Kuelekeza Wanafunzi Kwenye Tengenezo Linalomaanishwa na Jina Letu
1 “Ujumbe unasemwa katika lugha zaidi ya 200. Ujumbe unasikiwa katika nchi zaidi ya 210. Ujumbe unatolewa kibinafsi popote ambapo huenda watu wakapatikana. Wote huo ni sehemu ya kampeni kubwa zaidi ya kuhubiri ambayo ulimwengu umepata kujua, ujumbe wenye kuunganisha mamilioni duniani pote. Mashahidi wa Yehova wamepangwa kitengenezo kutimiza kazi hii kwa miaka zaidi ya mia moja!”
2 Ndivyo linavyoanza simulizi la vidio Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name. Hiyo yaendelea kujibu maswali haya: Mashahidi wa Yehova ni nani hasa? Utendaji wao umepangwaje? Unaelekezwaje? Unagharimiwaje? Hiyo hutia mioyoni mwa watazamaji wayo uhakika wa kwamba “Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wamezoezwa kuwa tengenezo la kusaidia jirani zao kujenga imani katika Biblia,” nayo huwatia moyo kujionea wenyewe tengenezo linalomaanishwa na jina letu. Baada ya kuona vidio hii, mwanamke aliyekuwa akijifunza alitokwa machozi ya shangwe na uthamini naye alisema: “Mtu yeyote awezaje kukosa kuona kwamba hili ndilo tengenezo la Mungu wa kweli, Yehova?”—Linganisha 1 Wakorintho 14:24, 25.
3 Mwanamke mwingine alikuwa amejifunza Biblia mara kwa mara kwa muda mrefu, lakini hakuwa akikubali kwamba Utatu ni fundisho lisilo la kweli. Kisha yeye na mume wake wakaonyeshwa vidio yetu. Walivutiwa sana na utoaji huo nao wakaitazama mara mbili usiku huohuo. Katika funzo lao lililofuata, mke alieleza tamaa yake ya kuwa Shahidi. Alisema alikuwa akikazia fikira itikadi yake katika Utatu, akashindwa kutazama tengenezo letu na watu waliomo ndani yalo. Kutokana na vidio hiyo alitambua kwamba alikuwa amepata tengenezo la kweli la Mungu. Alitaka kuanza kuhubiri nyumba hadi nyumba mara hiyo. Baada ya kuelezewa hatua za lazima za kuwa mtangazaji asiyebatizwa, yeye alisema: “Nitachukua hatua zihitajiwazo mara moja.” Aling’atuka kutoka kanisa lake, akaanza utendaji wa utumishi wa shambani, akawa hodari katika kukanusha Utatu.
4 Imethibitishwa vema kwamba wanafunzi wa Biblia hufanya maendeleo bora ya kiroho na kukua kuelekea ukomavu haraka zaidi wanapotambua tengenezo la Yehova na kushiriki nalo. Jambo la maana ni kwamba, baada ya wale watu 3,000 kubatizwa kwenye Pentekoste, ‘wakaendelea kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume na kushirikiana.’ (Mdo. 2:42, kielezi-chini katika New World Translation of the Holy Scriptures—With References.) Ni jambo la muhimu kwamba tusaidie wanafunzi wafanye vivyo hivyo leo. Twawezaje?
5 Timiza Daraka Hilo: Kila mwenye kufanya wanafunzi lazima atambue kwamba ni daraka lake kuelekeza mwanafunzi wa Biblia kwenye tengenezo la Mungu. (1 Tim. 4:16) Kila kipindi cha funzo chapaswa kuonwa kuwa jiwe la kukanyagia kuelekea ile siku yenye furaha wakati ambapo huyo mpya ataonyesha wakfu wake kwa Yehova kupitia ubatizo wa maji. Mojawapo ya maswali atakayoulizwa wakati wa sherehe ya ubatizo ni hili: “Je, waelewa kwamba wakfu na ubatizo wako unakutambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika ushirikiano na tengenezo la Mungu linaloelekezwa kwa roho?” Kwa sababu hiyo, ni jambo la maana atambue kwamba hawezi kumtumikia Mungu bila kushirikiana kwa juhudi na kutaniko la kweli la Kikristo.—Mt. 24:45-47; Yn. 6:68; 2 Kor. 5:20.
6 Endelea kuelimisha mwanafunzi kuhusu kutaniko la kwenu na tengenezo la kimataifa linalomaanishwa na Mashahidi wa Yehova. Fanya hivi katika kila kipindi cha funzo la Biblia, kuanzia na kile cha kwanza. Kuanzia mwanzo kabisa, mwalike mwanafunzi kwenye mikutano, na uendelee kumwalika.—Ufu. 22:17.
7 Tumia Vyombo Vinavyoandaliwa: Vichapo vyetu vilivyo bora zaidi kwa kutumia katika kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani ni broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? na kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Vyote hivyo hukazia uhitaji wa kushirikiana na kutaniko. Mwishoni mwa somo la 5 katika broshua Anataka husema: “Wewe wahitaji kuendelea kujifunza kumhusu Yehova na kuyatii matakwa yake. Kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwenu kutakusaidia ufanye hivyo.” Kitabu Ujuzi humtia moyo mwanafunzi kwa kurudiarudia ashiriki kwenye mikutano. Sura ya 5, fungu la 22, hutoa mwaliko huu: “Mashahidi wa Yehova . . . wanakuhimiza kwa uchangamfu ushiriki nao katika kumwabudu Mungu ‘katika roho na kweli.’ (Yohana 4:24)” Sura ya 12, fungu la 16, husema: “Uendelezapo funzo hili na kufanya desturi yako iwe kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, bila shaka imani yako itatiwa nguvu hata zaidi.” Sura ya 16, fungu la 20, husema: “Fanya liwe zoea lako kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova.” Hilo huongezea: “Hili litakusaidia uelewe kisha utumie ujuzi juu ya Mungu maishani mwako na litakuletea furaha. Kuwa sehemu ya udugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote kutakusaidia uendelee kuwa karibu na Yehova.” Sura ya 17 huzungumzia kikamili jinsi mtu apatavyo usalama wa kweli miongoni mwa watu wa Mungu. Tujifunzapo na wengine, ni daraka letu kukazia sehemu hizi za habari.
8 Broshua Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote ni chombo kizuri ambacho kimetokezwa kujulisha watu mmoja-mmoja tengenezo pekee lionekanalo ambalo Yehova anatumia leo kutimiza mapenzi yake. Habari yenye kina iliyo nayo kuhusu huduma yetu, mikutano na tengenezo itatia moyo msomaji ashiriki nasi katika kumwabudu Mungu. Mara tu funzo la Biblia lianzishwapo, inapendekezwa kwamba tumtolee mwanafunzi nakala ya broshua hii aisome mwenyewe. Hakuna haja ya kuisoma pamoja naye kama ilivyokuwa ikifanywa wakati uliopita.
9 Baadhi ya vidio ambazo Sosaiti imetokeza ni vyombo bora kabisa vya kuelekeza wanafunzi kwenye tengenezo linalomaanishwa na jina letu. Ingekuwa vizuri kama wangeweza kutazama (1) The New World Society in Action, pitio la filamu ya 1954 iliyonasa ile roho yenye utulivu, yenye matokeo, na yenye upendo ambayo kwayo tengenezo la Yehova hufanya kazi; (2) United by Divine Teaching, ambayo huchunguza muungano wenye amani ambao umeonyeshwa kwenye mikusanyiko yetu ya kimataifa katika Ulaya Mashariki, Afrika, Amerika Kusini, na Asia; (3) To the Ends of the Earth, ambayo ilitia alama ukumbusho wa miaka 50 wa Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower na yaonyesha matokeo ambayo wamishonari wamekuwa nayo katika kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri; (4) Jehovah’s Witnesses Stand Firm Against Nazi Assault, ambayo husema hadithi yenye kusisimua ya moyo mkuu wa Mashahidi na ushindi katika kabiliano la mnyanyaso wa kinyama wa Hitler; na, bila shaka, (5) Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name.
10 Weka Miradi Yenye Maendeleo Kuhusu Mikutano: Lazima wanafunzi waelezwe kwamba twahitaji kujifunza faraghani ambako huandaliwa kwa namna ya funzo la Biblia nyumbani na pia mazungumzo ya darasani ambayo huandaliwa kwenye mikutano ya kutaniko. (Yn. 6:45) Mtu mpya anahitaji kufanya maendeleo katika uelewevu wake wa Maandiko na tengenezo. Ili kufikia hayo, hakuna kitu cha badala ya mikutano. (Ebr. 10:23-25) Anza kumwalika mtu huyo kwenye mikutano ya kutaniko mara moja. Baadhi ya watu wapya wenye kupendezwa huanza kuhudhuria mikutano hata kabla ya kuwa na funzo la Biblia nyumbani la ukawaida. Bila shaka, twataka kuweka kielelezo kizuri sisi wenyewe kwa kuhudhuria kwa ukawaida.—Luka 6:40; Flp. 3:17.
11 Shiriki naye habari ya kutosha kuhusu mikutano na jinsi inavyoongozwa ili mwanafunzi ahisi kuwa mtulivu anapohudhuria mkutano wake wa kwanza. Kwa kuwa watu fulani hawajihisi huru zaidi wanapoenda mahali papya kwa mara ya kwanza, huenda ikafaa kuandamana na mwanafunzi kwenye Jumba la Ufalme anapohudhuria mkutano wake wa kwanza. Atahisi huru ukiwa pamoja naye anapokutana na washiriki wa kutaniko. Zaidi ya yote, uwe mkaribishaji mzuri kwa mgeni wako, ukimfanya ajihisi amekaribishwa na starehe.—Mt. 7:12; Flp. 2:1-4.
12 Tia moyo mwanafunzi ahudhurie siku ya kusanyiko la pekee, kusanyiko la mzunguko, au mkusanyiko wa wilaya kwenye fursa ya kwanza. Labda unaweza kumhusisha katika mipango yako ya usafiri.
13 Tia Ndani Uthamini wa Kuhisiwa Moyoni: Kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu, ukurasa wa 92, hueleza: “Kama mazungumzo yako na watu wenye kupendezwa yanaonyesha kwamba unathamini sana sana tengenezo la Yehova, itakuwa rahisi zaidi kwao kukua wasitawishe uthamini na wataongozwa wafanye maendeleo makubwa zaidi katika kupata kumjua Yehova.” Sikuzote sema kwa njia chanya, si kwa njia isiyofaa, kuhusu kutaniko la kwenu. (Zab. 84:10; 133:1, 3b) Katika sala unazotoa kwenye funzo la Biblia, taja kutaniko na uhitaji wa mwanafunzi kushirikiana nalo kwa ukawaida.—Efe. 1:15-17.
14 Kwa hakika twataka wapya wasitawishe uthamini wa kuhisiwa moyoni kuelekea uandamani na usalama wa kiroho ambao wapatikana miongoni mwa watu wa Mungu. (1 Tim. 3:15; 1 Pet. 2:17; 5:9) Tukiwa Mashahidi wa Yehova, acheni tufanye yote tuwezayo kuelekeza wanafunzi wa Neno la Mungu kwenye tengenezo linalomaanishwa na jina letu.
[Blabu katika ukurasa wa 3]
Wanafunzi hufanya maendeleo ya kiroho haraka zaidi wanapojionea wenyewe tengenezo
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Usikawie kuwaalika wanafunzi wahudhurie mikutano