Uwe Kielelezo Katika Kazi Zilizo Bora
1 Tunapokusanyika kwa wingi kwenye makusanyiko ya wilaya, watu huona jinsi tunavyojiendesha na jinsi tunavyowatendea wengine. Kwa hiyo kila mmoja wetu anapaswa kutilia maanani shauri hili la Biblia: ‘Iweni timamu katika akili, katika mambo yote mkijionyesha wenyewe kuwa kielelezo cha kazi zilizo bora.’ (Tito 2:6, 7) Huenda jitihada za pekee zikahitajiwa ili ‘kuangalia, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yetu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.’ (Flp. 2:4) Hebu tuone mambo fulani ambayo tunaweza kutumia kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Mtukuzeni Mungu.”
2 Mipango ya Mahali pa Kulala: Tuna nafasi nzuri ya kuonyesha kazi zilizo bora kuhusiana na mipango ya mahali pa kulala. Iwe tutalala hotelini, kwenye bweni au darasani, itathaminiwa sana tukionyesha matunda ya roho ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Pia, fikiria mapema ikiwa unahitaji kubeba matandiko, vyakula, chandarua cha mbu na maji safi ya kunywa. Fuata sheria zote zilizowekwa na wasimamizi wa shule au wa mahali penginepo pa kulala ili kuepuka hatari za moto. Upishi hauruhusiwi katika madarasa na mabweni mengi.
3 Wazazi na Watoto: Vijana wengi ulimwenguni wana tabia mbaya, lakini watoto wetu ni tofauti, na hilo humletea Yehova na tengenezo lake sifa. Hata hivyo, nyakati nyingine matatizo yametokea kwa sababu ya watoto kutoangaliwa. (Mit. 29:15) Wazazi hawapaswi kuwaacha watoto peke yao mahali pa kulala au sehemu nyingineyo ya kusanyiko.
4 Kabla ya kusanyiko wazazi fulani wameona inafaa kuzungumza na watoto wao kuhusu mwenendo unaofaa. (Efe. 6:4) Wanasaidia watoto waelewe kwamba upendo wa kweli wa Kikristo “haujiendeshi bila adabu” wala “hautafuti masilahi yao wenyewe.” (1 Kor. 13:5) Kusanyiko la wilaya ni wakati uliotengwa wa kufundishwa na Yehova. Watoto na watu wazima vilevile wanaweza kuheshimu mpango huo kwa mwenendo wao kusanyikoni na kwingineko.—Isa. 54:13.
5 Mwenendo wetu mzuri unaweza kuzuia maoni yasiyofaa na uvutie watu kwenye ibada ya kweli. (Mt. 5:16; 1 Pet. 2:12) Na tuwatolee ushahidi mzuri wote tutakaokutana nao kwenye kusanyiko letu la wilaya kwa mwenendo wetu na jinsi tunavyowatendea. Tukifanya hivyo ‘tutajionyesha wenyewe kuwa kielelezo cha kazi zilizo bora’ nasi tutamtukuza Yehova.—Tito 2:7.
[Maswali ya Funzo]
1. Kwa nini twapaswa hasa kuutunza mwenendo wetu tunapokuwa katika kusanyiko la wilaya?
2. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusiana na mipango ya mahali pa kulala?
3, 4. Watoto wanawezaje kumletea Yehova sifa, na wazazi wana daraka gani?
5. Mwenendo wetu mzuri unaweza kuwa na matokeo gani kwa wengine?
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Wajali Wengine
▪ Uwe mwenye subira na uwaheshimu wafanyakazi wa mahali pa kusanyiko
▪ Tii sheria za mahali pa kusanyiko kwa manufaa ya wote
▪ Usitumie chochote kinachoweza kusababisha moto
▪ Waangalie watoto wako ifaavyo