Kuelekeza Wanafunzi wa Biblia Kwenye Tengenezo la Yehova
1 Wanafunzi wa Biblia wahitaji kufahamiana na tengenezo la lile “kundi moja” ambalo Yesu alisema juu yalo kwenye Yohana 10:16. Ni lazima wathamini kwamba kujitambulisha wenyewe na tengenezo la Yehova ni jambo la muhimu sana kwa wokovu wao. (Ufu. 7:9, 10, 15) Kwa hiyo, yatupasa tuanze kuelekeza wanafunzi wa Biblia wetu kwenye tengenezo mara tu funzo la Biblia likiisha anzishwa.
2 Saidieni wanafunzi wenu wa Biblia wafahamiane na yale mambo mengi ya tengenezo la Yehova la kidunia. Kwa kufuata kiolezo cha karne ya kwanza, watu wote wa Yehova walikuwa katika makundi ambayo washiriki wayo walikuwa wazee, watumishi wa huduma, na wahubiri. Leo, washiriki wa makundi huonea shangwe kuhudhuria mikutano mitano kila juma. Kuna makusanyiko ya pindi kwa pindi na mikusanyiko iliyoratibiwa mwakani, na hiyo huandaa fursa za kushirikiana na Mashahidi wenzi kutoka maeneo mbalimbali. Pia, kuna mapainia, wamisionari, na waangalizi wasafirio, na pia Baraza Linaloongoza ambalo huelekeza kazi ulimwenguni pote. Unaweza kufanyaje mwanafunzi wako wa Biblia afahamiane na pande mbalimbali za tengenezo la Yehova? Waweza kuwasaidiaje waone kwamba muundo wa tengenezo una msingi wa Biblia?
TUMIA BROSHUA KUFANYA MAPENZI YA MUNGU
3 Broshua Kufanya Mapenzi ya Mungu ina habari yote juu ya tengenezo la Yehova. Kwa kuitumia waweza kuwafanya wanafunzi wa Biblia wafahamiane na tengenezo hatua kwa hatua na kuwasaidia wathamini linavyotenda. Njia nzuri ya kuanza ni kuzungumza yanayotukia kwenye Jumba la Ufalme. Hilo litamtia moyo mwanafunzi wa Biblia ahudhurie mikutano ya kundi. Kabla ya kumwalika kwenye hotuba ya watu wote kwa mara ya kwanza, pitia habari katika kurasa 14 na 15. Vuta fikira zake kwenye picha. Eleza mahali pa Jumba la Ufalme lenu na namna linavyoonekana. Hata waweza kumwonyesha picha ya Jumba la Ufalme unalohudhuria.
4 Wakati ziara ya mwangalizi wa mzunguko inapotangazwa kundini, zungumza pamoja na mwanafunzi wa Biblia kurasa 20 na 21. Tumia maswali kwenye mwisho wa ukurasa 21 kukazia mambo makuu. Zungumza pamoja naye msingi wa Kimaandiko wa mpango wetu wa sasa kwa kutumia fungu la kwanza katika ukurasa wa 20. Habari hiyo itafanya ziara ya kwanza ya mwanafunzi wako kwenye Jumba la Ufalme iwe na maana.
5 Vivyo hivyo, kabla ya mkusanyiko wenu wa wilaya, kusanyiko la mzunguko, au siku ya kusanyiko la pekee, zungumzeni habari iliyochapwa katika ukurasa wa 19. Vuta fikira zake kwenye yale yanayohusika katika mkusanyiko mkubwa, na kumwonyesha mweneo wa ulimwenguni pote unaoonyeshwa katika picha katika ukurasa wa 18. Wakati unapotoa maelezo juu ya kielezi kinachoonyesha kutolewa kwa kichapo kipya, waweza kutayarisha kwa ajili ya mazungumzo zaidi ya kurasa 24 na 25. Ili kueleza kazi ya painia, zungumzeni kurasa 22 na 23.
PATANISHA NA UHITAJI
6 Kama unavyoweza kuona, si lazima kuanza kwenye mwanzo wa broshua Kufanya Mapenzi ya Mungu. Badala ya hivyo, fursa na uhitaji utokeapo, zungumzeni mambo hususa kutoka broshua hiyo ambayo yatamsaidia mwanafunzi athamini tengenezo la Yehova na kumtia moyo ashirikiane na kundi la kwenu.
7 Kunena kwa usadikisho wakati wa kuzungumzia mambo hayo kutavuta mwanafunzi kwa njia yenye kudumu. Uwake roho. (Mdo. 18:25) Pia, hakikisha kwamba wewe, “umfundishaye mwingine,” waweka kielelezo chema katika kuonyesha uthamini kwa ajili ya tengenezo la Yehova. (Rum. 2:21) Kwa kufanya hivyo, waweza kusaidia wengine wajiunge na lile kundi moja analoongoza Yesu kwenye uhai wa milele.