Kutoa Habari Njema Kwa Kutumia Kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
1 Muda wa miaka ambayo imepita, karibu kila kimoja cha vichapo vyetu kimegusa katika njia fulani juu ya maisha na huduma ya Yesu Kristo. Hilo lafaa sana, kwani “hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.” (Matendo 4:12) Kitabu hicho ni cha pekee kwa habari ya kwamba ni mara ya kwanza kwa kimojapo vitabu vyetu kukazia hasa maisha ya Yesu.
2 Kukitoa kwa Wengine: Ni zipi baadhi ya sehemu zenye kupendeza katika kichapo hicho tunazoweza kutokeza? Sura ya 5 hutokeza swali linalofaa kwa wakati huu wa mwaka, “Kuzaliwa kwa Yesu—Wapi na Wakati Gani?” Waweza kunasa kupendezwa kwa kijana kwa ule usimulizi wenye kusisimua katika sura 44, “Kunyamazisha Dhoruba Inayotisha.” Mtu mwenye ugonjwa au udhoofu wa kimwili kwa hakika angefarijiwa na sura 57, “Huruma kwa Wanaosumbuka.” Sura 90, “Tumaini la Ufufuo,” lapasa kuvutia mtu yeyote ambaye amepata kuomboleza kifo cha mpendwa. Mazungumzo kuhusu hali za ulimwengu zenye kutaabisha yaweza kuongoza kwenye sura 111, “Ishara ya Siku za Mwisho.”
3 Waweza kusema hivi mlangoni: “Mungu hututazamia tufanye nini tukiwa Wakristo? Biblia hutuelekeza tuige kielelezo kilichowekwa na yule mtu mkuu zaidi ulimwenguni, Yesu Kristo. [Soma 1 Petro 2:21.] Aliwafundisha wafuasi wake wawapende majirani wao, waendelee kuwa safi kiadili, na kusali kuhusu kuja kwa Ufalme wa Mungu. Wokovu wetu wategemea kutambua na kutii Yesu akiwa Mwokozi wetu. [Soma Yohana 14:6.] Yesu hakuwa mtu wa kawaida. Kitabu hiki kinamfafanua kuwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi. Sura 59 inathibitisha hilo, ikimtambulisha kuwa ‘Kristo, yule Mwana wa Mungu anayeishi.’ Kwa kuwa tunamtegemea ili kupata wokovu, je, huhisi tunahitaji kujifunza mengi kadiri tuwezavyo juu ya kazi yake na yale aliyofundisha? Kitabu hiki kimetayarishwa hasa kwa kusudi hilo, na ningefurahia kukutolea nakala hii.”
4 Yaelekea utapata kwamba watu wengi wenye moyo mweupe watakubali na kusoma kitabu hicho. Hakikisha kufuatia maangusho yako yote. Katika visa vingine huenda ukaamua kutumia kitabu hicho ili kuanzisha mafunzo ya Biblia nyumbani. Kitakuwa kizuri hasa kwa funzo la familia na kwa mafunzo yanayoongozwa pamoja na vijana.
5 Wekea Msingi Ziara Nyingine: Bila shaka, iwe tumeacha trakti, kitabu Mtu Mkuu Zaidi, au fasihi nyingine au kuwa na mazungumzo mazuri tu, twaweza kusema hivi: “Ninapokuja mara nyingine, ningependa kushiriki na wewe jambo la hakika lenye kupendeza kuhusu jiji ambako Yesu alizaliwa.” Hakikisha kuandika kwa uangalifu ziara hiyo na kupendezwa kunakoonyeshwa.
6 Ufalme unaitolea ainabinadamu tumaini pekee la kweli. Acheni tuonyeshe tamaa yetu yenye bidii ya kushiriki pamoja na wote tunaokutana nao “[maarifa sahihi ya, NW] siri ya Mungu, yaani Kristo.”—Kol. 2:2.