Sanduku la Swali
● Mikutano ya utumishi wa shambani inapasa kuongozwaje?
Mkutano wa utumishi wa shambani ni mpango wa kundi uliosimamishwa imara. Unapasa uwe wenye utaratibu na kuongozwa kwa heshima. Mwelekeo na adabu ya wale wanaouhudhuria inapasa iwe kama ilivyo wakati wa kuhudhuria mikutano mingine ya kundi. Mkutano huo unapasa uanze kwa wakati wake hata ikiwa inajulikana kwamba wengine watakuja baadaye. Yule ambaye amepewa mgawo wa kuongoza mkutano huo anapaswa ajitayarishe kutoa kitu fulani chenye mafaa ambacho kinaweza kutumiwa siku hiyo katika utumishi. Huduma ya Ufalme Yetu inaandaa habari na madokezo yenye msaada kwa ajili ya mkutano huo.
Tunaweza kutumiaje habari hizo kwa matokeo na kunufaisha wote? (1) Sikiliza kwa umakini habari inayozungumziwa kama ilivyoorodheshwa chini ya juma linaloonyeshwa. Mathalani, habari ya kuzungumziwa kwa juma linaloanza Februari 13-19 ni juu ya jinsi ya kuweka msingi au kutayarisha mapema kwa ajili ya ziara za kurudia. Tukiwa na jambo hilo wazi katika akili zetu basi (2) fikiria maswali yanayozushwa. Ungejibuje kila swali ukiulizwa kwenye Mkutano wa Utumishi wa Shambani? Baada ya kufanya hivyo utakuwa umejitayarisha ili ushiriki katika mazungumzo wakati wa Mkutano wa Utumishi wa Shambani wakati ambapo maswali hayo yataulizwa na mambo hayo yatakaziwa. Labda maelezo yako yatatoa madokezo fulani yenye mafaa kwa wale wanaohudhuria kuhusu jinsi, katika habari hii, tunavyoweza kujitayarisha mapema kufanya ziara za kurudia. Utaratibu huo huo unatumiwa kwa mambo yanayoorodheshwa kwa ajili ya mazungumzo kila juma. Yule ambaye amepewa mgawo wa kuongoza atataka sana kujitayarisha akiwa na majibu na madokezo yanayofaa kwa mambo yanayozungumziwa.
Si lazima kuzungumzia andiko la siku kwenye kila mkutano. Ikiwa ni wazi kwamba andiko la siku hiyo linaandaa msingi wa kutoa kitia-moyo katika utumishi wa shambani, linaweza kuzungumziwa kifupi. Mkutano huo unapasa ufanywe mapema vya kutosha ili kuruhusu wakati kamili ulioratibiwa utumiwe shambani. Unapasa kuwa wenye urefu wa dakika 10 hadi 15. Hata hivyo, unaweza kuwa mfupi kidogo ikiwa unafuata mkutano wa kawaida wa kundi. Ratiba ya mapainia inapasa ifikiriwe, kwa kuwa mikutano ya utumishi wa shambani mirefu au yenye kuchelewa inaweza kuwalemea wale ambao wanapaswa kushikilia ratiba ya wakati kwa ukaribu sana.
Mipango inapasa ifanywe ili kila mmoja aliyepo awe na mahali alipogawiwa kufanya kazi. Bila shaka, huenda wengine wakawa wamefanya mipango ya kibinafsi katika utendaji wa ziara za kurudia au funzo la Biblia na hawapaswi kupewa mgawo wa eneo la kufanyia kazi.
Wote waliopo wanapaswa kutega sikio na kushirikiana wakati wote wa mkutano mpaka vikundi vya kwenda shambani vinapopangwa na sala imetolewa. Wale ambao tayari wamefanya mipango wanaweza kujulisha jambo hilo. Migawo hususa ya vikundi au maeneo inapasa imakamilishwe kabla ya kumalizia mkutano wa utumishi wa shambani—si mahali pa kuegesha magari wala mahali penginepo peupe. Mkutano wa utumishi wa shambani unapasa umalizwe kwa sala. Tunaweza kutazamia kwa uhakika baraka kubwa zaidi za Yehova juu ya kazi ya kuhubiri kwa siku hiyo ikiwa wote wanaohusika wanafuata madokezo haya.