Kuwasaidia Wengine Wamtukuze Yehova
1 Watu wanatangaziwa ujumbe muhimu kotekote duniani leo: “Hofuni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imewasili, na kwa hiyo mwabuduni Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na mabubujiko ya maji.” (Ufu. 14:6, 7) Ni pendeleo letu kushiriki kutangaza ujumbe huo. Watu wanahitaji kujua nini kumhusu Yehova ili wamhofu na kumwabudu?
2 Jina Lake: Watu wanahitaji kumjua Mungu wa kweli kwa jina ili wamtofautishe na miungu mingi ya uwongo inayoabudiwa leo. (Kum. 4:35; 1 Kor. 8:5, 6) Waandishi wa Biblia walilitumia jina tukufu la Yehova zaidi ya mara 7,000. Ijapokuwa sisi hutumia busara tunapowajulisha watu jina la Mungu, hatupaswi kamwe kulificha wala kuacha kulitumia. Mungu anataka wanadamu wote walijue jina lake.—Zab. 83:18.
3 Sifa Zake: Ili wamtukuze Yehova, watu wanahitaji kujua sifa zake. Inatubidi kuwafundisha kuhusu upendo wake mkuu, hekima yake isiyo na kifani, haki kamili, na kwamba yeye ndiye mwenye nguvu zote. Wanahitaji pia kujua kuhusu rehema yake, fadhili yake yenye upendo, na sifa nyingine nzuri ajabu. (Kut. 34:6, 7) Ni lazima pia wafundishwe kumhofu Mungu kwa njia inayofaa na kumheshimu, wakitambua kwamba wataweza kuishi milele tu iwapo watapata kibali chake.—Zab. 89:7.
4 Kumkaribia Mungu: Ili waokoke hukumu ya Mungu inayokuja, ni lazima watu wamwitie Yehova kwa imani. (Rom. 10:13, 14; 2 The. 1:8) Jambo hilo linatia ndani mengi zaidi kuliko kujua tu jina la Mungu na sifa zake. Tunahitaji kuwasaidia watu kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, ili wamtumaini kwa moyo wao wote. (Mit. 3:5, 6) Wanapofuata yale wanayojifunza maishani mwao, wanaposali kwa Mungu kwa moyo wao wote, na kuona jinsi anavyowasaidia maishani, imani yao itaimarishwa, nao watasaidiwa kumkaribia Yehova.—Zab. 34:8.
5 Na tutangaze jina la Mungu kwa bidii na tuwasaidie wengine kumtumaini kabisa na kumhofu. Huenda tukaweza kuwasaidia wengi zaidi kumjua Yehova na kumtukuza kwa sababu yeye ni ‘Mungu wao wa wokovu.’—Zab. 25:5.