Hali Zimebadilika
1 Biblia hutuambia kwamba “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Kor. 7:31, NW) Hiyo ni kweli kama nini leo! Hata katika muda wa maisha yetu, tumeona mabadiliko makubwa katika kufikiri na mwenendo wa watu kwa kila kiwango cha jamii ya kibinadamu. Ikiwa twataka kufanikiwa katika kuwafikia kwa ujumbe wa Ufalme, mfikio wetu wapaswa kupatana na hali hizi zenye kubadilika. Twataka kutoa habari njema kwa njia ambayo itapendeza watu na kuifikia mioyo yao.
2 Miaka mingi iliyopita, kazi ya kutoa ushahidi ilikuwa tofauti katika nchi nyingi kwa sababu, kwa ujumla watu waliishi maisha yenye utulivu hasa, na walihisi wakiwa salama. Dini ilikuwa takatifu maishani mwao. Biblia iliheshimiwa sana. Siku hizo kutoa ushahidi mara nyingi kulitia ndani mabishano yenye kukanusha kuhusu masuala ya kimafundisho. Leo, maisha za watu ziko taabani. Dini inadhihakiwa. Ni wachache wanaoamini Biblia. Na kwa walio wengi, nadharia ya mageuzi imeharibu imani katika Mungu.
3 Mwangalizi mmoja asafiriye aliona hivi: “Sasa, yaonekana kuna matatizo na magumu mengi sana katika maisha za watu hivi kwamba lazima tuwafundishe namna ya kuishi.” Wasiwasi wa wakati huu kwa watu kawaida unawahusu wenyewe, familia zao, na mahangaiko yao. Haya ndiyo mambo wanayoongea hasa wanapokuwa pamoja. Twahitaji kukumbuka hayo tunapokuwa katika kazi yetu ya kutoa ushahidi.
4 Ufalme wa Mungu Ndilo Tumaini Hakika Pekee la Wakati Ujao: Watu walio wengi hawatumainii utawala wa kibinadamu. Wao huona kwamba hakuna tazamio la kuona ulimwengu bora maishani mwao. Dini bandia imeshindwa kuwapa msingi wa tumaini. Ndiyo sababu uhitaji mkubwa wa wanadamu ni kusikia habari njema za Ufalme wa Mungu. Onyesha jinsi mwishowe utakavyoandaa utatuzi kwa matatizo yote yanayowakabili wanadamu.
5 Biblia Ndicho Chanzo Pekee Chenye Kutegemeka cha Mwongozo: Leo watu wengi wameongozwa vibaya na viongozi wanaotegemea hekima ya binadamu na falsafa za kilimwengu. Lazima watu watambue kwamba “kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yer. 10:23) Somo lenye thamani zaidi wawezalo kujifunza ni kwamba, ni lazima ‘wamtumaini BWANA kwa moyo wao wote, wala wasizitegemee akili zao wenyewe.’ (Mit. 3:5) Ingawa hali zimebadilika, Biblia haijabadilika. Hivyo, katika huduma yetu sikuzote twapaswa kukazia Neno la Mungu, tukifundisha wengine wathamini mwongozo walo uliopuliziwa wa kimungu. (2 Tim. 3:16, 17) Ili kutimiza kusudi hilo, twapaswa kuonyesha watu umaana wa Biblia kwa kuirejezea kwenye utoaji wetu mbalimbali, tukiitumia kujibu maswali yao, na kutetea uhitaji wa kuisoma na kutumia hekima yayo inayofaa.
6 Hata katika hali za leo zenye kubadilika, malengo yetu katika huduma yapasa kudumu yakiwa yaleyale. Twapaswa kuhubiri habari njema za Ufalme, kukazia uhakika katika Neno la Mungu, na kusaidia wengine waone uhitaji wa kujifunza Biblia pamoja nasi. Yale tusemayo yapaswa kupatana na mahitaji ya sasa ya wale tunaotolea ushahidi. Kwa kufanya hivi, twaweza kuwa washiriki wa habari njema na wengine na hivyo kupata watu wengi.—1 Kor. 9:19, 23.