Fuatia Kupendezwa Kulikoonyeshwa Katika Trakti Habari za Ufalme
1 Majuma machache yaliyopita, tumekuwa tukifurahia pendeleo la kugawanya trakti Habari za Ufalme Na. 35, yenye kichwa “Je, Watu Wote Watapata Kupendana?” Kila mahali wahubiri wanajitahidi kufikia watu wengi iwezekanavyo wanaostahili wakiwa na toleo hili la trakti Habari za Ufalme. (Mt. 10:11) Ijapokuwa kampeni imeratibiwa kuisha Jumapili, Novemba 16, ikiwa bado kuna eneo la kufanywa, huenda wazee wakawaomba mwendelee kugawanya trakti Habari za Ufalme Na. 35 maadamu gawio la kutaniko laendelea.
2 Toleo hili la trakti Habari za Ufalme limechochea kupendezwa kwa watu wengi. Wanaona kwamba wanadamu kwa ujumla wamepoteza shauku yao ya kiasili na kwa hiyo wanajiuliza wakati ujao una nini. (2 Tim. 3:3) Twataka kufuatia kupendezwa ambako kumeonyeshwa.
3 Trakti Habari za Ufalme Yapata Matokeo: Wakati wa kampeni ya 1995 ya trakti Habari za Ufalme, Mwanamke mmoja aliyepokea nakala moja alikuja mkutanoni kwenye Jumba la Ufalme kwa sababu alitaka kujifunza mengi zaidi juu ya yale ambayo Mashahidi wa Yehova huamini. Kwenye huo mkutano alikubali funzo la Biblia mara moja na baada ya hapo hakukosa mkutano. Baada ya muda mfupi, alikuwa ameandikia kanisa lake la zamani, akikomesha ushiriki wake!
4 Kufikia sasa, mamia ya watu katika eneo wamesoma ujumbe ulio katika trakti Habari za Ufalme Na. 35. Lakini itikio lao kuihusu lilikuwa nini? Hata kama walipendezwa sana na yale waliyosoma, walio wengi hawatachukua hatua mpaka mmoja wa Mashahidi wa Yehova awarudie tena. Je, unafanya mipango ya kurudi? Hangaiko lenye upendo kwa binadamu-mwenzi lapaswa kutuchochea tufanye hivyo. Wale wote ambao wameonyesha kupendezwa katika trakti Habari za Ufalme wapasa kutembelewa tena.
5 Utasema Nini Unaporudi? Labda utapenda kutoa maelezo machache kuhusu jinsi trakti Habari za Ufalme inavyofaa nyakati hizi kisha uulize swali lenye kuamsha fikira. Sikiliza kwa uangalifu mwenye nyumba anapojieleza mwenyewe ili uweze kujua yaliyo akilini mwake. Kisha vuta uangalifu kwenye hoja inayofaa katika broshua Anataka, iliyokaziwa katika trakti Habari za Ufalme. Ukipata itikio zuri, jaribu kuanzisha funzo la Biblia mara hiyo.
6 Huu ni utoaji mbalimbali uliodokezwa unaoweza kujaribu unaporudia wale walioonyesha kupendezwa na trakti “Habari za Ufalme” Na. 35:
◼ “Huenda ukakumbuka habari iliyochapishwa niliyokuachia majuzi. Ujumbe wake hugusia suala muhimu linalogawanya wanadamu leo—kukosa kuwaonyesha wengine upendo.” Vuta uangalifu kwenye uthibitisho uliotolewa kwenye ukurasa wa 2 wa trakti Habari za Ufalme chini ya kichwa “Upendo kwa Jirani Umepoa.” Kisha uulize, “Je, wafikiri ni kusudi la Mungu wanadamu waishi hivi?” Ruhusu itikio. Fungua somo la 5 katika broshua Anataka, na ujaribu kuanzisha funzo la Biblia.
◼ “Tulipokutana mara ya kwanza, nilikuachia habari fulani juu ya somo ‘Je, Watu Wote Watapata Kupendana?’ Wafikiri yawezekana kuwa na ulimwengu kama huo?” Ruhusu itikio. Fungua somo la 6 katika broshua Anataka, na usome fungu la 6. Kisha soma ahadi ya Mungu kwenye Mika 4:3, 4. Mwenye nyumba akionekana anapendezwa, toa broshua na funzo.
◼ “Mara ya mwisho nilipokutembelea, niliacha habari yenye kichwa ‘Je, Watu Wote Watapata Kupendana?’ Ilikuwa na toleo la funzo la Biblia nyumbani bila malipo. Nilirudi nikuonyeshe msaada wa funzo tunaotumia. [Onyesha kitabu Ujuzi.] Kitabu hiki hueleza waziwazi wakati watu wote watakapopendana, nacho hujibu maswali mengine ambayo huenda ukajiuliza: Kwa nini sisi huzeeka na kufa? Kwa nini Mungu huruhusu kuteseka? Inakuwaje kwa wapendwa wetu waliokufa?” Kisha uulize, “Je, nikuonyeshe jinsi ya kufanya mtaala wa funzo?” Mwenye nyumba akikataa toleo lako, mwulize kama angependa kusoma kitabu hicho yeye mwenyewe. Ikiwa angependa, toa nakala. Panga kurudi tena.
7 Mara tu eneo limalizwapo kuhubiriwa kikamili kwa kutumia trakti Habari za Ufalme Na. 35, twaweza kutoa kitabu Ujuzi sehemu inayobaki ya mwezi. Uchaguzi mzuri wa utoaji mbalimbali uliodokezwa kwa kitabu hiki waweza kupatikana kwenye ukurasa wa nyuma wa toleo la Huduma ya Ufalme Yetu la Machi, Juni, na Novemba 1996; na Juni 1997.
8 Ugawanyaji huu wa pekee wa trakti Habari za Ufalme wapaswa kutuchochea sote kuzidisha jitihada zetu katika kazi ya kuhubiri. Kwa msaada wa Yehova twaweza kuwa na hakika kwamba kampeni hii itapata mafanikio kamili, ikisaidia watu waone kusudi la Mungu la kutaka wanadamu wote wapendane. Yehova na aendelee kubariki jitihada zetu za bidii ya uendelevu tunapofuatia kupendezwa kulikoonyeshwa katika trakti Habari za Ufalme.