Sanduku La Swali
◼ Ni habari gani inayopasa kuzungumziwa katika mikutano ya utumishi wa shambani?
Kusudi la mkutano wa utumishi wa shambani ni kutusaidia tukazie fikira utendaji wetu unaofuata—huduma. Kwa hiyo, mwenye kuongoza mkutano huo apaswa kuwa amejitayarisha vizuri na awe tayari kusema jambo fulani hususa, linalotia moyo, na lenye kutumika. Ikiwa andiko la siku lazungumzia moja kwa moja kazi ya kuhubiri, linaweza kusomwa na kuzungumziwa kifupi. Hata hivyo, mkutano huo wapaswa kukazia hasa kazi ya kuhubiri, ukisaidia wote wanaoenda kuhubiri wawe tayari kutimiza huduma yao siku hiyo.—2 Tim. 4:5.
Mambo yanayofaa kutoka katika Huduma Yetu ya Ufalme yanaweza kuzungumziwa ili kujulisha wote toleo la wakati huo na jinsi ya kulitoa. Siku ya Magazeti, onyesho laweza kutolewa kwa kutumia utoaji ulio katika safu yenye kichwa “Mambo ya Kusema Kuhusu Magazeti.” Katika mahubiri mengine, utangulizi mmoja au tangulizi mbili kutoka kitabu Kutoa Sababu zinazofaa eneo lenu zaweza kukaziwa. Sehemu moja ya huduma yaweza kuzungumziwa au kutolewa onyesho, kama vile jinsi ya kutumia Biblia mlangoni, jinsi ya kushughulika na vizuia-mazungumzo ambavyo huenda vikatokezwa, jinsi ya kumpendekezea mtu funzo la Biblia, au jinsi ya kurudia watu wanaopendezwa.
Mikutano ya utumishi wa shambani haipaswi kupita dakika 10 hadi 15, ambazo zatia ndani kupanga kikundi, kugawa eneo, na kutoa sala. Wakati wa kuondoka, wote wapaswa kujua wanaenda na nani na eneo watakalohubiri, na wanapaswa kwenda kwenye eneo bila kukawia. Kwa sababu mkutano huo ni mfupi, ni muhimu kila mtu afike kwa wakati. Ikiwa mkutano wa utumishi wa shambani unafanywa baada ya Funzo la Mnara wa Mlinzi, wapaswa kuwa mfupi zaidi. Si lazima andiko la siku lisomwe, kwa kuwa tayari watu wamefurahia mazungumzo murua ya Kimaandiko.
Ndugu waliobatizwa wenye kustahili wapaswa kupewa mgao wa kuongoza mkutano wa shambani mapema. Ikiwa wakati mwingine hakuna ndugu wa kuongoza mkutano huo, wazee wanapaswa kuchagua akina dada waliobatizwa wanaoweza kufanya hivyo kukiwa na uhitaji. Akiwa ameketi, dada huyo anaweza kuanzisha mazungumzo mafupi ya andiko la siku au mambo mengine yanayohusiana na utumishi wa shambani. Anapaswa kufunga kitambaa kichwani.
Mikutano ya utumishi wa shambani huandaa fursa bora ya kutiwa moyo na kutayarishwa kwenda katika huduma. Kiongozi wa mkutano huo akijitayarisha vizuri, wote watanufaika.