Kudumisha Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Tekinolojia ya Kompyuta
1 Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo katika karne ya kwanza wasikengeushwe fikira, kwa sababu “muda ubakio si mwingi.” (1 Kor. 7:29) Mwisho wa mfumo huu wa kale wa mambo ukaribiapo, ni jambo la haraka kama nini kwetu sisi ‘kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu’ na ‘kukomboa wakati’! Wakati ni wenye thamani.—Mt. 6:33, NW; Efe. 5:15, 16.
2 Tekinolojia imesifiwa kuwa jambo lenye kuokoa wakati sana. Kwa kielelezo, kwa kubonyeza ufunguo wa kompyuta, mwenye kuitumia aweza kupata habari nyingi sana mara iyo hiyo. Mara nyingi kompyuta zaweza kufanya kwa sekunde chache jambo ambalo lingalichukua saa au majuma kadhaa kufanya kwa njia nyingineyo. Zinapotumiwa vizuri, hizo ni vyombo vyenye kusaidia.
3 Je, Kweli Itaokoa Wakati?: Kwa upande mwingine, tekinolojia hiyo haipatikani kwa mtu anayeitumia bila kuwa na gharama kubwa—ya fedha na pia ya wakati. Saa nyingi huenda zikatakiwa ili kujifunza jinsi ya kufanya kompyuta itimize kazi fulani. Zaidi ya hayo, mtu anayesisimuliwa na tekinolojia hiyo yenyewe aweza kumaliza wakati ambao ungeweza kutumiwa kwa njia bora zaidi. Ni lazima tudumishe maoni yenye usawaziko, tukikumbuka kanuni inayohusika katika onyo la Paulo lenye upole la kutembea ‘kama watu wenye hekima, tukikomboa wakati.’—Ona 1 Wakorintho 7:31.
4 Watu kadhaa wenye nia njema wamebuni programu za kompyuta ili kuweka rekodi za kutaniko. Bila shaka, jinsi mtu atumiavyo kompyuta yake ni uamuzi wa kibinafsi. Hata hivyo, rekodi za kutaniko ambazo fomu zimeandaliwa kwa ajili yazo hazipasi kuwekwa katika kompyuta, kwa kuwa watoto au watu wengine wasioruhusiwa wangeweza kuzifikia. Rekodi zote za kutaniko—rekodi za hesabu, kadi za Maandishi ya Mhubiri, na kadhalika—zapaswa kuwekwa kwenye fomu zilizoandaliwa na Sosaiti, na habari kwenye fomu hizi za kutaniko hazipaswi kuhifadhiwa katika kompyuta. Katika njia hii, rekodi za siri za kutaniko zitalindwa.
5 Waangalizi wenye kuchukua madaraka wapaswa kuwa na utambuzi katika kutoa migawo kwa ajili ya programu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na ya Mkutano wa Utumishi. Wanahitaji kufikiria habari itakayozungumziwa katika sehemu fulani. Kwa kielelezo, katika shule habari nyingine huenda ikawa haifai kushughulikiwa na mwanafunzi yeyote yule. Kusudi la utoaji na pia sifa za ustahili za mtu mmoja-mmoja na namna ya habari yapasa kufikiriwa. Kompyuta haipaswi kuachwa kuamua mambo hayo.
6 Ndugu anayegawiwa sehemu itakayotolewa kwenye mikutano ya kutaniko hapaswi kutegemea habari iliyotayarishwa na mtu mwingine, hasa mtu asiyemjua, kwa sababu tu imeandaliwa kwenye mfumo wa kompyuta na kuitumia kutampunguzia kazi. Wakristo wenye kuchukua daraka hawafanyi kimbelembele kutayarisha hotuba za Biblia au sehemu za mkutano na kuziweka katika mifumo ya kompyuta ili zipatikane kwa wengine na kutumiwa. Hata hivyo, kompyuta na Watchtower Library ya Sosaiti kwenye CD-ROM vyaweza kuwa vyombo vyenye thamani mikononi mwa ndugu mmoja-mmoja, vikichangia utafiti wenye matokeo katika wakati mfupi unaopatikana.
7 Kwa habari ya kunakili na kugawa miongoni mwa akina ndugu programu za kompyuta, orodha na habari inayohusiana na hiyo, na kutayarisha na kugawa sehemu za Mkutano wa Utumishi na za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kupitia kompyuta au njia nyinginezo, kwa kawaida ni afadhali kwa akina ndugu kutayarisha habari yao wenyewe, wakifikiria manufaa za mahali pao. (1 Tim. 4:13, 15) Mambo ya kikutaniko hayapaswi kwa vyovyote vile kutumiwa vibaya ili kupata faida ya kifedha.
8 Namna gani ugawaji wa nakala zilizochapishwa kwa kompyuta za maandiko yanayotumiwa katika Funzo la Mnara wa Mlinzi au katika Funzo la Kitabu la Kutaniko? Yaweza kufaa zaidi kwa wahubiri kuandika maandishi yao na kutia alama zao humo humo katika Biblia na vichapo vinavyotumiwa kwa mafunzo. Kutumia mkutanoni nakala zilizochapishwa za Maandiko ambayo yametajwa katika vichapo kungeweza kuzuia matumizi ya Biblia yenyewe katika kutafuta maandiko. Hata hivyo kufungua Maandiko wakati wa Funzo la Biblia au kwenye mkutano wa kutaniko ni sehemu ya mazoezi yanayopokewa, yakitutayarisha kwa ajili ya matumizi ya Biblia yenye matokeo katika huduma ya shambani. Katika hali zilizo nyingi, hasa kukiwa na manukuu marefu zaidi, kusoma moja kwa moja kutoka kwenye Biblia ni jambo lenye matokeo zaidi, na hasa wakati wasikilizaji wanatiwa moyo kufuatia katika Biblia.
9 Mitego Mingine Yenye Uzito: Kama ilivyoonyeshwa kwenye ukurasa 17 wa toleo la Agosti 1, 1993, la Mnara wa Mlinzi, kuunganisha kompyuta na mfumo wa simu uliounganishwa na kompyuta nyinginezo kwaweza kufungulia njia hatari za kiroho zenye uzito. Kama vile mtu mbaya awezavyo kutia virusi—programu iliyobuniwa ili kufisidi na kuharibu faili za kompyuta—katika mfumo wa simu uliounganishwa na kompyuta, waasi-imani, makasisi, na watu wanaojaribu kufisidi wengine kiadili au vinginevyo waweza kwa uhuru kutia mawazo yao yenye sumu katika mifumo hiyo. Isipokuwa kama mfumo wa simu wenye kuunganishwa na kompyuta, hata mmoja uitwao “MY [Mashahidi wa Yehova] pekee,” unasimamiwa ifaavyo, matumizi yao yakizuiwa kwa wale tu ambao ni watumishi wa Yehova waaminifu, walio wakomavu, huo ungeweza kuweka Wakristo wanaoutumia katika “mashirika mabaya.” (1 Kor. 15:33, NW) Sosaiti imepokea ripoti kwamba mifumo hiyo iitwayo eti ya faragha imetumiwa ili kukisia kuhusu mambo ya kiroho na pia kutoa mashauri mabaya, kueneza porojo na habari ya uwongo, kuingiza kisiri mawazo yasiyofaa, kutokeza maswali na shaka zinazopindua imani ya wengine, na kueneza mafafanuzi ya kibinafsi juu ya Maandiko. Kijuujuu, habari fulani huenda ikaonekana kuwa yenye kupendeza na yenye kuarifu, na hata hivyo huenda ikawa imefungamanishwa na mambo yenye sumu. Wakristo hutegemea “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ili kupata chakula cha kiroho cha wakati unaofaa na ili kupata maelezo ya wazi. (Ona Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1994, kurasa 9-11.) Mkristo ana daraka lenye uzito la kulinda imani yake dhidi ya uvutano wote wenye kufisidi na, jambo la msingi kuhusiana na hilo ni kwamba, yeye apaswa sikuzote kujua ni nani anayeshirikiana naye.—Mt. 24:45-47; 2 Yohana 10, 11.
10 Mnara wa Mlinzi uo huo ulikazia umaana wa kustahi sheria za haki ya uchapaji. Kampuni zilizo nyingi zinazotayarisha na kuuza programu za kompyuta huhifadhi haki zazo za uchapaji, nazo huandaa leseni zikionyesha jinsi programu hizo zaweza kutumiwa kisheria. Kwa kawaida leseni husema kwamba mwenyeji hawezi kuwapa wengine nakala za programu hiyo; kwa kweli, sheria ya haki ya uchapaji ya kimataifa hufanya iwe haramu kufanya hivyo. Watu wengi wenye pupa hawaoni vibaya kuvunja sheria. Lakini Wakristo wanapaswa wawe wenye kudhamiria katika mambo ya kisheria, wakimpa Kaisari yaliyo ya Kaisari.—Mt. 22:21; Rum. 13:1.
11 Kampuni fulani kubwa zinauza kompyuta zenye programu zilizowekwa ndani kimbele na kupewa leseni. Hata hivyo, maduka fulani ya kompyuta hayatoi leseni kwa sababu programu ambazo yanaweka ndani kimbele ni nakala haramu, hiyo ikimaanisha kwamba mwenye kununua anakiuka sheria kwa kutumia programu hizo. Kuhusiana na hili, Wakristo wapaswa kuepuka kuingiza katika, au kunakili kutoka katika mifumo ya simu iliyounganishwa na kompyuta, habari ya kielektroni ambayo haki zayo za uchapaji zimehifadhiwa (kama vile vichapo vya Sosaiti) na ambayo inanakiliwa bila ruhusa ya kisheria kutoka kwa wenyeji.—Ebr. 13:18.
12 Thamani ya matumizi yoyote ya tekinolojia ni lazima ipimwe dhidi ya hatari ziwezazo kutokea zinazohusiana na matumizi yayo. Kama vile televisheni iwezavyo kutumiwa kwa manufaa mazuri, matokeo yasiyofaa ambayo inakuwa nayo juu ya wanadamu leo yamesababisha hata vyanzo vya kilimwengu vionyeshe hangaiko lenye uzito. Mifumo ya kompyuta huenea ulimwenguni pote na yaweza kuleta habari yenye thamani isiyo na kikomo nyumbani na kazini. Inatoa huduma nyingi zinazohitajiwa sana kwa biashara na mashirika na pia kwa watu mmoja-mmoja wanaohitaji kwenda sambamba na masilahi ya kibinafsi na ya kibiashara katika jamii tunamoishi inayosonga mbele upesi. Wakati uo huo, mifumo ya kompyuta inakumbwa na matatizo kama vile ponografia, propaganda za chuki zenye kugawanya, na habari yenye mambo mengi kuhusu jinsi ya kufanya matendo mabaya na maovu.
13 Kwa hiyo, kuna sababu nyingi za maana kwa nini ni lazima Mkristo adumishe maoni yenye usawaziko kuhusu tekinolojia ya kompyuta. Watu wengi mmoja-mmoja wanafurahia New World Translation, mabuku ya Insight, na programu ya GetVerse, ambazo Sosaiti imeandaa kwenye disketi. Wengine wamenufaika kwa kutumia Watchtower Library kwenye CD-ROM iliyotolewa na Sosaiti, inayotia ndani uwezo mwingine mbalimbali wa kufanya utafiti. Ingawa atambua thamani ya tekinolojia fulani, mtu anayetumia tekinolojia hiyo ya kisasa kwa makusudi yenye manufaa apaswa pia kuwa mwangalifu kujilinda mwenyewe na wengine dhidi ya mambo yoyote yasiyofaa. Twahitaji kudhihirisha usawaziko ili kwamba hata yale matumizi ya tekinolojia yasiyodhuru yasimalize wakati wetu mwingi uliowekwa wakfu au kutukengeusha fikira kutoka kwenye kazi na miradi yetu mikubwa.—Mt. 6:22; 28:19, 20.