Uwe Mtakatifu Katika Mwenendo Wako Wote
1 Tukiwa watumishi wa Mungu mtakatifu, Yehova, tunajitahidi kuwa watakatifu katika mwenendo wetu wote. (1 Pet. 1:15, 16) Hilo linamaanisha kwamba tujitahidi kushika viwango vya Yehova katika maisha yetu yote. Kusanyiko la wilaya mwaka huu litatupatia nafasi ya pekee ya kuonyesha mwenendo mtakatifu.
2 Kwenye Mahoteli na Mabweni: Msimamizi mmoja wa hoteli iliyotumiwa na wajumbe wa kusanyiko mwaka jana alisema: “Mashahidi wa Yehova walikuwa watu wazuri sana walipokuwa hapa. . . . Tungependa wageni kama nyinyi.” Kutii vikumbusho vifuatavyo kutatusaidia tudumishe sifa yetu njema: (1) Usiweke vyumba vingi kuliko unavyohitaji, na usiweke watu wengi katika chumba chako kupita idadi inayoruhusiwa. (2) Ikiwa itakubidi ufute ombi lako la chumba, waarifu wenye hoteli mara moja. (3) Shirikiana kwa ukamili na wasimamizi. (4) Usipikie mahali ambapo haparuhusiwi kupikia na uwe mwangalifu kuhusu hatari za moto. (5) Toa bakshishi kwa ajili ya huduma bora. (6) Acha chumba chako cha kulala kikiwa safi. (7) Onyesha matunda ya roho unaposhughulika na wafanyakazi wa hoteli, hasa wakati wenye shughuli nyingi za kuingia na kutoka.—Gal. 5:22, 23.
3 Mwenendo wetu mwema unaweza kutoa ushahidi wenye nguvu. Mwaka uliopita Shahidi mchanga alimwomba kwa heshima mhudumu wa mapokezi wa hoteli karatasi na kalamu kisha akamshukuru. Jambo hilo lilimvutia mhudumu huyo, na alisikiwa akisema: “Siku hizi si rahisi kuona vijana wenye tabia nzuri kama hiyo.” Hata hivyo, katika hali chache, watoto wasiosimamiwa wameonekana wakicheza uwanjani, wakiongea kwa sauti kubwa, na kukimbia-kimbia kwenye vijia vya hoteli. Wazazi hawapaswi kuacha watoto bila uangalizi bali wanapaswa kuwasimamia na kuhakikisha kwamba mwenendo wao unamletea Yehova sifa.—Met. 29:15.
4 Mikahawani: Mhudumu mmoja katika mkahawa karibu na kusanyiko moja alisema hivi: “Mashahidi ni watu tofauti. Wanawaheshimu watu wengine.” Mwenendo mzuri hutia ndani kuepuka kusema kwa sauti kubwa na kucheka kwa njia inayoweza kuwasumbua wengine walio katika chumba cha kulia. Pia tunapaswa kukumbuka kwamba katika maeneo mengi ni jambo la kawaida kuachia wahudumu bakshishi, ikitegemea huduma uliyopewa. Hata tunapokuwa tukila na kunywa, tunajitahidi kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.—1 Kor. 10:31.
5 Kusanyikoni: Mwenendo wetu mzuri unapaswa kuonekana hasa tunapokuwa kusanyikoni. Tafadhali fuata mwongozo wa wakaribishaji, kwenye maegesho na kwenye uwanja. (Ebr. 13:17) Familia zinapaswa kuketi pamoja badala ya kuruhusu watoto, kutia ndani matineja, kuketi pamoja na vikundi vya vijana wengine. Vifaa vya kurekodia vya aina yoyote visiunganishwe na mfumo wa umeme au wa sauti wa kusanyiko na vitumiwe tu kwa njia ambayo haitawasumbua wengine. Ikiwa ungependa kupiga picha, usitumie mwangaza wakati wa vipindi. Peja na simu za mkononi zinapasa kurekebishwa ili zisiwasumbue wengine. Ukiona aksidenti uwanjani, tafadhali mjulishe mkaribishaji au Idara ya Huduma ya Kwanza.
6 Mwenendo wetu hututofautisha na wengine na humtukuza Mungu wetu. (1 Pet. 2:12) Kwenye kusanyiko, matendo ya Mashahidi wa Yehova yataonekana wazi. Kwa hiyo, azimia kuwa mtakatifu katika mwenendo wako wote.
[Maswali ya Funzo]
1. Kwa nini ni muhimu tuwe watakatifu katika mwenendo wetu wote?
2. Tunawezaje kuonyesha mwenendo mzuri hotelini?
3. Mwenendo wa Mashahidi wachanga unaweza kuwavutiaje wengine?
4. Tunaweza kuonyeshaje tunawajali wengine tunapokuwa kwenye chumba cha kulia?
5. Mwenendo mzuri unatia ndani nini tunapokuwa kusanyikoni?
6. Mwenendo wetu kusanyikoni humtukuzaje Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 5]
Onyesha Mwenendo Mtakatifu
◼ Tii matakwa yote ya mahali pa kulala
◼ Simamia watoto wako
◼ Wafikirie wengine