Waangalizi Wanaoongoza —Kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi
1 Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova ni uandalizi wa msingi wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” wa kutupatia chakula cha kiroho “kwa wakati ufaao.” (Mt. 24:45) Mzee anayeongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi ana daraka muhimu akiwa mwalimu mwenye uwezo anayeweka kielelezo bora katika maisha ya Kikristo.—Rom. 12:7; Yak. 3:1.
2 Ili kufundisha kwa matokeo, lazima kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi ajitahidi sana kutayarisha kila juma. Yeye hufanya hivyo kwa sala na kwa uangalifu. Kupendezwa kwake na kutaniko kwaonyeshwa katika jitihada ya kweli ya kufikia mioyo yetu kwa habari inayochunguzwa. Yeye hukazia mambo makuu ya somo na kutusaidia tuone jinsi yanavyohusiana na kichwa cha makala.
3 Kujitayarisha kikamili upande wake, hutia ndani kuchunguza maandiko mapema ili ajue jinsi yanavyotumika. Yeye hutanguliza Neno la Mungu kwa kutia moyo kutaniko litumie sana Biblia wakati wa funzo. Jambo la maana linapokosa kuelezwa kutanikoni au matumizi ya andiko la msingi yanapokosa kutajwa, yeye huuliza swali hususa la ziada ili kuvuta uangalifu kwa habari hiyo. Kwa njia hiyo, yeye hutusaidia tufikie mkataa ufaao na tujue jinsi ya kutumia yale tunayojifunza maishani mwetu.
4 Kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi hujitahidi hatua kwa hatua kuboresha uwezo wake wa kufundisha. Yeye hatoi maelezo kupita kiasi bali hututia moyo tutoe maelezo—kwa maneno yetu wenyewe, mafupi, na yenye kulenga shabaha. Huenda mara kwa mara akatukumbusha kwamba elezo la kwanza kwenye fungu lapaswa kuwa fupi, jibu la moja kwa moja kwa swali lililochapwa. Maelezo ya ziada kutoka kwa wasikilizaji yaweza kuvuta uangalifu kwenye matumizi ya andiko, hoja zenye kutegemeza, au kwenye matumizi yanayofaa ya habari hiyo. Kwa kuchochea utayarishaji wa kibinafsi na wa familia, kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi huchochea tamaa ya kila mtu ya kushiriki.
5 Tukiwa ‘watu waliofundishwa na Yehova,’ twathamini “zawadi zikiwa wanadamu,” kama viongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi, “wafanyao kazi kwa bidii katika . . . kufundisha.”—Isa. 54:13; Efe. 4:8, 11; 1 Tim. 5:17.