‘Walioandaliwa Vifaa Kikamili kwa Ajili ya Kila Kazi Njema’
1 Leo watu wa Yehova wamebarikiwa kwa wingi wa chakula cha kiroho. (Isa. 25:6) Kuna habari nyingi za Kimaandiko za kufurahia kupitia funzo la kibinafsi na la familia na kwenye mikutano ya kutaniko, makusanyiko, na mikusanyiko. Lakini je, twatumia kwa manufaa hayo yote tukiwa na lengo la ‘kuwa hodari, tulioandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema’?—2 Tim. 3:17.
2 Hebu fikiria orodha ya chakula cha kiroho ya mwaka wa 1998, ambao umefikia nusu yake! Kupitia mikutano ya kutaniko ya kila juma, tunapitia baadhi ya mambo makuu ya vitabu 23 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, tukipitia habari inayopatikana katika vichwa vya Biblia vya Mazungumzo 49, na tukichunguza kurasa 138 za kitabu Wapiga-Mbiu. Pia twapitia thuluthi tatu ya kitabu Ujuzi, karibu kitabu chote cha Furaha ya Familia, na kitabu chote cha Neno la Mungu. Kwa kuongezea, tunalishwa kwa matoleo 12 ya Huduma ya Ufalme Yetu, makala 52 za funzo la Mnara wa Mlinzi, na karibu hotuba za watu wote zipatazo hesabu hiyohiyo kuhusu habari mbalimbali za Biblia. Programu zenye mambo mengi za mkusanyiko na kusanyiko zaongezwa katika yote hayo. Ni utajiri wa mambo mazuri ya kiroho tuliyo nayo kama nini!
3 Shukuru kwa Ajili ya Maandalizi ya Yehova: Ili tunufaike kikamili, twahitaji kuelewa kwa nini Yehova huandaa chakula kingi hivyo cha kiroho. Kujilisha vitu hivi vizuri hujenga imani yetu na kuimarisha uhusiano wetu naye. (1 Tim. 4:6) Hata hivyo, chakula cha kiroho hakitolewi ili tu kutufundisha sisi. Hicho hutuchochea kushiriki kweli na wengine na hutuandaa tuwe wenye matokeo tukifanya hivyo tukiwa wahudumu wa habari njema.—2 Tim. 4:5.
4 Acheni tusipuuze mahitaji yetu ya kiroho, lakini sikuzote tusitawishe tamaa ya maandalizi mengi na yenye kutosheleza kiroho kutoka katika meza ya Yehova. (Mt. 5:3; 1 Pet. 2:2) Ili kunufaika kikamili twahitaji kutenga wakati wa kutosha kwa ajili ya mambo ya maana kama vile funzo la Biblia la kibinafsi na la familia na kuhudhuria mikutano. (Efe. 5:15, 16) Thawabu zenye kuleta furaha za kufanya hivyo zitalingana na kitia-moyo kilichopuliziwa ambacho Paulo aliandikia Wakristo waaminifu Waebrania, kama ilivyoandikwa kwenye Waebrania 13:20, 21.