Kusitawisha Upendezi Uliochochewa na Trakti Habari za Ufalme Na. 36
1 Je, umemaliza kugawanya trakti ulizogawiwa za Habari za Ufalme Na. 36? Trakti hiyo yauliza swali lifaalo ambalo kila mtu apaswa kutafakari: “Milenia Mpya—Unaweza Kutarajia Nini Wakati Ujao?” Mwaka wa 2000 ulipokuwa unakaribia, matarajio ya milenia mpya yalitofautiana sana. Trakti Habari za Ufalme Na. 36 yachunguza baadhi ya matarajio hayo na kutukumbusha kwamba hali za ulimwengu haziandai sababu ya kutarajia mema. Milenia itakayoleta amani na usalama ambao watu wengi wanatafuta ni Utawala wa Milenia wa Kristo Yesu. Uhakika wetu katika uhalisi wa Ufalme wake ulituchochea tumpe kila mtu tuliyemfikia trakti Habari za Ufalme Na. 36.
2 Matokeo ya Trakti Habari za Ufalme: Kampeni zilizopita za kugawanya trakti Habari za Ufalme zimethibitika kuwa kichocheo kizuri kwa kazi yetu. Kuhusu trakti Habari za Ufalme Na. 35, ofisi ya tawi ya Kanada iliandika hivi: “Kampeni hiyo ya pekee iliungwa mkono kwa uchangamfu na wahubiri na mapainia shambani, na mambo mengi yaliyoonwa yenye kutia moyo yalifurahiwa.” Pasina shaka umeonyesha uchangamfu huohuo katika kugawanya trakti Habari za Ufalme Na. 36.
3 Kampeni ya sasa ya trakti Habari za Ufalme imeratibiwa kwisha Novemba 17, 2000. Je, eneo lote ambalo kutaniko lenu lilipewa limehubiriwa kikamili? Kama halijamalizwa, huenda wazee wakawaomba kuendelea na kampeni hii hadi mwisho wa Novemba.
4 Itikio la kugawanya trakti Habari za Ufalme Na. 36 katika eneo lenu limekuwaje kufikia sasa? Watu wachache watajaza kuponi na kuomba nakala ya broshua Anataka na/au funzo la Biblia la nyumbani. Hata hivyo, wengi wa wale wanaoonyesha kupendezwa mara ya kwanza kuhusu milenia huenda wasichukue hatua isipokuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova awarudie. Wote ambao wameonyesha kupendezwa wanapasa kutembelewa tena. Wakati mzuri wa kufanya hivyo utakuwa lini? Wapasa uwe haraka iwezekanavyo.
5 Ona mambo haya yaliyoonwa yanayotokana na kurudia wale walioachiwa trakti Habari za Ufalme Na. 35. Painia mmoja huko Ireland alimwachia mwenye mkahawa mmoja trakti Habari za Ufalme. Mwanamke huyo alipendezwa na ujumbe huo na kumwalika dada huyo tena. Dada alirudi siku mbili baadaye, na funzo la Biblia likaanzishwa. Huko Denmark, nakala ya trakti Habari za Ufalme iliachwa kwenye nyumba ambayo haikuwa na mtu nyumbani. Siku hiyohiyo mwanamke aliyeishi humo alituma kuponi kwenye ofisi ya tawi, nayo ofisi ikaituma kwenye kutaniko la huko. Kabla ya juma kwisha, dada wawili walimzuru, wakapanga funzo, na mwanamke huyo akahudhuria mkutano wake wa kwanza kwenye Jumba la Ufalme!
6 Jambo la Kusema Unaporudi: Kufanya ziara za kurudia za trakti Habari za Ufalme ni rahisi na ni sehemu yenye kufurahisha ya huduma yetu. Unapofanya hivyo, inafaa kubeba nakala moja ya trakti Habari za Ufalme Na. 36, kwa kuwa huenda mwenye nyumba asiwe na yake. Unaweza kujaribu madokezo haya.
7 Baada ya kumkumbusha mwenye nyumba wewe ni nani, unaweza kusema:
◼ “Nilikuachia trakti yenye kichwa ‘Milenia Mpya—Unaweza Kutarajia Nini Wakati Ujao?’ Je, haukutiwa moyo kusoma kwamba hivi punde Utawala wa Milenia wa Kristo Yesu utaanza, ukileta hali za Paradiso duniani kote? [Mwonyeshe picha za Paradiso katika trakti Habari za Ufalme Na. 36.] Kwenye ukurasa wa nyuma, unaalikwa kuomba nakala ya broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?” Mwonyeshe broshua hiyo, fungua somo la 5, soma swali la kwanza na fungu la 1 na la 2, na umwombe mwenye nyumba atoe maelezo. Soma na mzungumzie andiko moja au mawili. Ikiwezekana, chunguzeni swali na fungu jingine, kisha upange kurudi na kuendeleza mazungumzo.
8 Kwa kuwa toleo la Novemba la kufuatia kupendezwa litakuwa broshua “Anataka” au kitabu “Ujuzi,” unaweza kusema:
◼ “Nilipokutembelea hivi majuzi, nilikuachia nakala ya trakti ‘Milenia Mpya—Unatarajia Nini Wakati Ujao?’ Inakutolea fursa ya funzo la Biblia nyumbani bila malipo. Nimerudi ili kukuonyesha kichapo tunachotumia kujifunzia. [Onyesha broshua Anataka, na ufungue ukurasa wa nyuma; au uonyeshe kitabu Ujuzi, na ufungue ukurasa wa 188-189.] Milenia inayozungumziwa na Biblia italeta hali unazoona katika picha hii. Ili tustahili kuishi katika Paradiso, twahitaji kuwa na ujuzi sahihi kuhusu Mungu. Tafadhali ukiniruhusu naweza kukuonyesha kifupi jinsi tunavyojifunza Biblia.”
9 Kugawanywa kwa trakti Habari za Ufalme Na. 36 kumetuchochea kuzidisha huduma yetu, na hivyo kutoa ushahidi mkubwa. Yaelekea kwamba hiyo imeamsha kupendezwa kwa watu wengi katika eneo. Jitihada yetu ya pamoja ya kusitawisha upendezi huo kwa msaada wa Yehova, itatuletea shangwe ya kupata watu wengi zaidi walio mfano wa kondoo.—Mt. 10:11; Mdo. 13:48, 49, 52.