Kwa Nini Twendelee Kuhubiri?
1 Je, kazi ya kuhubiri imefanywa kwenu kwa muda mrefu sana? (Mt. 24:14) Ikiwa ndivyo, huenda ukahisi kwamba eneo la kutaniko lenu limekamilishwa. Sasa unapohubiri, labda watu wengi unaowakuta hawapendezwi na ujumbe wa Ufalme. Hata hivyo, ona yale yanayosemwa kuhusu wanafunzi wa kweli wa Yesu kwenye ukurasa wa 141 wa kitabu cha Unabii wa Isaya II: “Mahali fulani fulani, huenda matokeo ya huduma yao yakaonekana kuwa si kitu yakilinganishwa na kiasi cha kazi na jitihada wanazofanya. Hata hivyo, wao huvumilia.” Lakini kwa nini twendelee kuhubiri?
2 Mkumbuke Yeremia: Iwe watu watasikiliza au hawatasikiliza, lazima tuvumilie katika kazi ya kuhubiri. Yeremia alihubiri kwa miaka 40 katika eneo lilelile hata ingawa ni wachache tu waliomsikiliza huku wengi wakipinga ujumbe wake. Kwa nini Yeremia alivumilia? Kwa sababu alikuwa akifanya kazi ambayo Mungu alikuwa amemwamuru afanye. Pia kujua kwake yale ambayo yangetokea wakati ujao kulimchochea aendelee kuhubiri.—Yer. 1:17; 20:9.
3 Hali yetu inafanana na hiyo. Yesu “a[me]tuagiza sisi tuwahubirie watu na kutoa ushahidi kamili kwamba Huyu ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa hakimu wa walio hai na wafu.” (Mdo. 10:42) Ujumbe tunaohubiri unaweza kuleta uhai kwa wale wanaosikiliza au kifo kwa wale wanaokataa. Watu watahukumiwa kulingana na jinsi wanavyoitikia habari njema. Kwa hiyo, daraka letu ni kufanya hasa kama tuliyoamriwa. Kuhubiri hutupatia fursa ya kuwaonyesha watu upendo wetu mwingi, hata wasipotusikiliza. Pia twaonyesha ujitoaji wetu kwa Yehova tukiendelea kufanya yale ambayo twapaswa kufanya. Lakini kuna sababu nyingine ya kuendelea kuhubiri.
4 Tunafaidika: Hata itikio liweje katika eneo, kufanya mapenzi ya Mungu hutupatia amani ya moyoni, uradhi, na furaha, ambazo haziwezi kupatikana kwa njia nyingine. (Zab. 40:8) Maisha yetu huwa na maana. Kadiri tunavyoshiriki katika huduma, ndivyo mioyo na akili zetu zinavyoelekezwa kwenye tumaini na shangwe ya kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu. Kufikiria daima ahadi hizo za Kimaandiko huboresha hali yetu ya kiroho na kuimarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova.
5 Hata kama hatupati matokeo ya haraka katika kazi yetu ya kuhubiri, huenda mbegu ya kweli iliyopandwa kwenye moyo wa mtu fulani ikachipuka kwa wakati ufaao wa Yehova. (Yn. 6:44; 1 Kor. 3:6) Hakuna mmoja wetu anayejua ni watu wangapi ambao bado watajifunza juu ya Ufalme kupitia jitihada za watu wa Yehova, hapa kwetu au ulimwenguni pote.
6 Twapaswa kutii maagizo haya ya Yesu kwa uharaka: “Fulizeni kutazama, fulizeni kuwa macho, kwa maana hamjui ni lini ulio wakati uliowekwa rasmi. Lakini lile niwaambialo nyinyi nawaambia wote, Fulizeni kulinda.” (Mr. 13:33, 37) Hivyo basi, sote na twendelee kutangaza habari njema za Ufalme, tukifurahisha moyo wa Yehova tunaposhiriki kutakasa jina lake kuu na takatifu.