Funzo la Kitabu la Kutaniko Huchochea Utendaji Wenye Kuelimisha
1 Funzo la Kitabu la Kutaniko hutimiza fungu la maana sana katika programu yenye kuelimisha ya tengenezo la Yehova. Vikundi vya funzo la kitabu vimetawanyika kotekote kwenye eneo, ikifanya iwe rahisi kwa wote kuhudhuria. Kukiwa na funzo lililo katika ujirani wao, wenye kupendezwa huenda wakakubali kwa wepesi mwaliko wa kuhudhuria.
2 Jitihada yafanywa ili kuweka kila kikundi kikiwa kidogo. Hili lamwezesha kiongozi atoe msaada wa kibinafsi kwa kila mtu. Si wote wanaojifunza kwa kiwango kilekile. Kama mtu yeyote ana ugumu wa kuelewa jambo hata baada ya kujifunza somo hilo mapema, kiongozi anaweza kulizungumzia pamoja naye zaidi baada ya funzo. Isitoshe, kukiwa na kikundi kidogo, kuna fursa nyingi zaidi za kutoa maelezo na kushiriki kusoma maandiko. Je! wewe huchangia mazungumzo kwa kutoa maelezo kwa ukawaida? Je! wewe hujaribu kujibu kwa maneno yako mwenyewe? Utayari wako wa kushiriki waweza kukunufaisha wewe na wengine. Unapotayarisha, tumia uwezo wako wa kufikiri kutambua jinsi unavyoweza kutumia kibinafsi mambo kadhaa yaliyo kwenye somo.—Ebr. 5:14.
3 Kwa kuchunguza njia za kufundisha zinazotumiwa na kiongozi wa funzo la kitabu, unaweza kujifunza jinsi ya kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani katika njia yenye kupendeza zaidi na yenye ufundi. Baada ya mafungu kusomwa na ndugu mwenye ustahili, maswali huzungumzwa. Kiongozi wa funzo hutia moyo wote waseme kwa sauti yenye kusikika. Kadiri wakati uruhusuvyo, yeye hujitahidi kufanya watu wahisi huru kutoa maelezo juu ya maandiko yaliyowekwa bila manukuu ya kutusaidia tuelewe jinsi yanavyotumika. (Linganisha Nehemia 8:8.) Wakati mwingine anaweza kuongeza elezo lake fupi lenye kuelewesha au atumie maswali ya kuongezea kuelewesha jambo hususa. Mfano au kielelezo chaweza kutusaidia tuone jinsi habari hiyo ihusuvyo maisha yetu.
4 Hudhurio la mkutano katika Mafunzo kadhaa ya Kitabu ya Kutaniko liko chini sana. Je! wewe huhudhuria kwa ukawaida? Ikiwa sivyo, umekuwa ukikosa uandalizi wa maana sana. Mpango wa funzo la kitabu ni mojapo njia ambazo Yehova aonyesha kutujali sisi. (1 Pet. 5:7) Yeye ataka tufanye maendeleo katika ujuzi na hekima ili kwamba tuwe wenye nguvu kiroho. Kwa upande ule mwingine, Shetani anataka kupunguza ukuzi wetu wa kiroho na kutudhoofisha ili tusimtumikie kabisa Yehova na tengenezo lake. Usiruhusu hili litendeke! Acha hali yenye uchangamfu, yenye upendo katika kikundi hiki chenye ukaribu iguse moyo wako na ikuchochee uendelee kumsifu Yehova.—Linganisha Zaburi 111:1.
5 Mikutano ya utumishi iliyopangwa kufaa wahubiri inapangwa mahali pengi pa funzo la kitabu. Hiyo yaweza kuwa ya katikati ya juma, mwisho-juma, au ushahidi wa jioni. Kiongozi wa funzo la kitabu huhakikisha kwamba kuna eneo la kutosha na kwamba mtu fulani atakuwako ili kuongoza shambani. Mikutano ya huduma ya shambani haipaswi kupita dakika 10-15. Kiongozi aweza kuchunguza kifupi andiko la siku ikiwa linahusu utendaji wetu wa kuhubiri naye atoe pendekezo moja au mawili hususa ya utumishi wa shambani au atoe wonyesho mfupi wa toleo la karibuni.
6 Kiongozi ajitahidi kwa kipindi cha wakati kuhubiri na kila mmoja katika kikundi chake, akitoa kitia-moyo kinachofaa na mazoezi.—Linganisha Marko 3:14; Luka 8:1.