Mpango wa Funzo la Kitabu la Kundi
Sehemu ya 1: Daraka la Kiongozi wa Funzo
1 Funzo la Kitabu la Kundi hutimiza fungu muhimu katika usitawi wa kiroho wa watu wa Yehova. Katika miezi iliyo mbele, tutachunguza pande mbalimbali za mpango wa Funzo la Kitabu la Kundi na kufikiria jinsi tuwezavyo kunufaika. Katika toleo hili tunataka kuelekeza fikiria juu ya jinsi kiongozi wa funzo la kitabu la kundi awezavyo kufanya funzo liwe lenye kutia moyo na lenye kutia imani nguvu.
2 Ili awe mwenye mafanikio katika kufundisha kwake, kiongozi apaswa kujitayarisha vizuri. Akiwa mwanafunzi mwenye kuchukua kwa uzito funzo la Neno la Mungu, si kwamba tu ni lazima ajue majibu kwa kila swali bali apaswa pia kuelewa kwa nini jibu hilo ni sahihi. Jitihada yake yapaswa kuwa ni kusaidia wote katika funzo wajue sababu za majibu. (1 Pet. 3:15) Hilo litaimarisha uthamini wao kwa habari hiyo.
MIRADI KATIKA KUONGOZA FUNZO
3 Mradi mmoja wa kiongozi ni kutumia habari katika funzo kutia nguvu imani ya wote wanaohudhuria na kuwachochea watake kufanya mapenzi ya Mungu kikamili zaidi. (Zab. 110:3; 2 The. 1:3-5) Ili kutimiza hilo, lazima kiongozi atue mahali penye kufaa ili ‘kushindilia’ mambo ambayo hujenga uhakika wa moyoni katika Yehova, Neno lake, na tengenezo lake. (Gal. 6:6, NW, Ref. Bi. kielezi cha chini) Maswali yaliyotungwa kwa ustadi yaweza kutumiwa kutokeza mambo hayo yenye kujenga imani kadiri wakati uruhusuvyo.
4 Mradi mwingine ni kusaidia wote waone jinsi wanavyoweza kutumia habari katika njia yenye manufaa. Waweza kuitumiaje katika huduma ya shambani? Katika kutia akina ndugu moyo pamoja na wapya? Katika kutia nguvu familia zao na wao wenyewe? Viongozi wa Funzo la Kitabu la Kundi Watayarishapo kila somo, wapaswa kujaribu kutambua matumizi yenye manufaa ya mambo hususa katika funzo.
5 Habari fulani huenda ikatumiwa kusaidia watu wa ukoo wasio waamini, wanashule wenzi, au wafanyakazi wenzi. Habari nyingine huenda ikasaidia wale walio katika familia zilizogawanyika au labda katika familia za mzazi mmoja. Kiongozi aweza kuwauliza maswali wale wanaohudhuria ili kuwasaidia wafikiri na kuona jinsi wanavyoweza kutumia kwa njia yenye manufaa habari inayozungumzwa. Kiongozi apaswa kujitahidi kuendeleza funzo likiwa lenye kupendeza, akilifanya liwe zaidi ya mazungumzo ya maswali na majibu.—Linganisha 1 Wakorintho 14:9, 19.
ONYESHA KUPENDEZWA KWA KIBINAFSI
6 Kwa kupendezwa kibinafsi na kila mmoja katika kikundi, kiongozi aweza kutia moyo ushiriki kamili. Wale ambao kidogo ni waoga waweza kugawiwa kimbele wasome andiko, au waweza kupewa swali kimbele wajitayarishe kujibu. Wote wapaswa kujitahidi kutoa maelezo kwa maneno yao wenyewe. Kwa kusikiliza maelezo kwa makini, kiongozi aweza kuamua kama baadhi yao wahitaji usaidizi wa kibinafsi. Aweza kutumia wengine wenye ujuzi katika kikundi watoe uangalifu huo kwa watu mmoja mmoja.
7 Funzo la Kitabu la Kundi ni baraka kwetu. Linatutolea fursa ya kukutana katika vikundi vidogo na kupokea uangalifu zaidi wa kibinafsi. Haitupasi kamwe kuliona kuwa lenye umaana mdogo kuliko ile mikutano mingine. Kiongozi wenu wa Funzo la Kitabu la Kundi huchukua kwa uzito daraka lake la kutumia kila funzo kuitia imani yako nguvu katika Yehova na kujenga uthamini wako kwa maandalizi ya kiroho ya Mungu.