Nufaika na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya 1996—Sehemu ya 1
1 Je, umesoma maagizo yaliyotolewa pamoja na “Ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya 1996”? Je, ulitambua baadhi ya mabadiliko? Kuanzia Januari hadi Aprili, Mgawo Na. 3 utategemea “Bible Topics for Discussion” kama ipatikanavyo katika New World Translation au Vichwa vya Mazungumzo ya Biblia, na kuanzia Mei hadi Desemba, utategemea kitabu Ujuzi kilichotolewa karibuni. Mgawo Na. 4 utakuwa hotuba juu ya kitabu Kutoa Sababu.
2 Migawo ya Wanafunzi: Mgawo Na. 3 wanagawiwa dada. Unapotegemea “Bible Topics for Discussion” kama ipatikanavyo katika New World Translation au Vichwa vya Mazungumzo ya Biblia, kikao chapaswa kutia ndani ushahidi wa mlango kwa mlango au wa vivi hivi. Unapotegemea kitabu Ujuzi, unapasa kutolewa kama ziara ya kurudia au funzo la Biblia nyumbani. Huu wapaswa kuwa wenye msaada sana, kwa kuwa kitabu Ujuzi kitatumiwa zaidi kwa kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani.
3 Ikiwa kikao ni funzo la Biblia nyumbani, dada wote wawili waweza kuwa wameketi. Ingia mara moja kwenye funzo kwa kutoa maelezo mafupi ya utangulizi, kisha uulize swali lililochapishwa. Sehemu ya mwenye nyumba yapaswa kufanywa iwe halisi. Maandiko ambayo hayakunukuliwa yanaweza kutafutwa na kusomwa kadiri wakati uruhusuvyo. Dada anapaswa kutumia ufundi wa kufundisha kwa kumvuta mwenye nyumba kwa maswali na kwa kusababu juu ya maandiko yaliyotumiwa.
4 Ni nini lipasalo kufanywa ikiwa kuna maandiko mengi zaidi yasiyonukuliwa katika mgawo kuliko yawezavyo kuzungumzwa kwa dakika tano? Chagua maandiko ya msingi yanayokazia mambo makuu. Ikiwa kuna maandiko machache tu, mambo makuu katika somo yaweza kuzungumzwa kwa upana zaidi. Pindi kwa pindi, fungu au sentensi kutoka kitabu yaweza kusomwa kisha izungumzwe pamoja na mwenye nyumba.
5 Sanduku lenye kichwa “Tahini Ujuzi Wako,” linalopatikana mwishoni mwa kila sura ya kitabu Ujuzi, laweza kupitiwa kifupi na mhubiri ambaye mgawo wake washughulikia fungu la mwisho la sura hiyo. Masanduku ya habari yaliyo kati ya mafungu yaliyotolewa kuwa mgawo yanaweza pia kuzungumzwa kadiri wakati uruhusuvyo. Sanduku la habari likitokea palipo na migawo miwili, dada anayeshughulikia mgawo wa kwanza anaweza kulishughulikia. Picha zilizo katika kitabu zaweza kutolewa maelezo zinapohusu habari inayofikiriwa.
6 Mgawo Na. 4 wapaswa kuwa wenye kupendeza sana na wenye kutumika. Mgawo huu utategemea habari katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko. Wanapogawiwa ndugu, huu wapaswa uwe hotuba kwa wasikilizaji wote. Kwa kawaida itafaa zaidi kwa huyo ndugu kutayarisha hotuba yake akifikiria wasikilizaji kwenye Jumba la Ufalme ili iwe yenye kuarifu na kunufaisha kikweli wale wanaoisikia hasa. Dada anapopewa sehemu hii, habari yapasa itolewe kama vile ilivyoonyeshwa kwa Mgawo Na. 3.
7 Tukitumia kwa manufaa kamili mazoezi yanayoandaliwa kwenye shule, tutaweza ‘kulihubiri neno’ vizuri zaidi katika njia inayoonyesha ‘usanifu mzuri wa kufundisha.’—2 Tim. 4:2, NW.