Kuingiza Sheria ya Mungu ‘Ndani ya Sehemu Zetu za Ndani’
1 Ilitabiriwa kwamba Yesu angekuwa na sheria ya Yehova ‘ndani ya sehemu zake za ndani.’ (Zab. 40:8, NW) Jambo hilo lilithibitika kuwa kweli, nalo lilimsaidia afanye mapenzi ya Baba yake.
2 Vilevile wanafunzi wake wapakwa-mafuta walikuwa na sheria ya Yehova ‘katika akili zao na imeandikwa katika mioyo yao.’ (Ebr. 8:10, NW) Hilo liliwawezesha kudumisha mwenendo mwema na kutimiza huduma yao kikamili. Sisi sote tunaweza kuhakikishaje kwamba sheria ya Yehova imo akilini mwetu na imeandikwa katika ubamba wa mioyo yetu?—Mit. 3:3.
FUNZO LA KIBINAFSI NA UTAFITI
3 Funzo la kibinafsi la Neno la Mungu linaweza kutusaidia tuufanye ukweli uwe wetu wenyewe. Funzo linatia ndani kufanya utafiti na kutafakari. Ni kukaza fikira kunakoendelezwa, kwenye kusudi pamoja na kuangalia habari zote ndogo ndogo kwa umakini. Hatupasi kusoma vichapo vya Sosaiti tunapovipokea tu bali tunapaswa kujitia nidhamu wenyewe ili tuwe na programu ya funzo la ukawaida ambayo itatutayarisha kwa ajili ya mikutano yetu yote ya kila juma.
4 Mazoea mazuri ya kujifunza yanaimarisha usadikisho wetu kuhusu ukweli na kung’arisha tumaini letu kwa wakati ujao. Ndiyo, ‘tunakulia wokovu.’ (1 Pet. 2:2) Tunapojifunza mambo yenye kupendeza kutoka katika Maandiko, tunataka kusema juu yayo. Hivyo tunachochewa kuonyesha jirani zetu upendo kwa kuwaambia mambo ambayo tumejifunza. Ushiriki wetu wa kusema “neno la ufalme” kwa bidii unafungamana na uthamini wa mambo ya kiroho ambayo tumepata kupitia mazoea mazuri ya kujifunza.—Mt. 13:19.
MISAADA YA KUJIFUNZA
5 Tengenezo la Yehova limetuandalilia kile tunachohitaji ili tupate maarifa bora zaidi ya ukweli. Je! wewe unatumia Index ya 1930-1985 vizuri? Tukiwa na chombo hiki kizuri na vichapo mbalimbali ambavyo vinapatikana sasa, ni hazina iliyoje ya maarifa sahihi tuliyo nayo! Tusisahau vitabu Insight na Revelation Climax. Je! unavitumia kwa matokeo mazuri?
6 Kupata faida zote kutokana na funzo la kibinafsi kunategemea wakati tunaotumia kujifunza. Kulingana na zilivyo hali zako za kila siku, amua wakati na mahali ambapo kimya na ufaragha unaohitajiwa unaweza kupatikana ili kukaza fikira na kutafakari. Hakikisha unasali ili upate msaada wa Yehova kabla ya kuanza funzo. Ili kutenda kwa hekima katika nyakati hizi zenye hatari, ukweli wa Neno la Mungu unapasa kuwa umeandikwa ndani ya mioyo na akili zetu. (Mit. 7:1-3; Yos. 1:8) Yehova anatumia roho yake kukaza imara sheria na vikumbusha vyake ndani ya mioyo yetu. (Yoh. 14:26; 1 Kor. 2:10) Yeye hatapuuza ombi la moyo mweupe la kutaka msaada wa kupata na kuelewa hazina za Neno lake.—Mit. 2:1-6.
7 Tunahitaji kuwa wa kawaida na wenye uthabiti katika programu yetu ya funzo ili tuingize sheria ya Yehova ‘ndani ya sehemu zetu za ndani.’ Hivyo tunakuza hali ya kiroho zaidi, tunapata kuelewa ukweli vizuri zaidi, tunafanyia maendeleo ustadi wetu katika kuwasaidia wengine wajifunze ukweli, na tunadumisha msingi imara katika “njia ya uzima.”—Zab. 16:11; Kol. 2:7.