‘Twendeni Nyumbani kwa Yehova’
1 Daudi aliitikia kwa shauku mwaliko huu: “Na twende nyumbani kwa BWANA [Yehova, NW].” (Zab. 122:1) “Nyumbani” kwa Yehova, kukiwakilishwa na hekalu, kulikuwa mahali pa kukutania kwa wale waliokuwa na tamaa ya kuabudu Mungu wa kweli. Palikuwa patakatifu pa usalama na amani. Leo, kundi la Kikristo la ulimwenguni pote ni “nyumba” ya Mungu, “nguzo na msingi wa kweli.” (1 Tim. 3:15) Maandalizi yote ya wokovu yanatolewa kupitia mfereji huu. Kwa sababu hiyo, “mataifa yote yatauendea makundi makundi” ikiwa wanatamani kufurahia baraka zinazoahidiwa chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.—Isa. 2:2.
2 “Nyumbani” humo mna zaidi ya makundi 69,000 katika nchi 229. Milango ya Majumba ya Ufalme ulimwenguni pote iko wazi, kukiwa na wafanyakazi wenye bidii zaidi ya milioni nne wanaoeneza mwaliko huu: “Njoo! . . . Na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” (Ufu. 22:17) Wengi wamesikia ujumbe huu na kuuitikia kwa uthamini. Wengine wamevutiwa lakini bado hawajaja kwenye nyumba ya Yehova kwa kushirikiana na kundi la Kikristo. Watu kama hao wana ‘uhitaji wa kiroho’ unaoweza kutoshelezwa na maandalizi yapatikanayo tu katika kundi. (Mt. 5:3, NW) Tunaishi katika nyakati za hatari, na mwisho wa mfumo huu ukikaribia kasi sana. Mwelekeo baridi na wa kusitasita waweza kutokeza kukawia kwenye hatari. Ni jambo la haraka kwamba watu ‘wamkaribie Mungu’ kwa kukaribia zaidi tengenezo lake. (Yak. 4:8) Tunaweza kuwasaidiaje?
3 Elekeza Kupendezwa Kwenye Tengenezo: Kuanzia kukutana kwetu kwa mara ya kwanza na watu wenye kupendezwa, tunapaswa kuwa tukiwaelekeza fikira zao kwenye tengenezo. Ingawa huenda sisi binafsi tukaweza kupata maandiko na kueleza mafundisho ya msingi, sisi si chanzo cha ujuzi huo. Kila kitu ambacho tumejifunza kimetoka kwenye tengenezo, kupitia jamii ya mtumwa ambayo hutoa “chakula kwa wakati wake.” (Mt. 24:45-47) Kutoka mwanzoni, wapya wanapaswa kujua kuwa ibada safi yatia ndani zaidi ya sisi tu au hata kundi la wenyeji; kuna sosaiti ya ulimwenguni pote iliyopangwa kitengenezo, ya kitheokrasi, inayofanya kazi chini ya mwongozo wa Yehova.
4 Mwongozo tunaopokea hutoka kwa Yehova, ambaye ameahidi kutuongoza na kutufundisha. (Zab. 32:8; Isa. 54:13) Mafundisho hayo yanaenezwa hasa kupitia fasihi yetu. Tukiweza kusaidia wenye kupendezwa kuanza kuistahi sana fasihi yetu, wakiitambua kuwa chanzo cha mafundisho yenye kuokoa uhai, wataelekea zaidi kuisoma na kutumia ujumbe wayo badala ya kuitupilia mbali upesi. Sikuzote tunapaswa kuitoa na kuitumia fasihi hiyo katika njia ambayo hukuza staha kwayo. Hilo huwafundisha wapya wathamini tengenezo na kutegemea maandalizi yalo.
5 Julisheni wenye kupendezwa kwamba kuna mahali pakuu pa kukutania katika jumuiya hiyo ambapo mafundisho hutolewa kwa ukawaida. Waonyeshe mahali pa Jumba la Ufalme na nyakati za kukutana. Waelezee tofauti kati ya mikutano yetu na vikusanyiko vya kidini ambavyo huenda wakawa wamehudhuria wakati uliopita. Kila mmoja anakaribishwa; hakuna kukusanywa wala kuombwaombwa kibinafsi kwa fedha. Wahudumu waliowekwa wanapoongoza programu, kila mmoja ana fursa ya kutwaa sehemu kwa kutoa maelezo na kushiriki katika sehemu za programu. Familia zakaribishwa; watoto wanatiwa ndani ya mazungumzo yetu ya Biblia. Wahudumu wetu hawavai mavazi au nguo za pekee. Jumba la Ufalme limepambwa kwa njia inayopendeza na halina mishumaa, sanamu, wala mifano. Wale wanaohudhuria ni wakaaji hasa wa ujirani.
6 Elekeza Kupendezwa Hatua kwa Hatua Kwenye Mafunzo ya Biblia: Kusudi kuu la funzo la Biblia ni kufundisha kweli ya Neno la Mungu. Lapaswa pia kujenga ndani ya mwanafunzi uthamini wa tengenezo la Yehova na kumjulisha uhitaji wa maana wa kuwa sehemu yalo. Kazi kubwa iliyofanywa na Yesu na wanafunzi wake katika karne ya kwanza iliwavutia wenye moyo mweupe na kuwaunganisha kwa ajili ya kazi chini ya baraza kuu lenye kuongoza. Katika jumuiya ambamo itikio lilikuwa zuri, makundi yalianzishwa ili kutoa mazoezi na mafundisho ya kawaida. Wale waliohudhuria walitiwa nguvu kiroho, wakisaidiwa kuvumilia nyakati za dhiki. (Ebr. 10:24, 25; 1 Pet. 5:8-10) Katika siku zetu ni kusudi la Yehova ‘kuvijumlisha vitu vyote katika Kristo.’ (Efe. 1:9, 10) Kama tokeo, tuna ‘ushirika wa ndugu’ wa ulimwenguni pote.—1 Pet. 2:17, NW.
7 Funzo la Biblia la kila juma lapasa kutia ndani maagizo yatakayosaidia wanafunzi wathamini tengenezo na kutumia kwa manufaa maandalizi kwa ajili ya wokovu wao. Chukua dakika chache kila juma kusimulia au kufafanua jambo fulani juu ya tengenezo na jinsi linavyofanya kazi. Unaweza kupata mambo yenye kusaidia ya kuzungumzia katika Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1985. Zile broshua Mashahidi wa Yehova katika Karne ya Ishirini na Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote zazungumzia pande kuu za tengenezo na jinsi zinavyoweza kutunufaisha. Kufanya mipango ili wanafunzi waweze kutazama ile vidio Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name kutawasaidia wajionee wenyewe lile ambalo linatimiza. Ripoti na mambo yaliyoonwa yaliyoteuliwa kutoka kwenye Kitabu–Mwaka yaweza kuonyesha mafanikio ya kazi katika nchi na tamaduni nyingine kuliko zetu wenyewe. Vichapo vingine vyaweza kutumiwa pia. Baada ya kipindi fulani cha wakati, eleza hatua kwa hatua mambo kama vile kwa nini sisi huenda nyumba kwa nyumba, kusudi la mikutano yetu, jinsi kazi yetu inavyogharimiwa, na utendaji wetu wa ulimwenguni pote.
8 Kufahamiana na Mashahidi wengine kwaweza kuwa na tokeo la kuwachochea wapya, kukipanua maoni yao juu ya kundi. Kwa hiyo, wakaribishe wahubiri wengine wahudhurie funzo hilo mara kwa mara. Mtu fulani katika kundi mwenye malezi kama yake au upendezi kama wake huenda akapanua zaidi maoni ya mwanafunzi wako. Labda mzee anaweza kuandamana nawe ili wafahamiane tu. Kupanga kwenda na mwangalizi wa mzunguko au mke wake kwaweza kuthibitika kuwa baraka kwelikweli. Ikiwa kuna Mashahidi wanaoishi karibu na hapo, kuwafahamisha kwa mwanafunzi wa Biblia kwaweza kutoa kitia-moyo zaidi kwa mwanafunzi cha kuhudhuria mikutano ya kundi.
9 Tia Moyo Wapya Waje Kwenye Mikutano: Wapya wanahitaji kutambua jinsi lilivyo jambo la maana kuhudhuria mikutano. Jaribu kuchochea kupendezwa kwao. Onyesha makala zitakazozungumzwa katika funzo la Mnara wa Mlinzi. Taja vichwa vya hotuba zinazokuja. Simulia mambo makuu ya sehemu itakayotimizwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Funzo la Kitabu la Kundi. Onyesha hisia zako mwenyewe juu ya yale unayojifunza kwenye mikutano na kwa nini unahisi uhitaji wa kuhudhuria. Ikiwa unaweza, toa usafiri. Kumpigia simu kabla ya mikutano kwaweza kutoa kichocheo zaidi cha kuhudhuria.
10 Mwanafunzi wa Biblia anapokuja mkutanoni, mfanye ahisi kuwa amekaribishwa. Mjulishe kwa wengine, kutia ndani wazee. Ikiwa anahudhuria hotuba ya watu wote, mjulishe kwa msemaji. Mwonyeshe Jumba la Ufalme lote. Mweleze kusudi la meza za fasihi na magazeti, visanduku vya mchango, maktaba, na andiko la mwaka. Mjulishe kuwa jumba hilo si nyumba ya ibada tu bali pia ni kitovu ambacho kutoka kwacho kazi ya kuhubiri hupangwa.
11 Eleza jinsi mikutano yetu huongozwa. Mwonyeshe mwanafunzi vichapo tunavyotumia. Eleza kwamba Biblia ndicho kitabu chetu kikuu cha mafundisho. Kila mtu aweza kushiriki, kutia ndani watoto. Eleza kwamba muziki wote na maneno ya nyimbo katika kitabu chetu cha wimbo yalitungwa na Mashahidi wa Yehova ili yatumiwe katika ibada yetu. Elekeza fikira kwenye unamna-namna wa malezi ya wale wanaohudhuria. Toa maelezo chanya juu ya roho ya urafiki na ukaribishaji-wageni. Kupendezwa huko kwenye fadhili, na moyo mweupe kwaweza kuwa mojapo ya mambo yenye nguvu zaidi katika kumchochea mwanafunzi arudi tena.
12 Kwa Nini Wengine Huenda Wakawa Wanakawia: Mara nyingi, licha ya yote ufanyayo, wengine husitasita kukaribia tengenezo. Usikate tamaa upesi. Jaribu kujiweka katika hali yao. Kufikia sasa, hawajahisi uhitaji wa kuhudhuria ibada za kidini isipokuwa kwenye pindi za pekee. Huenda ikawa wanabanwa na familia au marafiki wa karibu. Huenda ikawa wanahofu majirani ambao husema maneno ya dharau. Na bila shaka, huenda wakawa na vikengeusha fikira mbalimbali vinavyohusiana na shughuli za kijamii na za kitafrija. Huenda wakaona hayo kuwa vizuizi vikubwa sana; unapaswa kuwasaidia waone mambo ifaavyo na ‘kuhakikisha mambo ya maana zaidi.’—Flp. 1:10, NW.
13 Toa sababu za Kimaandiko za kuvumilia. Kazia kwamba sisi sote twahitaji sana kitia-moyo na kujengwa kiroho tunakopata katika ushirika wetu pamoja. (Rum. 1:11, 12) Yesu alionyesha wazi kwamba upinzani wa familia si sababu halali ya kutuzuia. (Mt. 10:34-39) Paulo alitusihi tusiwe na aibu kujitambulisha hadharani kuwa wanafunzi wa Yesu. (2 Tim. 1:8, 12-14) Shughuli za kibinafsi na vikengeusha fikira vyapasa kudhibitiwa; la sivyo, vinakuwa mtego. (Lk. 21:34-36) Wale wanaostahiki baraka ya Yehova wanapaswa kujitoa kwa nafsi yote, si kwa moyo-nusu. (Kol. 3:23, 24) Kukaza kikiki uthamini huo wa kanuni za Biblia kwaweza kuwafungulia njia ya kufanya maendeleo kiroho.
14 Milango Iko Wazi: Nyumba ya Yehova ya ibada ya kweli imekwezwa juu ya nyinginezo zote. Mwaliko huu unatolewa katika nchi 229 ulimwenguni pote: “Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA [Yehova, NW], . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.” (Isa. 2:3) Wapya wanapoitikia ifaavyo maisha zao zaweza kuokoka. Kuelekeza kupendezwa kwao kwenye tengenezo la Yehova ni mojawapo njia bora zaidi tuwezayo kuwasaidia.