Kutangaza Habari Njema-Kwa Kitabu Amani ya Kweli
1 Tunapoona mambo yakielekeza kwenye utimizo wa unabii wa 1 Wathesalonike 5:2, 3, tunapiga moyo konde kuendelea kujishughulisha sana katika kuwaonya watu juu ya kile kinachokaribia sana. Kwa sababu hiyo, katika huduma yetu ya shambani wakati wa Juni, tutaonyesha kitabu Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje? Kichapo hiki kizuri kunashughulika na yale ambayo watu wanafikiria na kinawatolea msingi timamu wa tumaini.
SABABU KWA NINI NI
CHA WAKATI UNAOFAA
2 Watu wengi wanajiuliza kama jitihada za sasa za amani za mataifa mawili yenye nguvu zitafanikiwa au ikiwa hazitafanikiwa zitayaingiza mataifa katika vita vya kinyukilia. Kitabu Amani ya Kweli kinaweza kuwapa faraja kwa maarifa ya kwamba Mungu ataletea aina ya binadamu amani yenye kudumu. Kusudi lake kwa ajili ya dunia haliruhusu wanadamu waiharibu. Njaa, umaskini mbaya sana, na ukosefu wa makao ni fungu la kawaida kwa mamilioni. Kitabu Amani ya Kweli kinaelekeza kwenye utatuzi halisi wa pekee kwa matatizo yanayotaabisha mataifa. Ukosefu wa usalama wa kibinafsi kwa sababu ya uhalifu unaositawi unawafanya wengi wahisi wakiwa kama watu walioshikwa mateka katika makao yao wenyewe. Kitabu Amani ya Kweli kinatoa mwangaza wa Kimaandiko kwenye ponyo. Mitindo ya maisha ya ki-siku-hizi, kutia na kutendea vibaya na kutumia vibaya nguvu za kufanya ngono ambazo Mungu alitupatia, kumeharibu uhai wa watu mmoja mmoja na jamaa zisizohesabika. Kitabu Amani ya Kweli kinaonyesha viwango vya Mungu na ulinzi unaopewa wale wanaochagua kuishi kulingana navyo.
UTOAJI WAKO
3 “Chanzo cha Amani na Usalama wa Kweli” kitakuwa ndicho Kichwa cha Mazungumzo kipya kuanzia Juni. Maandiko mawili yatakayotumiwa ni 1 Wathesalonike 5:3 na Mika 4:3, 4. Utapata kwamba madokezo kadhaa ya utangulizi yanayotolewa katika kitabu Reasoning kurasa 9-15 yanaweza kurekebishwa yalingane na kichwa hiki na mahitaji ya eneo la kwenu.
4 Katika mazungumzo yako, tumia maandiko mawili yaliyoonyeshwa ili kuonyesha kwamba amani inayotokezwa na wanadamu si ya kudumu lakini kwamba amani ya Mungu ni ya milele. Baada ya kusoma na kutoa maelezo kifupi kuhusu Mika 4:3, 4, unaweza kumvuta mwenye nyumba kwenye mazungumzo kwa kumwuliza anafikiri utimizo wa unabii huo utamaanisha nini kwa aina ya binadamu inayoteseka. Je! angefurahia kuona unabii huu ukitimizwa katika wakati wetu? Kisha unaweza kufungua picha inayoelekeana na ukurasa 99 katika kitabu Amani ya Kweli, toa maelezo kuihusu, kisha uelekeze fikira kwenye taarifa moja au mbili zilizochaguliwa ambazo zinafaa kwenye kurasa chache zinazofuata ambazo zinaonyesha tumaini lenye kutegemeka la amani na usalama wa duniani pote. Bila shaka, huenda ukataka kuelekeza fikira kwenye sehemu nyingine ya kitabu katika mazungumzo yako na mwenye nyumba fulani hasa.
5 Ikiwa hamna akiba ya kitabu Amani ya Kweli au vikiisha, muwe huru kutumia kitabu kingine chochote kinachopatikana chenye kurasa 192.
6 Amani ya kweli si ukosefu wa vita vya kutumia silaha tu, kwa kuwa inatia ndani afya njema, usalama, na hali njema ya kawaida. Ni Yehova peke yake, “Mungu wa amani,” na Mwana wake Yesu Kristo, “Mwana-Mfalme wa Amani,” wanaweza kuwahakikishia baraka za milele wale wanaofanya amani pamoja nao. (1 The. 5:23; Isa. 9:6, NW) Tunaweza kuwasaidia majirani wetu waone shangwe ya kuwa na amani pamoja na Mungu na Mwana wake sasa na kupata faraja katika tumaini la amani ya duniani pote ambayo itapatikana karibuni. Tunaweza kufanya hivi ikiwa ‘nyayo zetu zimevishwa vifaa vya habari njema za amani,’ tukitoa kitabu Amani ya Kweli wakati wa Juni.—Efe. 6:15, NW.