“Milenia Mpya—Unaweza Kutarajia Nini Wakati Ujao?”
1 Swali hilo limefikiriwa na watu duniani kote. Ijapokuwa mwanadamu ametimiza mengi kwa karne nyingi, watu wanakata tamaa kwa sababu matatizo ya msingi ambayo yamewapata wanadamu kwa milenia kadhaa yangalipo. (Ayu. 14:1; Zab. 90:10) Wanadamu wanaweza kupata wapi msaada?
2 Mwezi wa Oktoba na Novemba, tutakuwa na fursa ya pekee ya kuwapa jirani zetu jibu la swali hilo. Jinsi gani? Kupitia kugawanya trakti Habari za Ufalme Na. 36. Ina kichwa “Milenia Mpya—Unaweza Kutarajia Nini Wakati Ujao?” Nusu ya kwanza ya mwezi wa Oktoba, tutatoa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kisha kuanzia Jumatatu, Oktoba 16, hadi Ijumaa, Novemba 17, tutagawanya kwa bidii trakti Habari za Ufalme Na. 36. Wakati wa kampeni hii, tutakazia fikira kuangusha trakti Habari za Ufalme Na. 36 katikati ya juma. Kwenye miisho-juma, tutaitoa pamoja na magazeti ya karibuni.
3 Je, Utashiriki Kikamili? Wazee, watumishi wa huduma, na mapainia wangependa kuongoza katika kampeni hii, kwa kuwa wao wako mstari wa mbele katika kazi hii. Huenda wahubiri wengi wamerekebisha hali zao ili wafanye upainia-msaidizi mwezi mmoja au miezi yote miwili ya ugawanyaji huo wa trakti. Wengine wanapanga kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma kuliko kawaida.
4 Viongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko wanaweza kumtia moyo kila mshiriki wa kikundi chao ashiriki kikamili kugawanya trakti Habari za Ufalme Na. 36. Huenda kukawa na wahubiri ambao wamekuwa wasiotenda katika kazi ya kuhubiri. Wazee wapaswa kuwatembelea ili waone jinsi wanavyoweza kuwasaidia. Labda mipango inaweza kufanywa ili mhubiri mwenye uzoefu aandamane na mtu asiyetenda katika utumishi miezi hiyo. Utoaji sahili wa trakti Habari za Ufalme Na. 36 huenda ukawa jambo linalohitajiwa tu ili kufanya wahubiri hao wawe watendaji tena.
5 Hiyo itakuwa fursa nzuri pia kwa wanafunzi wa Biblia ambao wanakaribia kumaliza kujifunza kitabu Ujuzi na ambao wanastahili kuwa wahubiri wasiobatizwa kuanza kushiriki katika huduma. Hata wachanga wanaweza kushiriki ifaavyo katika kazi hii yenye kusisimua.
6 Utoaji sahili ndio unaohitajika tu. Unaweza kusema:
◼ “Nimejitolea kutumia wakati wangu ili kusaidia kugawanya ujumbe huu muhimu sana kwa kila familia hapa [jina la jiji, mji au wilaya]. Hii ni nakala yako. Tafadhali isome.” Huenda ikafaa kutobeba mkoba wa mahubiri unapogawanya trakti Habari za Ufalme Na. 36.
7 Mikutano ya Utumishi wa Shambani Iliyopangwa Vizuri: Wazee wanapaswa kuhakikisha kwamba mipango ya kutoa ushahidi inafaa na ni yenye kutumika. Mwangalizi wa utumishi hasa anapaswa kuhakikisha kwamba kuna eneo la kutosha la nyumba hadi nyumba na eneo la kibiashara ili kila mtu aweze kushiriki kikamili katika kazi hiyo. Inapowezekana, mikutano ya utumishi wa shambani ipangwe kila siku ya juma, miisho-juma, na jioni. Mipango yaweza kufanywa ili kukutana saa za jioni kwa manufaa ya wanafunzi wa shule, wafanyakazi wa zamu, na wengineo.
8 Jambo la Kufanya kwa Wasiokuwepo Nyumbani: Mradi wetu ni kuongea na wenye nyumba wengi iwezekanavyo. Ikiwa humpati mtu yeyote nyumbani, andika mahali hapo kisha urudi wakati tofauti siku hiyo. Ikiwa hujafaulu kuwapata wenye nyumba hao kufikia juma la mwisho la kampeni, unaweza kuwaachia nakala ya trakti Habari za Ufalme Na. 36 mahali ambapo haionwi na wapita-njia. Wazee wa kwenu wanaweza kuagiza kutaniko liache nakala ya trakti Habari za Ufalme Na. 36 mahali ambapo hapana watu nyumbani kwa mara ya kwanza wanapohubiri sehemu za mashambani na sehemu zenye eneo kubwa lisiloweza kukamilishwa wakati wa kampeni hiyo.
9 Na Tuwe na Shughuli Nyingi! Makutaniko yapaswa kujitahidi kukamilisha eneo lao kabla kampeni haijaisha tarehe 17 mwezi wa Novemba. Ikiwa eneo lenu ni kubwa mno, wahubiri wengine wanaweza kuhubiri peke yao mahali ambapo ni salama. Mpango huu utafanya iwe rahisi kufikia watu wengi iwezekanavyo wanaostahili. Hakikisha unaweka maandishi sahihi ya wote walioonyesha kupendezwa.
10 Wazee wanapaswa kukadiria magazeti ya ziada ambayo kutaniko litahitaji na kuyaagiza. Hakuna haja ya kuagiza trakti Habari za Ufalme Na. 36, kwa kuwa zitatumwa kwa kila kutaniko. Mapainia wa pekee, wa kawaida, na wasaidizi watapokea nakala 250 kila mmoja, ilhali wahubiri wa kutaniko watagawiwa nakala 50 kila mmoja. Kwa hiyo sasa je, uko tayari na watamani kuwa na shughuli nyingi katika utendaji huu wa pekee? Tuna pendeleo kama nini kuwajulisha jirani zetu wote kile ambacho Mungu ameahidi kwa wakati ujao ulio karibu!