Hekimika—Tumia Mambo Unayojifunza
1 Ni mradi wa binadamu walio wengi kuishi maisha ya furaha, yenye amani. Maelfu ya vitabu na makala vinatoa shauri juu ya jinsi ya kuwa na ndoa yenye kufanikiwa, jinsi ya kulea watoto, jinsi ya kufanikiwa kifedha, jinsi ya kupata na kudumisha afya njema, na habari nyingine nyingi tofauti-tofauti zinazohusiana na kusaidia watu wapate furaha. Ijapokuwa hekima fulani inayotumika yaweza kupatikana katika vichapo vya kilimwengu, watu walio wengi katika ulimwengu hawana furaha na amani. Ni kwa nini hivyo?
2 Jibu laweza kupatikana katika Biblia kwenye Mithali 1:7, NW, ambapo panasema: “Hofu ya Yehova ndio mwanzo wa maarifa. Hekima na nidhamu ndivyo wapumbavu tu wamedharau.” Mtu hawezi kutazamia amani na furaha kama yeye hatambui na kuheshimu Chimbuko la maarifa na hekima ya kweli, Yehova Mungu.
3 Ulimwengu umefukarika—wafa njaa kiroho. Ajabu ni kwamba, hali hii ya kusikitisha ni ya kujiletea, kwa kuwa utele wa chakula cha kiroho unapatikana duniani pote, na ni cha kuchukuliwa bure. (Mit. 1:20, 21; Ufu. 22:17) Kwa sababu watu katika ulimwengu wanakataa hekima kutoka kwa Yehova, wanaendelea kujikwaa-kwaa katika giza la kiroho. (Mit. 1:22-32) Kwa upande mwingine, tukiwa watu wa Yehova, wanaostahi sheria zake na kufuata amri zake, tunalishwa vizuri kiroho na tuna furaha. (Isa. 65:13, 14) Pia, upendo unaojaa katika tengenezo la Mungu hututambulisha sisi kuwa wanafunzi wa kweli wa Kristo. (Yohana 13:35) Ndiyo, udugu wa ulimwenguni pote wa Mashahidi wa Yehova hutoa uthibitisho ulio hai kwamba kuambatana na mafundisho ya Biblia ndio mwendo wa hekima kufuata.
4 Bado, wengine ambao wanashirikiana na tengenezo la Yehova huenda wasiwe wanapata furaha ambayo yaweza kuwa yao. Huenda hata wakaathiri vibaya furaha ya wengine wanaowazunguka kwa mambo wanayosema na kufanya. Yaweza kuwaje hivyo? Ni kwa sababu tu hawafuati hekima ya Mungu maishani mwao. Huenda wakahudhuria mikutano ya kundi, makusanyiko ya mzunguko, na mikusanyiko ya wilaya. Huenda wakajua ya karibuni ambayo vichapo vya Sosaiti vinasema, lakini mtindo wao wa maisha na namna wanavyoshughulika na wengine, kutia ndani Wakristo wenzao, hauonyeshi matumizi ya ukweli ambao wamejifunza. Ni nini linalohitaji kufanywa? Watu hao wanahitaji kukaza fikira juu ya ‘kupanda kwa roho’ ili wapate kuleta furaha ya kweli maishani mwao wenyewe na kuchangia furaha ya wale wanaowazunguka.—Gal. 6:7, 8.
MAMBO YA KUTUMIA
5 Sisi mmoja mmoja tukilegea, kuacha kuwa wenye hadhari, na kushindwa na Shetani, ulimwengu, au mnofu wetu usiokamilika, tutapoteza shangwe ya kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova. Sasa, kuliko wakati mwingine uliotangulia, ni lazima kuwa chonjo kutumia mambo tunayojifunza kwenye mikutano yetu ya kundi na makusanyiko na pia kupitia maandalizi mengine ya tengenezo. Ulimwengu ambamo twaishi ni mahali hatari panapobadilika daima. Tunahitaji kuwa chonjo kutumia shauri ambalo Yehova huandaa kwa upendo kupitia jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” tukitambua ni chakula cha wakati unaofaa.—Mt. 24:45-47.
6 Katika programu ijayo kwa ajili ya siku ya pekee ya kusanyiko, habari nyingi nzuri zimeandaliwa juu ya jinsi ya kusimama imara tukiwa kundi moja. Madokezo yenye kutumika juu ya jinsi ya kupambana na mavutano yenye kudhoofisha, kama vile mastakimu zenye kuvunja moyo, roho ya kilimwengu ya kujitegemea, na vikengeuo vyenye kupoteza wakati. Je! sisi tunafuata shauri zuri la kutegemea kikamili Yehova na njia zake, kutambua na kutii mamlaka ya kitheokrasi, kujinyenyekeza na kuwa na kiasi, na kununua wakati kwa ajili ya mambo ya kitheokrasi? (Mik. 6:8; Efe. 5:15, 16; Ebr. 6:10; 13:17) Je! washiriki wa jamaa wanasaidiana ili kujipatanisha na mtindo wa maisha ya Kikristo? Uchaguzi wetu wa vitumbuizo, tabia zetu, na kawaida zetu za kila siku zapasa kuongozwa na mashauri tunayopokea katika Maandiko. Isipokuwa kuwe na jitihada ya bidii ya kutumia mambo tuliyojifunza, kutakuwako maendeleo kidogo ya kiroho au kusiweko, na amani yetu ya akili na furaha vitaathiriwa vibaya.—Flp. 4:7-9; Yak. 1:22-25.
7 Jitihada ya pamoja katika funzo la kibinafsi na la jamaa inahitajiwa. Watch Tower Publications Index chaweza kutuelekeza kwenye habari ya kindani juu ya matumizi ya kanuni za Biblia. Kitabu Young People Ask ni kifaa bora kabisa kwa wazazi kutumia katika kuwasaidia watoto wao wakabiliane na ulimwengu wa kishetani wa leo uliotatanika sana. Kwa kurejezea habari hiyo, tutapata maoni ya Yehova juu ya mambo na twaweza kuongozwa na kanuni za uadilifu. Kutofanya hivyo kutakuwa ni kama kuwa na dawa ya maradhi fulani lakini kutoimeza, hata ingawa tunajua ingemaliza ugonjwa unaotusumbua. Funzo la kawaida la kibinafsi na la jamaa litafanya imani yetu ikue na kutupa nguvu za kuvumilia. Katika wakati wa jaribu, imani yetu haitafifia, na kusababisha tukengeuke.—Mt. 13:6; Luka 8:13; Ebr. 2:1.
8 Wazee na watumishi wa huduma wanapaswa kuweka kielelezo katika kusimamia nyumba zao. Hiyo ingetia ndani kuwasaidia wake na watoto wao watumie mambo wanayojifunza katika Neno la Mungu na tengenezo ili waendelee kuwa na nguvu kiroho. Katika njia hiyo, jamaa yote yaweza kuwa kielelezo kizuri katika maisha ya Kikristo na kuandaa kitia-moyo kwa wengine ndani na nje ya kundi.—Efe. 6:4; 1 Tim. 3:4, 12, 13.
WA KUSAIDIWA
9 Kati ya wale wanaohudhuria Ukumbusho kila mwaka kuna wengi wanaohitaji kitia-moyo zaidi ili watumie yale wanayojifunza na kushirikiana kwa tendo na tengenezo. Mfikirio wa upendo waweza kuonyeshwa kwa wanafunzi wa Biblia wetu kwa kuwafundisha jinsi ya kutumia kanuni za Biblia maishani mwao na jinsi ya kutimiza amri za uadilifu za Mungu. Tunapaswa kuonyesha hangaiko kwa ajili ya wale wanaofanya maendeleo kuelekea kuwa ndugu na dada zetu katika imani.
10 Wowote ambao wamekuwa wasio wa kawaida au wasiotenda wapaswa kusaidiwa waone uhitaji wa kushiriki katika utendaji wa kawaida pamoja na tengenezo. Wanahitaji kupata tena amani na furaha waliyokuwa wakionea shangwe hapo awali walipomtumikia Yehova kwa ukamili zaidi. (Yn. 13:17) Kwa kuwasaidia kwa fadhili waamshe tena uthamini wao kwa ajili ya ukweli na ‘kumpa Mungu dhabihu ya sifa,’ wataweza kutumia mambo wanayojifunza na kubaki kwenye barabara inayoongoza kwenye uhai.—Ebr. 13:15; ona Huduma ya Ufalme Yetu, Julai 1979, kurasa 1, 2, na Machi 1977, ukurasa 3.
11 Watu wote wa Mungu wanahitaji kwenda sambamba na tengenezo la Yehova lenye kwenda kasi. Hatuwezi kujiruhusu tuvutwe kuingia katika hali ya kutosheka. Sikuzote ni lazima tudumishe hali yetu ya kiroho, kwa kwenda pamoja na habari ya karibuni zaidi inayoandaliwa kupitia tengenezo la Mungu na kuitumia mara hiyo. Hiyo inataka jitihada ya bidii-nyendelevu na nyakati nyingine dhabihu ya kibinafsi. Lakini Yehova hatutaki tufanye kile tusichoweza. Yeye ndiye Muumba wetu, na yeye anajua yanayotufaa kabisa. Kwa hiyo acheni tujithibitishe wenyewe kuwa walio na hekima kwa kuendelea kufundishwa na Yehova na kutumia mambo tunayojifunza. Hilo litamletea sifa na kutokeza manufaa ya milele kwa ajili yetu.—Isa. 48:17; 54:13.