‘Toa Ushahidi Kamili’—Kwa Kuhubiri Katika Nyumba za Ghorofa Zenye Wapangaji
1. “Kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema” kunatia ndani nini?
1 Kama mtume Paulo, tunatamani “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema.” (Mdo. 20:24) Kwa hiyo, tunajitahidi kuwatangazia ujumbe wa Ufalme watu wengi iwezekanavyo katika eneo letu, kutia ndani watu wengi wanaoishi katika nyumba za ghorofa zenye wapangaji. Nyakati nyingine, inaweza kuwa vigumu kuruhusiwa kuwatembelea watu wanaoishi katika majengo hayo. Hata hivyo, kwa kuwa majengo hayo yana watu wengi sana, tunaweza kupata nafasi nyingi zaidi za kueneza habari njema.
2. Kwa nini busara na hekima inahitajiwa tunapohubiri katika nyumba za ghorofa zenye wapangaji?
2 Kwa sababu ya hatari ya uhalifu na jeuri, nyumba nyingi za ghorofa zenye wapangaji zinafungwa na zina walinzi au kamera za ulinzi. (2 Tim. 3:1, 2) Huenda wasimamizi wakaweka sheria ya kwamba watu ambao hawajaalikwa hawaruhusiwi kuingia humo. Msimamizi au mtunzaji wa jengo anaweza kutuomba tuondoke, hasa ikiwa mpangaji fulani analalamika. Kwa hiyo, ni muhimu kutumia busara na hekima.
3. Ni wakati gani mzuri wa kuhubiri katika nyumba za ghorofa zenye wapangaji, na kwa nini?
3 Wakati wa Kuhubiri: Kama ilivyo katika maeneo mengine, ni vizuri kuhubiri katika majengo hayo wakati ambapo wakaaji wanaweza kupatikana nyumbani. Huenda watu wakaanza kutushuku tukiingia wakati ambapo wapangaji wengi hawapo. Wahubiri wengi wamefanikiwa kuwapata watu nyumbani mapema saa za jioni na pia Jumamosi na Jumapili alasiri. Kuhubiri majengo hayo asubuhi sana, hasa mwishoni mwa juma, kunaweza kuwafanya wasimamizi walalamike.
4, 5. Tunaweza kuingiaje katika majengo ambayo yana lango linalofungwa?
4 Kuingia Katika Majengo: Wahubiri hawapaswi kuwasiliana na msimamizi au mfanyakazi mwingine wa majengo hayo kabla ya kushiriki katika huduma. Ikiwa jengo lililofungwa lina simu kwenye lango la kuingilia, tunaweza kuitumia kumtafuta mtu ambaye angependa tuingie na kuzungumza naye. Ikitegemea aina ya jengo, tunaweza kuhubiri nyumba kwa nyumba ndani ya jengo hilo baada ya kuzungumza na mpangaji aliyeturuhusu tuingie. Hata hivyo, nyakati nyingine ni jambo la hekima kutoka katika jengo na kutumia simu iliyo langoni kuzungumza na mkaaji mwingine. Tunapaswa kutumia busara tunapoamua idadi ya wapangaji tutakaozungumza nao kwa njia hiyo katika pindi hiyo.
5 Huenda wapangaji wengine wakataka uwaambie kusudi la kuwatembelea kupitia simu iliyo langoni. Wakisema hivyo, jitambulishe kwa njia ya urafiki. Mwite mwenye nyumba kwa jina lake ikiwa linajulikana. Taja kwa ufupi habari unayozungumzia. Baadhi ya wahubiri wamefanikiwa kwa kusoma utangulizi fulani moja kwa moja kutoka katika kitabu Kutoa Sababu.
6. Tunapaswa kufanya nini tunapohubiri katika majengo yenye mlinzi?
6 Ikiwa jengo lina mlinzi ambaye haturuhusu tuhubiri katika nyumba za watu, tunaweza kumhubiria. Walinzi wengi wanapenda kusoma vitabu vyetu. Huenda hata tukafaulu kuanzisha funzo la Biblia na kuliongoza langoni. Mlinzi akituruhusu kumtembelea mpangaji fulani ambaye anapendezwa, kwa kawaida si vizuri kutumia nafasi hiyo kubisha milango mingine katika jengo hilo.
7. Tunapaswa kuzingatia nini kuhusu mfuko au mkoba wetu wa mahubiri?
7 Sura na Tabia Nzuri: Kubeba mifuko au mikoba mikubwa sana kunaweza kuwafanya watu watukazie fikira. Kwa hiyo, tunaweza kubeba mfuko au mkoba mdogo au kutobeba mkoba wowote. Wahubiri fulani wanabeba kitabu cha toleo katika faili ndogo na wanabeba Biblia mkononi au katika mfuko wa nguo.
8. Vikundi vinapaswa kupangwaje vinapohubiri katika nyumba za ghorofa zenye wapangaji?
8 Si vizuri kukusanyika katika vikundi vikubwa, hasa katika eneo la mapokezi, maegesho, au barabarani, kwa kuwa watu watatukazia uangalifu isivyo lazima. Tunapaswa kuchukua tahadhari zinazofaa tunapohubiri majengo yaliyo katika maeneo yenye wahalifu wengi. (Met. 22:3) Kwa mfano, vikundi viwili au vitatu vya wahubiri wawili-wawili vinaweza kuhubiri kwenye ghorofa ileile karibu-karibu. Kikundi kimoja kinaweza kubisha mlango huku kikundi kingine kikingoja.
9. Tunaweza kuonyeshaje adabu nzuri, na kwa nini ni muhimu kufanya hivyo?
9 Mnapoingia katika jengo, panguseni viatu na mfunge mlango ifaavyo. Tunapoonyesha adabu nzuri, wapangaji hawatakuwa na sababu ya kulalamika. Mnapokuwa ndani ya jengo, elekeeni moja kwa moja kwenye ngazi au kwenye sehemu ya ghorofa ambayo mtahubiri badala ya kuzurura-zurura karibu na lango. Hilo litawazuia watazamaji wasiwashuku.
10. Tunaweza kuepukaje kupiga kelele isivyo lazima ndani ya majengo?
10 Katika nyumba nyingi za ghorofa, kelele husambaa kwenye vijia. Kwa hiyo, usizungumze kwa sauti kubwa sana ambayo itamsumbua mwenye nyumba. Unapozungumza na wahubiri wengine, zungumza kwa sauti ya chini, kwa utulivu, na kwa kiasi ili watu wasiwashuku. Ili kuepuka kuwasumbua wapangaji, baadhi ya wahubiri wanahubiri upande mmoja wa ghorofa na kwenda upande wa pili mpaka wanapomaliza nyumba zote, badala ya kubisha mlango mmoja baada ya mwingine kwa kufuatana. Isitoshe, kubisha mlango kwa nguvu au kwa kishindo kunaweza kuwaogopesha watu walio ndani.
11. Ni mapendekezo gani yanayoweza kutusaidia tunapobisha mlango wenye tundu la kumtazama aliye nje?
11 Ikiwa mlango una tundu la kumtazama aliye nje, simama mahali ambapo mtu aliye ndani anaweza kukuona wewe na mwenzako. Simama mbele ya tundu hilo, na ukigundua kwamba kuna mtu anayekutazama, msalimu kwa uchangamfu na utoe utangulizi wako. Mtu huyo akikuuliza, ‘Wewe ni nani?’ ni vizuri kumwambia jina lako na la mhubiri mwenzako. Huenda mwenye nyumba akatulia na kufungua mlango. Hata asipofungua, bado unaweza kumhubiria.
12. Tunaweza kuepukaje matatizo tunapoacha vichapo katika nyumba ambazo hazina watu?
12 Nyumba Ambazo Hazina Watu: Watunzaji wengi wa majengo hayo wanalalamika kwamba wanalazimika kuokota vichapo ambavyo vimetupwa kwenye vijia au uani. Vichapo vinavyoachwa nje ya mlango vinaweza kwa urahisi kuanguka sakafuni na kuwa takataka. Kwa hiyo, kichapo chochote ambacho kinaachwa kwenye nyumba ambazo hazina watu kinapaswa kuwekwa mahali ambapo hakionekani kamwe.
13. Tunapaswa kufanya nini tukimkuta mwenye nyumba aliyekasirika?
13 Wenye Nyumba Waliokasirika: Tukikutana na mwenye nyumba ambaye anatisha kumuita mtunzaji wa jengo, ni vizuri kuondoka kwenye ghorofa hiyo na kurudi wakati mwingine. Nyakati nyingine, ni jambo la hekima kuondoka kabisa kwenye jengo hilo ili kuepuka ugomvi na mtunzaji. Hata ikiwa mwenye nyumba hakatai kutembelewa wakati ujao, ni vizuri kuandika namba ya nyumba au ghorofa anamoishi na kueleza kwamba hataki kutembelewa, kisha uweke habari hizo kwenye ramani ya eneo hilo. Kama inavyokuwa kuhusiana na watu ambao hawataki kutembelewa, watu hao wanapaswa kuulizwa mara kwa mara ikiwa wamebadili maoni yao.
14, 15. Tunapaswa kufanya nini tukiombwa tuondoke na msimamizi wa jengo fulani?
14 Ukiombwa Uondoke: Ikiwa wakati unapohubiri katika jengo fulani unaombwa uondoke na mtunzaji, mlinzi, mdumishaji, au msimamizi mwingine wa jengo hilo, ni jambo la hekima kutii mara moja. Kadiri iwezekanavyo, tunataka kuepuka ugomvi na vitisho vya kwamba tutachukuliwa hatua ya kisheria au polisi wataitwa. Kwa kawaida, wafanyakazi wa majengo hayo hawawachukii Mashahidi wa Yehova lakini wanafanya tu kazi yao.
15 Nyakati nyingine, msimamizi wa jengo fulani anapokuomba uondoke, unaweza kumweleza kwa fadhili na busara sababu ya ziara yako. (1 Pet. 3:15) Tunatambua kwamba ana daraka la kuhakikisha kwamba wapangaji hawasumbuliwi na kudumisha ulinzi katika jengo hilo. Labda anaweza kukuruhusu uendelee kuwatembelea wapangaji. Lakini akikataa, ondoka kwa upole. Ikiwa hali zinaruhusu, unaweza kumwomba idhini ya kuleta vichapo kwa ukawaida katika sehemu ya mapokezi au ofisini. (Kol. 4:6) Mwangalizi wa utumishi anapaswa kujulishwa mara moja hali kama hizo.
16. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunaendelea kukabili matatizo tunapojaribu kuhubiri katika jengo fulani la kupanga?
16 Labda, baada ya muda fulani kupita, wahubiri wanaweza kujaribu kwa busara kuhubiri katika jengo hilo tena. Hata hivyo, wakiendelea kukabili matatizo, wazee wanapaswa kuwasiliana na ofisi ya tawi na kuomba msaada badala ya wahubiri kujaribu kutatua matatizo hayo kwa njia yao. Wahubiri wakishindwa kabisa kuhubiri jengo fulani, wanaweza kujaribu kuwahubiria wapangaji kwa njia nyingine, kama vile kwa simu au barua. Wahubiri fulani huhubiri barabarani mbele au karibu na jengo hilo saa za asubuhi na jioni wakati ambapo watu wengi wanaenda kazini au kurudi nyumbani.
17. Kwa nini ni muhimu kuhubiri katika nyumba za ghorofa zenye wapangaji?
17 Mwisho wa mfumo huu mwovu u karibu sana. Ni wale tu wanaoliitia jina la Yehova ndio watakaookolewa. “Hata hivyo, watawezaje kumwitia yeye ambaye hawajamwamini? Nao watamwaminije yeye ambaye hawajamsikia?” (Rom. 10:13, 14) Watu wengi wenye “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” wanaishi katika nyumba za ghorofa zenye wapangaji. (Mdo. 13:48) Tukitumia busara na hekima, tunaweza kuwahubiria habari njema.