Tafuta Mafunzo ya Biblia kwa Bidii
1 Kuna ushuhuda wenye kuongezeka kwamba wakati unapungua kwa ulimwengu huu wa kale. (2 Tim. 3:1-5) Hilo lamaanisha nini? Lamaanisha kwamba maisha ya watu yamo hatarini. Hata hivyo, tunaweza kuwasaidia waokolewe. (Mit. 3:27) Kwa kusudi hili, twapaswa kujitahidi sana kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia.
2 Mengi mazuri yametimizwa kwa kugawanywa kwa fasihi yetu yenye msingi wa Biblia. Lakini watu wanahitaji sana msaada wa kibinafsi kupitia funzo la Biblia nyumbani linaloongozwa kwa ukawaida. Twaweza kuwasaidiaje waone uhitaji huo?
3 Tunaweza kuuliza maswali yanayowahusu watu wengi. Maswali hayo yangeweza kukazia juu ya kwa nini maadili yameshuka sana, kwa nini maisha ya familia yamo katika hali mbaya, kwa nini jeuri na uhalifu ni tisho hivyo, kwa nini Mungu mwenye upendo ameruhusu hali za sasa na kadhalika. Uwe macho kwa masuala na matukio yanayowapendeza watu katika eneo lenu. Elekeza kwa majibu ya Biblia yaliyo wazi kwa maswali hayo. Onyesha jinsi fasihi tunayogawanya yaweza kuwasaidia wajifunze yale Biblia husema kuhusu mambo hayo na mambo mengine ya maana yanayotuathiri sisi sote.
4 Ni jambo la maana kumvuta mwenye nyumba kwenye mazungumzo. Uwe chonjo kutambua kinachomhusu yeye. Sitawisha mazungumzo yako kwenye mapendezi au mahangaiko yake. Elekeza kwenye habari iliyo katika kitabu, broshua, gazeti, au trakti ambayo inaeleza utatuzi wa Biblia kwa matatizo ya ainabinadamu. Kabla hujaondoka, uliza swali moja au mawili ambayo unaamini yataamsha hamu yake kwa ziara yako ifuatayo. Unaporudi, hakikisha umemkumbusha maswali hayo, na kisha utumie fasihi kumsaidia kupata majibu ya Biblia.
5 Kuanzisha kwetu mafunzo na kuyaongoza kwa ukawaida kwaweza kubadili maisha ya watu. Tunahitaji kuonyesha kupendezwa halisi kwa mahangaikio ya wale tunaokuta katika shamba au vikao vya vivi-hivi. Inahitaji utayarishaji mzuri ili kuchochea kupendezwa kwao kwa kuendelea. Inahitaji subira ili kuendelea kurudi tena mpaka uwaweke katika hali ya ulishaji wa kawaida wa kiroho. Inahitaji kupendezwa kwa upendo na watu wenyewe. Tunapaswa kutaka kuwasaidia kwa unyoofu waokolewe kutokana na uharibifu unaokuja. Kazi yetu ya mafunzo ya Biblia yapaswa kuwa jambo la ukawaida na la sala yenye bidii.—1 The. 5:17.
6 Inatia moyo kuona kwamba karibu watu milioni moja wamekuwa wanafunzi waliobatizwa katika miaka mitatu iliyopita. (Mt. 28:19, 20) Sasa tunaongoza mafunzo ya Biblia karibu milioni nne na nusu kila mwezi, na hilo laonyesha hangaikio letu kwa uhai wa wengine. Namna gani wewe? Je! umekuwa ukijitahidi kushiriki katika kazi ya mafunzo ya Biblia nyumbani? Kumbuka, maisha yetu na ya wale wengine yanategemea uaminifu wetu kwa jambo hilo.—Eze. 3:17-19.