Nufaika na Programu ya 1999 ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
1 Yesu alikuwa Mwalimu Stadi. Watu “[wali]staajabishwa na njia yake ya kufundisha.” (Mr. 1:22) Ijapokuwa hakuna mmoja wetu awezaye kusema na kufundisha kama alivyofanya Yesu, twaweza kujitahidi kumwiga. (Mdo. 4:13) Ili kufikia mradi huo, kushiriki katika programu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kutatusaidia twendelee kuboresha stadi zetu za kusema na kufundisha.
2 Katika 1999, Mgawo Na. 1 utategemea hasa makala kutoka katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ya 1997. Kuelewa kwetu mambo ya kiroho kutaboreshwa zaidi tukisoma habari hiyo mapema kisha kuisikia kwenye programu ya shule. Wale waliogawiwa kutoa hotuba hizo za maagizo wanapaswa kuonyesha matumizi ya habari hiyo, wakiitoa kwa njia yenye kupendeza na changamfu. Mgawo Na. 3 utategemea kitabu Furaha ya Familia, na Mgawo Na. 4, utategemea “Vichwa vya Biblia vya Mazungumzo,” ijapokuwa huenda chanzo cha habari kikabadilikana kuhusu migawo hiyo. Mwangalizi wa shule apaswa kuifikiria kwa uangalifu habari hiyo kabla ya kutoa migawo. Wanafunzi wote waliogawiwa kutoa habari iliyo katika kitabu Furaha ya Familia wanapaswa kuwa kielelezo bora katika maisha yao wenyewe ya familia.
3 Tumia Shauri, na Utayarishe Vizuri: Kila mtu aweza kufanya maendeleo zaidi katika ufundi wa kusema na kufundisha. (1 Tim. 4:13) Kwa sababu hiyo, twapaswa kutafuta shauri na tusilione kuwa jambo la kuepukwa kamwe. (Mit. 12:15; 19:20) Kutoa kweli kwa matokeo mikutanoni na katika huduma ya shambani huhitaji zaidi ya kusimulia mambo ya hakika tu au kusoma maandiko ili kutimiza wajibu. Twahitaji kufikia mioyo na kuchochea wale watusikilizao. Twaweza kufanya hivyo kwa kusema kweli kwa njia yenye kusadikisha kutoka moyoni mwetu. (Linganisha Matendo 2:37.) Shauri tunalopokea katika shule litatusaidia tutimize jambo hilo.
4 Mara unapopokea mgawo, fikiria sifa za usemi utakazofanyia kazi kama inavyoelezwa katika kitabu Kiongozi cha Shule. Fikiria unachohitaji kufanya ili kutumia shauri ulilopokea wakati uliopita. Tafakari juu ya kichwa chako, kikao utakachotumia kama chahitajiwa, na jinsi utakavyotumia maandiko yaliyo katika habari yako uliyogawiwa. Fikiria kwa uzito juu ya njia nzuri zaidi ya kutumia habari hiyo kufundisha na kuchochea.—1 Tim. 4:15, 16.
5 Kama unahofu kujiandikisha katika shule, sali kuhusu jambo hilo kisha uzungumzie hisia zako na mwangalizi wa shule. Kila mtu anaweza kunufaika kwa kutumia kwa manufaa programu itakayotolewa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika 1999.