Sanduku La Swali
◼ Ni tahadhari gani inayohitajiwa tunapohubiri maeneo hatari?
1 Kwa kuongezeka, twasikia ripoti za jeuri, uvunjaji, na vurugu ya kijamii, hasa katika maeneo ya mijini. Ingawa twahisi tukiwa na hangaiko, twajua kwamba hata katika maeneo yasiyo na utulivu kuna watu wenye moyo mnyoofu, watakaoitikia ujumbe wa Ufalme. Kwa hiyo kwa wakati unaofaa, twapaswa kuwa na ujasiri wa kusonga mbele, tukiwa na uhakika na utunzi wa Yehova.—Mit. 29:25; 1 The. 2:2.
2 Tunapoenda kwenye eneo linalokadiriwa kuwa na hatari, Yehova hututazamia tuwe wenye kutahadhari na tutumie uamuzi mzuri. Uwe chonjo. “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.” (Mit. 22:3) Wahubiri wenye ustadi wanathamini hekima ya kuhubiri pamoja na wengine wakiwa wawili wawili au katika vikundi vya wahubiri kadhaa, ikiwa ni lazima. Mhubiri 4:9, 12 husema: “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja . . . Hata ikiwa mtu aweza kushinda yule aliye peke yake, wawili watampinga.” Wahalifu hutafuta wale walio peke yao na hivyo rahisi kushambulia.
3 Usibishane na wale wanaoweza kuonekana kuwa wenye kutisha au kushindana. Uwe mwepesi kujitambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wahubiri fulani hubeba Biblia au gazeti Mnara wa Mlinzi au Amkeni! mikononi mwao kwa kusudi la utambulisho.
4 Watupie jicho watu mmoja-mmoja wanaozurura kwenye eneo hilo. Tahadhari unapoingia lifti pamoja na watu wasioonekana kuwa wenyeji wa jengo hilo. Usivae vito vya thamani vyenye bei mno. Ikiwa ni lazima uwe nje baada ya giza kuingia, epuka kutembea kwenye barabara zilizo na giza ambapo kuna magari ya usafiri machache. Ikiwa umepatwa na wanyang’anyi, usikinze ikiwa tu ni pesa au mali zako wanazotaka; uhai wako ni wenye thamani zaidi ya kitu chochote cha kimwili ulicho nacho.—Mk. 8:36.
5 Ndugu wanaoongoza wanahitaji kuwa chonjo, wakijua pale wahubiri wapo katika eneo. Kwa kawaida ni vizuri kufanya kikundi kishughulike sana na eneo hilohilo ili wengine wawe karibu sikuzote. Jeuri ya aina yoyote au msukosuko ukitokea katika ujirani, kikundi chapaswa kuondoka eneo hilo mara moja.
6 Tukiwa chonjo na wenye tahadhari, twaweza kuendelea kuwafikia wale walio kwenye maeneo yenye jeuri sana “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika.”—Eze. 9:4.