Acheni Sote Tumheshimu Yehova na Mwana Wake
Jinsi Ambavyo Wote Watakaohudhuria Ukumbusho Aprili 8 Watanufaika Sana
1 Ni nani leo wanaoheshimiwa sana? Ni wale wafanyao matendo yaonwayo kuwa yenye fahari na ulimwengu. Hata hivyo, mara nyingi, matendo yao husahaulika upesi. Lakini vipi matendo yanayonufaisha wanadamu kikweli? Tutazingatia tendo kuu zaidi kati ya matendo hayo tunapoadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana baada ya jua kushuka siku ya Aprili 8, 2001.
2 Ni nani anayestahili heshima ya pekee? Biblia hujibu hivi: “Wastahili, Yehova, . . . kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” (Ufu. 4:11) Akiwa Muumba, Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote. Ataendelea kustahili heshima milele na milele!—1 Tim. 1:17.
3 Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alifanya matendo ambayo yatawaletea wanadamu baraka tele kwa umilele. Alimwiga Baba yake kikamilifu. (Yn. 5:19) Utii wake mshikamanifu na utumishi wake mwaminifu ulimfanya “astahili kupokea uwezo na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka.” (Ufu. 5:12) Baba yake alimheshimu kwa kumtawaza awe Mfalme. (Zab. 2:6-8) Sisi nasi, tutakuwa na fursa ya kumheshimu Baba na Mwana tuadhimishapo Mlo wa Jioni wa Bwana Aprili 8, 2001.
4 Kwa kusikitisha, ni watu wachache tu katika historia yote ambao wamewapa Yehova na Mwana wake heshima wanayostahili. Nyakati nyingine, hata watu wa Mungu wa kale, Waisraeli, walimtolea Yehova utumishi wa kijuujuu tu. Huo ulikuwa ukosefu mkubwa wa heshima. (Mal. 1:6) Heshima inayofaa hutaka utii na uaminifu kwa sababu tunapenda na kuthamini yale yote ambayo Yehova na Mwana wake wametufanyia. Hofu na staha yetu ya kimungu huonyeshwa na heshima hiyo, huku tukimkiri Yehova na Yesu katika njia zetu zote. Kutaniko la Kikristo hujitahidi kufundisha na kusaidia wengine wafanye vivyo hivyo.
5 Pindi ya Pekee ya Kuonyesha Heshima: Mwadhimisho wa Ukumbusho ndio mkutano wa maana zaidi kwa watu wa Yehova kila mwaka. Kila mmoja aliye na tamaa ya kumtumikia na kumheshimu Yehova apaswa kuwapo. (Luka 22:19) Tunatazamia kwamba zaidi ya watu milioni 14 watahudhuria Ukumbusho kutia ndani Mashahidi watendaji milioni 6. Hiyo itakuwa fursa nzuri kama nini ya kumheshimu Baba yetu wa mbinguni! Ijapokuwa mwadhimisho huo wakazia fikira Yesu, heshima na staha kwa yale aliyotimiza humtukuza Baba aliyemtuma.—Yn. 5:23.
6 Tunaweza kufanya nini ili kuunga mkono pindi hii ya pekee? Twaweza kusaidia wanaopendezwa wanufaike kabisa. Wasihi wahudhurie, na ikiwa wanahitaji msaada wa kufika jitolee kuwasaidia. Elezea kusudi la hotuba. Wajulishe kwa wengine. Kile wanachoona na kusikia huenda kikawachochea watake kuungana nasi katika kumheshimu Yehova.
7 Usipuuze yawezayo kutimizwa na programu hiyo. Mwanafunzi mmoja wa chuo kikuu alisema hivi: “Nimehudhuria Ushirika Mtakatifu kanisani mwangu mara nyingi, lakini hii ni tofauti sana. Naona hasa ni kama vile ambavyo Biblia husema, nafikiri nyinyi mna kweli.” Alianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na upesi akabatizwa.
8 Saidia Wapya Wafanye Maendeleo: Uwe macho kutambua wapya wanaohudhuria Ukumbusho na uwatembelee upesi baada ya mkutano huo, ili kupitia mambo yenye kutia moyo waliyojifunza na kuyaona. Wajulishe mikutano ile mingine, ambamo wanaweza kuongeza ujuzi wao wa Biblia. Kwa kuchunguza sura ya 17 ya kitabu Ujuzi, “Pata Usalama Miongoni mwa Watu wa Mungu,” watajua maandalizi mengi sana ya kiroho yanayotolewa na kutaniko, ambayo wanaweza kufaidika kwayo. Panga watazame vidio Our Whole Association of Brothers ili waweze kujionea wenyewe umoja, shangwe, na bidii ya watu wa Yehova!
9 Ni muhimu wapya wafahamu jinsi wao wenyewe wawezavyo kumwonyesha Yehova heshima na staha. Waeleze kwamba Yehova hupendezwa na sala za moyoni naye ni chanzo daima cha burudisho la kiroho. (1 Yh. 5:14) Ukitumia somo la 8 hadi 12 katika broshua Anataka, eleza aina ya mwenendo ambao humheshimu Yehova. Kwa kuzungumzia yaliyoandikwa katika broshua Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini?, ukurasa wa 30-31, tia moyo wapya wafikirie jinsi wanavyoweza kumheshimu Yehova kwa kuhubiri.
10 Kuthamini dhabihu ya Yesu na pendeleo letu la kutumikia kama wanafunzi wake humheshimu Baba na huwaletea wengine baraka. Yesu aliahidi hivi: “Ikiwa yeyote angenihudumia mimi, Baba atamheshimu yeye.”—Yn. 12:26.