Uandikishwaji Katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
1 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi imekuwa chombo cha mazoezi kwa mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wawe wahudumu wa habari njema. Wengi wetu twakumbuka jinsi tulivyokuwa wenye hofu na wenye kupungukiwa tulipojiandikisha katika shule kwa mara ya kwanza, na sasa twatambua zaidi fungu layo katika usitawi wetu wa kiroho tukiwa wasemaji na wafundishaji wa Neno la Mungu. (Linganisha Matendo 4:13.) Je, umejiandikisha katika shule hii yenye kutokeza?
2 Ni nani awezaye kujiandikisha? Ukurasa wa 73 wa kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu hujibu: “Wote ambao ni watendaji wanaoshirikiana na kundi, kutia na wapya wanaohudhuria mikutano, wanaweza kujiandikisha majina ikiwa maisha yao yanapatana na kanuni za Kikristo.” Twaalika wote walio na sifa za ustahili—wanaume, wanawake, na watoto—wamfikie mwangalizi wa shule na kumwomba waandikishwe.
3 Programu ya Shule ya 1997: Programu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya 1997 hutia ndani mafundisho ya namna mbalimbali ya Biblia. Kwa kuongezea kusitawisha uwezo wetu wa kusema na kufundisha, twajifunza kutokana na hazina nyingi za kiroho zinazopatikana katika utaratibu wayo wa masomo kila juma. (Mit. 9:9) Tukitayarisha kwa ajili ya shule, inayotia ndani usomaji wa Biblia kila juma, na twahudhuria kwa ukawaida, twaweza kupata manufaa kubwa ya kiroho kutokana na hiyo programu.
4 Katika 1997 usomaji ulio mwingi wa Biblia kwa Mgawo Na. 2 ni mfupi kuliko miaka iliyopita. Anapotayarisha mgawo huu, mwanafunzi apaswa kuangalia wakati wa usomaji wake sawasawa kisha achunguze atatumia muda gani wa zile dakika tano zilizowekwa kwa ajili ya usomaji wake zinavyoweza kutumiwa kwa utangulizi na umalizio. Hili litaruhusu mwanafunzi atumie wakati wake kikamili na asitawishe uwezo wake wa kusoma na ustadi wake wa kusema bila kutazamia.—1 Tim. 4:13.
5 Ushahidi wa vivi hivi umeongezwa kuwa kikao cha utoaji katika Mgawo Na. 3, ambao wategemea kitabu Ujuzi. Kwa sababu hiyo, dada aweza kuchagua ama ziara ya kurudia, ama funzo la Biblia nyumbani, au ushahidi wa vivi hivi kuwa kikao cha mgawo huu. Bila shaka, mkazo mkubwa wapaswa kuendelea kuwa juu ya ufundishaji wenye matokeo na si kikao.
6 Uwe una pendeleo la kutoa hotuba ya maagizo, mambo makuu ya Biblia, au mgawo wa mwanafunzi, unaweza kuonyesha uthamini kwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kwa kutayarisha na kurudia sehemu yako vizuri, kwa kuitoa na usadikisho na idili, kwa kutokupitisha wakati, kwa kusikiliza na kutumia shauri la mwangalizi wa shule, na kwa kujitahidi sikuzote kutimiza mgawo wako kwa uaminifu. Hivyo kujiandikisha kwako katika shule kutathibitika kuwa baraka kwako na wote wanaohudhuria.