Mikutano Huchochea Kwenye Kazi Zilizo Bora
1 Sehemu mbili muhimu za ibada yetu ni kuhudhuria mikutano na kushiriki katika utumishi wa shambani. Hizo mbili huenda sambamba. Sehemu moja huwa na uvutano kwa ile nyingine. Mikutano ya Kikristo huchochea kwenye kazi zilizo bora, ambazo kati ya hizo iliyo nzuri zaidi ni kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Ebr. 10:24) Ikiwa tungeacha kuhudhuria mikutano, upesi huenda tukaacha kuhubiri kwa sababu hatutachochewa kufanya hivyo.
2 Kwenye mikutano ya kila juma, twapokea maagizo ya kiroho yanayokusudiwa kutuchochea kuhubiri. Uharaka wa nyakati hukaziwa kwetu, ukitushurutisha tuwapelekee wengine ujumbe wa Biblia upao uhai. Twatiwa moyo na kuimarishwa tuvumilie katika kazi ya kuhubiri. (Mt. 24:13, 14) Kwa kutumia kwa manufaa fursa za kutoa maelezo mikutanoni, twazoea zaidi kueleza imani yetu mbele ya wengine. (Ebr. 10:23) Kwa kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, twapokea mazoezi ya kuwa wahudumu wenye matokeo zaidi na kuboresha stadi zetu za kufundisha.—2 Tim. 4:2.
3 Jinsi Ambavyo Mikutano ya Utumishi Hutuchochea Kuhubiri: Sisi sote twatiwa moyo tuchunguze habari iliyo katika Huduma ya Ufalme Yetu kimbele. Kisha habari hii inakaziwa katika akili zetu tunapohudhuria Mkutano wa Utumishi na kuona utoaji unapoonyeshwa jukwaani. Tunapokuwa katika utumishi wa shambani, twaweza kufikiri juu ya Huduma ya Ufalme Yetu, tukumbuke maonyesho ambayo yalitolewa, na hivyo tutoe ushahidi wenye matokeo zaidi. Haya yamekuwa mambo yaliyoonwa na wahubiri wengi.
4 Kwa kufuatilia yaliyo katika Mkutano wa Utumishi, watu fulani hufanya miadi na wengine ili pamoja washiriki katika huduma. Wahubiri wanakumbuka mambo yanayohusu kazi ya shambani nao wanachochewa kuyajaribu kwa sababu mikutano hii imewatia moyo washiriki katika kazi ya kuhubiri kila juma.
5 Hatuwezi kubadilisha mikutano yetu ya Kikristo na kitu kinginecho, mahali ambapo twakutana na waabudu wenzetu na kuchochewa kwenye kazi zilizo bora. Ili huduma yetu isitawi, lazima tuhudhurie kwa ukawaida mikutano ya kutaniko. Na tuonyeshe uthamini kwa uandalizi huu mzuri ajabu kutoka kwa Yehova kwa ‘kutoachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe.’—Ebr. 10:25.