Sema Juu ya Yehova Kila Siku
1 Watu hufurahia kuongea juu ya kile wakipendacho moyoni mwao, kwa maana katika wingi wa moyo kinywa husema. (Luka 6:45b) Ni nini kilicho cha thamani moyoni mwetu? Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Na ulimi wangu utanena haki yako, na sifa zako mchana kutwa.” (Zab. 35:28) Alikuwa na uthamini wenye kina kirefu kwa Yehova naye aliliona kuwa pendeleo lenye thamani kusema juu ya Mungu na kumsifu yeye kila pindi. Akiwa anamjua Yehova kwa ukaribu sana, mtunga-zaburi alikuwa na vitu vingi vya kushangilia. (Zab. 35:9) Twaweza kuigaje kielelezo chake bora?
2 Sema Juu ya Yehova Nyumbani Mwako: Kila siku kusema juu ya Yehova kwapaswa kuwa jambo la maongezi katika familia. Wazazi wampendao Yehova kwelikweli watasema kwa urahisi juu yake katika utendaji wao wote. (Kum. 6:5-7) Wakifanya hivyo, watoto wataona kwamba baba na mama yao huishi kupatana na imani nao wanapenda sheria ya Mungu. Ndipo watoto watakapoliona funzo la Biblia la familia kuwa wonyesho wa kweli wa ujitoaji kimungu wa wazazi wao.—2 Pet. 3:11.
3 Sema Juu ya Yehova Pamoja na Ndugu Zako: Wakati wa kawaida yetu ya kitheokrasi ya kila juma, tuna fursa nyingi za kulisha akili zetu na mioyo yetu chakula cha kiroho. Hatukosi kamwe mambo mazuri ya kuongea. (Luka 6:45a) Je, kuna jambo lolote ulilopata kutokana na funzo lako la kibinafsi au usomaji wa Biblia wa kila juma ambao ulifurahia hasa? Lishiriki na ndugu zako, kwa njia hiyo ukiwasaidia waongeze upendo wao kwa Yehova.—Zab. 35:18; Ebr. 10:24.
4 Sema na Wengine Juu ya Yehova: Katika shughuli zetu za kila siku pamoja na watu—kazini, shuleni, na pamoja na washiriki wa familia wasioamini—yapasa iwe wazi bila shida kwamba jambo letu kuu maishani ni kutoa ushahidi juu ya Yehova. Badala ya kuchafuliwa na semi za ulimwengu, zisizo za uungwana na za kishenzi, usemi wetu wapaswa kumkweza Mungu. Kila siku, katika kila fursa, sema na wengine juu ya habari njema alizotuamuru tuzihubiri.—Mdo. 5:42; Kol. 4:6.
5 Tukiwa waabudu wa kweli wa Yehova, sikuzote na tutafute pindi za kusema juu ya Mungu wetu asiyelinganika, Yehova.—Zab. 106:47.