Lazima Tuheshimu Mamlaka ya Yehova
Wewe hufikiria nini unaposikia majina haya ya watu wa kale: Kora, Dathani, na Abiramu? Uasi! Dhidi ya nini? Mamlaka ya Mungu. Masimulizi ya jinsi walivyojiendesha yanapatikana katika Hesabu sura ya 16, na mambo makuu ya kisa hicho yanapatikana katika makala, “Tii kwa Uaminifu Mamlaka ya Kimungu,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2002. Utafaidika kwa kusoma habari hizo na kutazama video Respect Jehovah’s Authority. Utaona matatizo yaliyozuka baina ya wana waaminifu wa Kora na baba yao mwasi, aliyekuwa akishindana na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. (Hes. 26:9-11) Drama hiyo ya mambo halisi yaliyotokea inapaswa kutuchochea tuwe washikamanifu kwa Yehova hata zaidi.
Unapotazama vidio hiyo, tafuta mambo ambayo yanaonyesha jinsi Kora na waasi wenzake walivyokosa kuwa washikamanifu kuhusiana na mambo haya sita muhimu: (1) Walikosaje kuheshimu mamlaka ya Mungu? (2) Waliachaje mambo kama vile kiburi, kujitakia makuu, na wivu yawaathiri? (3) Walikaziaje kutokamilika kwa wale waliokuwa wamewekwa rasmi na Yehova? (4) Walikuwa wamekuza mtazamo gani wa kulalamika? (5) Kwa nini hawakuridhika na mapendeleo yao ya utumishi? (6) Waliwatangulizaje marafiki na watu wa familia zao badala ya ushikamanifu kwa Mungu?
Fikiria jinsi mambo tunayojifunza katika drama hiyo ya Biblia yanavyohusu maoni yetu kuhusu mamlaka ya Mungu leo: (1) Tunapaswa kuitikiaje maamuzi ya wazee wa kutaniko, na kwa nini? (2) Tunawezaje kuondolea mbali nia zozote mbovu tulizo nazo? (3) Tunapaswa kuonaje kutokamilika kwa wale waliowekwa rasmi kuongoza? (4) Tunapaswa kufanya nini roho ya kulalamika ikianza kutia mizizi mioyoni mwetu? (5) Tunapaswa kuyaonaje mapendeleo yoyote ambayo tumepewa? (6) Ni nani ambao hawapaswi kamwe kutangulizwa mbele ya ushikamanifu wetu kwa Mungu, na huenda ikawa vigumu kufanya hivyo wakati gani hasa?
Baada ya kuzungumzia habari hii kutanikoni, mbona usiitazame tena vidio hiyo? Na ikazie hata zaidi akilini mwako sababu za kuheshimu mamlaka ya Yehova sikuzote!—Zab. 18:25; 37:28.