Saidia Wengine Wahudhurie Mikutano
1 “Marafiki wowote kwenye ujirani . . . ambao wanataka kuhudhuria mikutano wanakaribishwa kwa uchangamfu.” Tangu tangazo hilo lifanywe kwenye toleo la Zion’s Watch Tower, la Novemba 1880, Mashahidi wa Yehova wamekuwa na bidii ya kualika watu wakusanyike pamoja ili kufundishwa Biblia. (Ufu. 22:17) Hiyo ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli.
2 Ni Muhimu Kuhudhuria: Tunapata baraka tunaposhirikiana na kutaniko. Tunapata kumjua vema Mungu wetu wa ajabu, Yehova. Twakutana pamoja kutanikoni ili ‘tufundishwe na Yehova.’ (Isa. 54:13) Tengenezo lake huandaa programu yenye kuendelea ya mafundisho ya Biblia ambayo hutuvuta kwake na kutuonyesha jinsi ya kutumia “shauri lote la Mungu.” (Mdo. 20:27; Luka 12:42) Mikutano hutuzoeza kuwa stadi kufundisha Neno la Mungu. Vikumbusha vya Maandiko hutusaidia kufurahia uhusiano mzuri pamoja na wengine na pamoja na Yehova mwenyewe. Kushirikiana na wale wanaompenda Yehova huimarisha imani yetu.—Rom. 1:11, 12.
3 Usikawie Kumwalika: Alika kila mwanafunzi mpya wa Biblia kwenye mikutano mara tu funzo lianzapo. Mpe kikaratasi cha kukaribisha watu kwenye mikutano. Chochea kupendezwa kwake kwa kusimulia jambo lililokutia moyo katika mkutano uliopita na utaje habari itakayozungumziwa kwenye mkutano unaofuata. Eleza Jumba la Ufalme ni nini na mahali lilipo.
4 Mwanafunzi asipokubali mwaliko wako wakati huo, endelea kumwalika tena. Tumia dakika chache kila juma kumwonyesha jinsi ambavyo tengenezo letu hufanya kazi. Tumia broshua Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini? na vidio Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name ili kumjulisha juu yetu na mikutano yetu. Andamana na wahubiri wengine kwenye funzo hilo ili apate kufahamiana nao. Katika sala yako, mshukuru Yehova kwa ajili ya tengenezo na utaje uhitaji wa mwanafunzi kushirikiana nalo.
5 Usikose kusaidia wengine wahudhurie mikutano yetu. Uthamini wao kwa Yehova uzidipo kuongezeka, watachochewa kuishi kupatana na wanayojifunza na kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu lenye umoja.—1 Kor. 14:25.