Pendezwa na ‘Mayatima’
1 Yehova ni “baba wa yatima.” (Zab. 68:5) Hangaikio lake kwa mayatima laonyeshwa na amri hii aliyolipa taifa la Israeli la kale: “Usimtese mjane ye yote aliyefiwa na mumewe, wala mtoto yatima. Ukiwatesa watu hao katika neno lo lote, nao wakanililia mimi, hakika yangu nitasikia kilio chao.” (Kut. 22:22, 23) Pia sheria ya Mungu ilitia ndani mipango ya kuwapa watu kama hao vitu vya kimwili. (Kum. 24:19-21) Chini ya mpango wa Kikristo, waabudu wa kweli wanasihiwa “kutazama mayatima na wajane katika dhiki yao.” (Yak. 1:27) Twaweza kumwigaje Yehova katika kuonyesha upendo kwa wale wanaolelewa katika familia za mzazi asiye na mwenzi au zilizogawanyika kidini?
2 Mafundisho ya Kiroho: Ikiwa wewe ni mzazi asiye na mwenzi au una mwenzi asiyeamini, inaweza kuwa vigumu kujifunza Biblia pamoja na watoto wako kwa ukawaida. Lakini funzo la Biblia la ukawaida ni muhimu ili wawe watu wazima waliokomaa na wenye usawaziko. (Mit. 22:6) Kuzungumza mambo ya kiroho pamoja nao kila siku pia ni muhimu. (Kum. 6:6-9) Nyakati nyingine, huenda ukahisi umevunjika moyo, lakini usikate tamaa. Mwombe Yehova ili akupe nguvu na mwongozo ‘unapoendelea kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.’—Efe. 6:4.
3 Ikiwa wahitaji msaada wa kushughulikia madaraka yako ya Kimaandiko, wajulishe wazee. Huenda wakaweza kukupa madokezo yanayofaa au kukusaidia kuanzisha ratiba nzuri ya kiroho inayofaa familia yako.
4 Jinsi Wengine Wanavyoweza Kusaidia: Katika karne ya kwanza, Timotheo alikuwa mtumishi wa Yehova mwenye bidii ijapokuwa alilelewa katika nyumba iliyogawanyika kidini. Jitihada zenye bidii za mama na nyanya yake za kumfundisha maandiko matakatifu katika ujana wake bila shaka zilimsaidia sana. (Mdo. 16:1, 2; 2 Tim. 1:5; 3:15) Hata hivyo alinufaika pia kwa kushirikiana na Wakristo wengine, kutia ndani mtume Paulo, ambaye alimtaja Timotheo kuwa ‘mtoto wake mpendwa na mwaminifu katika Bwana.’—1 Kor. 4:17.
5 Vivyo hivyo leo, inanufaisha kama nini wakati ndugu na dada wakomavu wanapopendezwa na mayatima katika kutaniko! Je, unajua majina yao? Je, wewe huongea nao kutanikoni na katika pindi nyingine? Waalike wajiunge nawe katika huduma ya shambani. Labda unaweza kuwaalika pamoja na mzazi wao mmoja au yule mzazi wao mwamini washiriki katika funzo lenu la familia au kwenye tafrija zenye kujenga. Vijana hao wanapokuona kuwa rafiki yao, bila shaka wataiga mfano wako na kukubali kitia-moyo chako.—Flp. 2:4.
6 Yehova anapendezwa sana na mayatima, naye anabariki jitihada zetu za kuwasaidia kufuata kweli maishani mwao. Wengi kati ya vijana ambao walilelewa katika familia za mzazi asiye na mwenzi au zilizogawanyika kidini wamepokea kitia-moyo na sasa wanatumikia kwa uaminifu wakiwa mapainia, watumishi wa huduma, wazee, waangalizi wasafirio, wamishonari, au washiriki wa familia ya Betheli. Sisi sote na tutafute njia ambazo twaweza ‘kupanuka’ na kupenda mayatima, tukimwiga Baba yetu wa mbinguni.—2 Kor. 6:11-13.