“Je, Watu Wote Watapata Kupendana?”
1 Ujumbe mzuri, wenye kusisimua, wenye kuchangamsha moyo utatangazwa ulimwenguni pote katika lugha 169. Huu ni ujumbe gani? Nao utatolewaje?
2 Huo ujumbe unahusu upendo kwa jirani. Unapatikana katika trakti Habari za Ufalme Na. 35, yenye kichwa “Je, Watu Wote Watapata Kupendana?” Trakti hii Habari za Ufalme yachunguza kifupi hali ya mambo ya wakati wa sasa ulimwenguni pote, ikionyesha kwamba ni ukosefu wa upendo miongoni mwa watu ambao ndio chanzo cha maumivu ya moyoni na maumivu mengine mengi. Inaeleza ni kwa nini, katika siku yetu hasa, upendo kwa jirani umepoa na kinachomaanishwa kwa wakati wetu ujao.
3 Wakati uleule, trakti Habari za Ufalme Na. 35 yaonyesha kwamba upendo kwa jirani upo miongoni mwa mamilioni wanaoishi katika ulimwengu wa leo. Inatambulisha wale wanaoshiriki kurudisha Ukristo wa kale, yaani, ibada ya karne ya kwanza, ambayo ilijulikana kwa sababu ya upendo kwa jirani kama ilivyofundishwa na Yesu Kristo.—Luka 10:25-37.
4 Trakti Habari za Ufalme Na. 35 yamalizia kwa ufafanuzi wa jinsi hivi karibuni ulimwengu mzima wa wanadamu utakavyodhihirisha upendo kwa jirani chini ya usimamizi wa Ufalme wa Mungu kupitia Kristo. Wale wanaosoma ujumbe huu wanatiwa moyo kujipatia broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? na wajifunze jinsi ya kuwa sehemu ya mpango huu wenye upendo wa ulimwenguni pote unaofafanuliwa kwa kina katika Neno la Mungu.
5 Ni Nani Atakayeutoa Ujumbe Huu? Mwezi wa Oktoba na Novemba Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote watakuwa wakishiriki ujumbe huu wa upendo kwa jirani pamoja na watu wanaowajua, jirani zao, na jamaa zao. Wote walio na sifa ya ustahili wanatiwa moyo kushiriki waziwazi ugawanyaji wa trakti Habari za Ufalme Na. 35.
6 Mradi wa mwisho wa kampeni hii ni kuchochea upendezi wa watu wa kuwa na funzo la Biblia ama katika broshua Anataka ama katika kitabu Ujuzi. Kwa kuongezea, jitihada ya moyo wote upande wa kila mmoja wa watumishi wa Yehova itatokeza ushahidi mkubwa kwa ajili ya Mungu mwenye upendo, Yehova, na kwa ajili ya Mwana wake, Yesu Kristo.