Kupangwa “kwa Adabu na kwa Mpango”
1 Ili kusanyiko la wilaya lifaulu, lazima kuwe na jitihada za pamoja. Wasimamizi wa mkusanyiko hupanga mahali panapofaa pa kukusanyikia na vilevile mahali pa kulala. Watu na familia mbalimbali hufanya mipango yao ya kusafiri na ya mahali pa kulala. Na makutaniko hupanga kuwe na watu wa kujitolea katika idara nyingi zinazohitajiwa ili kuwezesha mkusanyiko uendelee. Lengo ni ili “mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.”—1 Kor. 14:40.
2 Unapojitahidi kuunga mkono mpango wa mkusanyiko, kumbuka kwamba nyakati nyingine matayarisho yanafanywa kwa miezi, na hata miaka kadhaa. Mamia ya akina ndugu hutumia wakati mwingi kupanga mambo. Hayo yatia ndani kukodi majengo, kukusanya vifaa, na kutafuta wafanyakazi. Wote hupata baraka za kiroho kwa sababu ya matayarisho hayo ya mapema. Twaweza kufanya nini ili tusaidie?
3 Shirikiana na Mipango ya Mahali pa Kulala: Ni muhimu sana kwamba sisi sote tushirikiane na mipango ya mkusanyiko. Hiyo ni lazima hasa tunapopangia mahali petu pa kulala. Kwa kweli, vyumba vingi vyahitajiwa kwa ajili ya kila mkusanyiko. Wengi wa ndugu zetu wana fedha chache na lazima wategemee vyumba visivyo ghali. Jitihada nyingi sana zimefanywa kujadiliana ili kupata bei zilizo nafuu kabisa. Lazima tufikirie kwa upendo mahitaji ya wengine na ‘tuangalie, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yetu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.’—Flp. 2:4.
4 Kutii kwetu miongozo ya mkusanyiko kuhusu mahali pa kulala huwanufaisha wote wanaohusika. Kupuuza miongozo hiyo hutokeza matatizo yasiyo ya lazima. Jinsi gani? Tunapotii madokezo hayo, wale wanaohusika wanajua mapema wamehifadhi vyumba vingapi na ni wageni wangapi watakaokuwapo. Hiyo husaidia katika kupanga na yaweza kutokeza uhusiano mzuri miaka inayofuata.
5 Fikiria Matokeo Haya Mazuri: Baada ya mkusanyiko mmoja, mwalimu mkuu alisema hivi: “Nimegundua kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wanyofu sana katika yote wanayofanya. Walipokaa katika shule yangu hawakuleta matatizo yoyote. Badala yake, walienenda vizuri sana na hawakuharibu chochote. Watoto wao hawakukimbia-kimbia huku na huko uwanjani. Ni furaha yangu kuwaalika tena katika shule hii.” Ingekuwa vizuri kama nini ikiwa wote wanaotukodisha majengo yao wangesema hivyo! Hilo lingetoa ushahidi mzuri kama nini!
6 Msimamizi wa hoteli fulani alisema: “Sidhani nimewahi kuona kikundi kikubwa kilichotenda kulingana na imani yao kama Mashahidi wa Yehova. Twatumaini kwamba mtarudi.” Maelezo hayo yanaonyesha kwamba mwenendo mzuri unatufurahisha na pia unafurahisha wengine wanaotutazama ulimwenguni pote.
7 Njia Rahisi Ambazo Twaweza Kushirikiana: Kuna mambo rahisi ambayo twaweza kufanya ili kushirikiana na mpango wa mkusanyiko wa kuhifadhi vyumba ukipanga kukaa hotelini. (1) Usihifadhi vyumba vingi vya hoteli usivyoweza kuvitumia. (2) Tuma amana ya kutosha kuweza kuhifadhi chumba kupitia Idara ya Mahali pa Kulala ya mkusanyiko unaotaka kuhudhuria. (3) Usitumie vibaya vifaa vyovyote vya hoteli. (4) Kumbuka kwamba wenye hoteli wanatazamia ifaavyo tuishi kulingana na kanuni zao.
8 Tukiwa watumishi wa Yehova Mungu, tuna fursa ya kuonyesha utu wake katika yote tufanyayo. Hii yatia ndani kufanya mipango na kuhudhuria mikusanyiko inayohusiana na jina la Mungu. Kumbuka kwamba, yeye ni “Mungu, si wa kukosa utaratibu, bali wa amani.” (1 Kor. 14:33) Hivyo, acheni tuazimie kwamba watazamaji watatambua sifa hii ya Yehova kutokana na yale wanayoona tukitenda—mwenendo wetu tunapopanga na kuhudhuria Mkusanyiko wa Wilaya wa “Walimu wa Neno la Mungu.” Watu wenye unyofu wa moyo na watambue kwamba wakusanyikaji wa Yehova wamepangwa kwa “adabu na kwa mpango.”—Zab. 68:26.