Mhofu Yehova Mchana Kutwa
1 “Kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA ndio mwanzo wa hekima.” (Zab. 111:10) Hutuchochea kufanya kazi njema na kutusaidia tujiepushe na lililo baya. (Mit. 16:6) Hofu hii ni staha yenye kina kwa Muumba wetu, ambayo hutuchochea kuepuka kutompendeza na kutomtii. Ni jambo ambalo twahitaji kusitawisha na kuonyesha mchana kutwa.—Mit. 8:13.
2 Kila siku, roho ya ulimwengu wa Shetani hutusonga sana ili tujipatanishe na njia zake mbovu. (Efe. 6:11, 12) Mwili wetu usio mkamilifu ni wenye dhambi na kwa asili huelekea kwenye mabaya. (Gal. 5:17) Kwa sababu hiyo, ili kutii amri za Yehova, tuwe na furaha, na tupate uhai, lazima tumhofu mchana kutwa.—Kum. 10:12, 13.
3 Kwenye Waebrania 10:24, 25, twahimizwa kukutana pamoja ili kutiana moyo “zaidi sana hivyo” nyakati hizi tunamoishi. Kuhudhuria mikutano kwa ukawaida ni muhimu ikiwa tutaokoka siku hizi za mwisho. Hofu yetu ya kutomchukiza Mungu hutuchochea tuhudhurie na kuthamini sana kusudi la mikutano. Wale wanaomhofu Mungu huona kushiriki katika mikutano ya Kikristo kuwa pendeleo kubwa.
4 Kutii amri ya kuhubiri habari njema za Ufalme ni njia nyingine ya kuonyesha kwamba twamhofu Mungu. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 10:42) Lengo letu kuu la kuhubiri ni kusaidia wengine wasitawishe hofu ya Yehova na kutii mapenzi yake. Twatimiza hilo kwa kufanya ziara za kurudia, tukijitahidi kuanzisha mafunzo ya Biblia, kisha kufundisha wengine amri zote za Mungu. Kwa njia hiyo twaonyesha hofu yetu kwa Yehova na upendo wetu kwa jirani.—Mt. 22:37-39.
5 Wale wasiomhofu Mungu hukosa kusitawisha uthamini kwa mambo ya kiroho, nao huathiriwa na hewa hatari ya ulimwengu huu, au mtazamo wake mbaya wa kiakili. (Efe. 2:2) Na tuazimie kwa uthabiti “kumtolea Mungu utumishi mtakatifu kwa hofu ya kimungu na kicho.” (Ebr. 12:28) Hivyo, tutapokea baraka za wale ambao humhofu Yehova mchana kutwa.