Sanduku la Swali
● Ni nini kazi za wale wanaotumikia wakiwa wakaribishaji kwenye mikutano ya kundi?
Wakaribishaji wapaswa kutoa salamu changamfu kwa wote wanaokuja kwenye mikutano. Kazi zao ni kutia na kuonyesha wenye kuchelewa mahali pa kuketi, kurekodi hudhurio, kudumisha utaratibu na usalama, na kuangalia kuna hewa ya kadiri inayofaa kwenye Jumba la Ufalme. Wakaribishaji wapaswa kuwa wenye urafiki, ndugu wenye kuchukua madaraka kwa uzito wasiongojea kuambiwa madaraka yao.—omSW kur. 63-4.
Wakaribishaji wapaswa kuwa macho kuona mahitaji ya wapya, wawafanye wahisi wamekaribishwa, na kuwasaidia wapate viti. Wote kundini wapaswa kuwa tayari kusaidia wapya wafahamikiane na kuhisi wamekaribishwa. Wanapowaelekeza waliochelewa kwenye viti vilivyo wazi, wakaribishaji wapaswa kujitahidi wasiwasumbue wale waliokwisha kuketi. Nyakati nyingine wanawapa wapya gazeti linalojifunzwa.
Kudumisha utaratibu wakati wa mikutano ni jambo la muhimu. Kwa kuwa tunatia moyo wazazi walete watoto wao kwenye mikutano, nyakati nyingine kutakuwako makatizo. Lakini watoto wanapoendelea kusumbua-sumbua au kukosa adabu, mkaribishaji apaswa kutoa msaada kwa fadhili, labda kudokeza mzazi atoe mtoto huyo nje ya jumba kwa muda fulani. Wazazi wenye watoto wachanga wakiketi mahali wanapoweza kutoka nje kwa urahisi inapohitajiwa kabisa, kuangalia mahitaji ya watoto wao wadogo kwaweza kufanywa bila kuondosha sana fikira za wengine.
Katika maeneo ambayo usalama ni tatizo, wakaribishaji wapaswa kupewa mgawo wa kulinda mali isiharibiwe au mivurugo ya wapinzani. Ikiwa mtu fulani ndani ya Jumba la Ufalme anajaribu kukatiza mkutano, apaswa kuulizwa aondoke. Akikataa na kuendelea kusababisha mvurugo, wazee waweza kuwasiliana na wenye mamlaka. Katika maeneo fulani huenda ikahitajiwa kwa ndugu waliopewa mgawo kukagua eneo la kuegeshea magari la Jumba la Ufalme wakati wa mikutano.—kmSW 12/84 uku. 8.
Hudhurio linapochukuliwa, watu wote wazima na pia watoto wachanga wanaosikiliza na kufaidika na mkutano, hata kwa kadiri isiyo kubwa, wapaswa kuhesabiwa.—kmSW 8/79 uku. 4.