Sanduku la Swali
● Tunawezaje kuwa makini kuhusu usalama wa Jumba la Ufalme?
Kwa kuwa tunaishi katika nyakati hatari, tunahitaji kuwa na hekima tunapozingatia usalama wa Jumba la Ufalme. Kama vile tunavyokuwa waangalifu kuhakikisha nyumba zetu ni salama, tunapaswa kufanya vivyo hivyo kuhusu Majumba yetu ya Ufalme. Ni jukumu la wazee kuhakikisha kwamba Jumba la Ufalme liko salama vya kutosha. Ni wazi kwamba kuna uhitaji wa kufanya hivyo kwa sababu kuna visa vinavyoripotiwa vya wizi na uharibifu wa majumba yetu katika sehemu mbalimbali.
Kwanza kabisa usalama mzuri unahusisha kufunga kabisa milango, mageti, na madirisha yote kila baada ya kutumia Jumba la Ufalme. Ndugu wanaotegemeka wanapaswa kusimamia mipango hiyo ya usalama kila mara jumba linapotumika. Pia, wanapaswa kufanya hivyo kunapokuwa na harusi au jumba linaposafishwa.
Ikiwa Jumba la Ufalme lina eneo la kuegesha magari, inapendekezwa kwamba kila inapofaa kuwe na mwangaza wa kutosha. Jambo hili litapunguza kuharibiwa kwa magari na uwezekano wa ndugu na dada kujeruhiwa wanapotoka kwenye jumba. Makutaniko mengine yamefanya mpango ili kuwe na ndugu wanaofanya mgawo wa ukaribishaji kwa zamu ndani na nje ya jumba wakati wa mkutano, ili kuhakikisha usalama katika eneo la maegesho na hivyo kupunguza visa vya wizi na uharibifu.
Makutaniko mengine hulazimika kufunga milango yote wakati mikutano inaendelea. Katika hali kama hizo wakaribishaji wenye kutegemeka wanapaswa kuwa mlangoni wakati wote ili kujua ni nani wanaoingia kwenye jumba. Baraza la wazee linapaswa kujua ni mambo gani wanayoweza kufanya yanayopatana na sheria za eneo wanamoishi, kuhusu usalama wa mahali pa kufanya mikutano ya hadharani. Ikiwa mipango kama hiyo inaanzishwa, kutaniko lipewe taarifa mapema ili wajue kwamba mlango wa kuingia kwenye Jumba la Ufalme utakuwa ukifungwa.
Tunataka ndugu na dada na wanaopendezwa wahisi wako salama wanapohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme na tungependa kulinda jumba letu dhidi ya uharibifu na wizi. Kwa hiyo, wazee katika kila kutaniko wanapaswa kuzingatia hali zilizopo katika eneo lao na watende kulingana na hali hizo ili kuhakikisha usalama wa wote wanaohudhuria mikutano na usalama wa Jumba la Ufalme.