Kuonea Shangwe Ushirika wa Kitheokrasi
1 Mashahidi wa Yehova huitana “ndugu” na “dada.” Hii inaonyesha uhusiano wa karibu unaopaswa kuwapo miongoni mwa watumishi wote wa Yehova Mungu.
2 Neno “ndugu” linamaanisha kihalisi “mwana wa wazazi wale wale.” Je! wewe unahisi vifungo vya uhusiano mchangamfu wa kiroho pamoja na wote ambao ni watumishi wa Yehova waliojitoa wakfu? Tunaweza kukuzaje zaidi aina ya upendo unaothibitisha kwamba sisi ni ndugu au dada kwa washiriki wetu wa Kikristo?
KWENYE MIKUTANO
3 Wanafunzi wa Yesu walithamini umuhimu wa kukutana pamoja. (Mdo. 2:42, 46; 20:7, 8) Sisi pia tunathamini pendeleo la ushirika mchangamfu wa Kikristo. (Rum. 16:3, 5) Hata hivyo, je! maneno tunayosema mikutanoni yanafunua kwamba tunahangaikia kikweli hali njema ya kiroho ya ndugu na dada zetu? Kupitia maelezo yetu mikutanoni, tunaweza kuendeleza upendo na kupendezwa kusiko kwa kibinafsi katika hali njema ya wengine. Tunataka kuwatia moyo ndugu zetu wawe wenye bidii katika kupiga mbiu ya habari njema na kuwa kielelezo chema katika pande zote za maisha ya kila siku.—Ebr. 10:24, 25.
4 Kuna fursa nyingi za ushirika wa kitheokrasi kabla na baada ya mikutano. Tunapaswa kutumia wakati huu kupanua ushirika wetu kwa kuwakaribisha wapya na kufahamiana na wengi iwezekanavyo. Kushiriki maono ya utumishi wa shambani na mazungumzo mengine yenye kujenga kutachangia kuwatia moyo wengine.—1 The. 5:11, 15.
USHIRIKA WENYE KUJENGA
5 Mtu hawezi kutembea na Mungu huku akikimbia kwa kushirikiana na wale walio katika jamii mbovu na yenye kuchukiza inayokubali kila kitu ambacho Mungu anakirihi. Biblia inaonya: “Mazungumzo [mashirika, NW] mabaya huharibu tabia njema.” (1 Kor. 15:33) Huenda wengine katika kundi wakawa na mwelekeo wa kukaribisha watu wa kilimwengu wanaofahamiana nao na watu wa ukoo wasioamini ambao hawapendezwi na ukweli kwenye vikusanyiko vya starehe, wakiwaza kwamba hilo litawasaidia waukubali ukweli. Hata hivyo, je! hilo ni jambo la hekima na linalolingana na Maandiko?
6 Tumeshauriwa tuangalie jinsi tunavyoshughulika na watu wa mataifa, wasioamini, na watu wa kawaida. (Ona toleo la Novemba 15, 1988 la Mnara wa Mlinzi kurasa 15-16.) Kwa nini tushirikiane isivyohitajiwa na watu ambao wangali wanafuatia njia za kilimwengu na ambao hawajawa waabudu wa Yehova? (2 Kor. 6:14, 15) Wengine ambao si waangalifu kiroho wanaweza kutafuta pia wengine ambao wanashikilia kuwaza na njia za kilimwengu badala ya kutafuta ushirika wa Wakristo waliokomaa ambao wanaweza kuwasaidia wawe imara katika imani. Wanakosa kuthamini kwamba kuhudhuria vikusanyiko vya starehe na watu wa kilimwengu, wasio na kanuni za kuwaongoza kunaweza kudhoofisha imani yao na kuwafisidi.—Linganisha 2 Wathesalonike 3:14, 15.
7 Kila mtu anayetaka kuzoea ukweli anapaswa atafute washiriki ambao wamejitoa kwa Yehova na ambao watamsaidia atembee katika njia ya ukweli na kuchangia maendeleo yake katika kumtumikia Yehova. Rafiki na washiriki wetu wanaweza kutuathiri sana. Kwa hiyo, jinsi lilivyo jambo lenye hekima kutafuta ushirika wa watu wanaomcha Mungu ambao wanadumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova!