungu?
1“Endelea Kutafuta-tafuta kama Kutafuta Hazina Zilizofichika” ndicho kilichokuwa kichwa cha hotuba yenye kuchochea ya siku ya pili ya “Haki ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya. Je! tunafuatia yale tuliyosikia na kujitahidi kuwa watafutaji hazina za hekima wenye bidii?—Mit. 2:1-6.
2Tungekuwa watafuta-hazina wabaya ikiwa tunasoma Biblia mara chache au ikiwa kwa kawaida tunashindwa kusoma Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Je! tunachimba ili tupate vito vyenye thamani vya hekima katika Neno la Mungu tunapotayarisha hotuba, kutafakari juu ya jibu kwa swali la Biblia, au kutafuta masuluhisho ya matatizo? Wakati unaotumiwa kwa utafiti na kutafakari unahitajiwa ili kutafuta vito vya Biblia, lakini ni furaha iliyoje inayopatikana!—Mit. 3:13-18.
3Sasa tunaweza kutumia kwa ukawaida kichapo kipya Insight on the Scriptures pamoja na Fahirisi, Konkodansi, Reference Bible, na vichapo vingine vyenye kutokeza katika maktaba yetu ya kitheokrasi. Jinsi Yehova ametupatia kwa ukarimu msaada tunaohitaji ili tutafute “mambo yenye kina kirefu ya Mungu”!—1 Kor. 2:10, NW.
4Afya yetu ya kiroho inahusiana moja kwa moja na hekima ya kimungu. Jumapili asubuhi ya mkusanyiko wetu, madokezo mengi mazuri yalitolewa katika hotuba “Kudumisha Afya ya Kiroho Katika Ulimwengu Mgonjwa.” Je! unakumbuka jinsi tunaweza kuepuka ugonjwa wa kiroho kwa sababu ya udhaifu wa mnofu, mavutano ya kilimwengu, na hila za Ibilisi? Msemaji wa mkusanyiko alionyesha kwamba tunaweza kujenga na kudumisha afya ya kiroho kwa kutoacha kamwe kujilisha wenyewe kiroho kupitia funzo, kwa kuhudhuria na kushiriki mikutanoni, na kushiriki utumishi wa shambani inavyofaa. Kujihadhari kama vile kukataa ushirika mbaya na vitumbuizo vya kilimwengu vyenye kushusha maadili huku tukiepuka pia watu ‘wasioyakubali maneno yenye uzima’ kutatusaidia tudumishe imani yenye afya.—1 Tim. 6:3, 4; Tito 1:13.
5Tunapofuata mambo tuliyojifunza kwenye “Haki ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya, acheni tupige moyo konde kufikiria inavyofaa yale tunayosikia kwenye mikutano ya Kikristo na hivyo tupate hekima zaidi ya kimungu na utambuzi.—2 Tim. 2:7.