Sehemu ya 7—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kutoa Sala Wakati wa Funzo
1 Baraka ya Yehova ni muhimu ili mwanafunzi wa Biblia afanye maendeleo ya kiroho. (1 Kor. 3:6) Kwa hiyo inafaa kuanza na kumalizia funzo kwa sala. Nyakati nyingine tunaweza kutoa sala hata tunapojifunza kwa mara ya kwanza pamoja na wanadini. Lakini tunapoongoza funzo pamoja na wanafunzi wengine huenda tukahitaji kutumia busara ili tutambue wakati unaofaa wa kuanza kutoa sala. Unaweza kutumia Zaburi 25:4, 5 na 1 Yohana 5:14 kumsaidia mwanafunzi kuelewa kwa nini tunapaswa kusali, na Yohana 15:16 ili kueleza umuhimu wa kusali kwa Yehova katika jina la Yesu Kristo.
2 Ni nani anayepaswa kutoa sala wakati wa funzo la Biblia? Ikiwa ndugu aliyebatizwa anaandamana na dada kwenye funzo, ndugu ndiye anayepaswa kutoa sala. Hata hivyo, dada anaweza kuongoza funzo akiwa amefunika kichwa. (1 Kor. 11:5, 10) Kwa upande mwingine, ikiwa mhubiri mwanamume ambaye hajabatizwa anaandamana na dada aliyebatizwa kwenye funzo, dada ndiye anayepaswa kutoa sala. Katika kisa kama hicho, dada anapaswa kufunika kichwa anapotoa sala na anapoongoza funzo.
3 Mambo Unayoweza Kutaja Katika Sala: Si lazima utoe sala ndefu kwenye funzo la Biblia, lakini unapaswa kutaja mambo hususa. Mbali na kumwomba Mungu abariki funzo na kumshukuru kwa kweli mlizojifunza, inafaa kumsifu Yehova kwa sababu yeye ndiye Chanzo cha mafundisho hayo. (Isa. 54:13) Tunaweza pia kutaja mambo yanayoonyesha kwamba tunamjali sana mwanafunzi na tunathamini tengenezo ambalo Yehova hutumia. (1 The. 1:2, 3; 2:7, 8) Tunapomwomba Yehova abariki jitihada za mwanafunzi za kuishi kupatana na yale anayojifunza, huenda akaona umuhimu wa kuwa ‘mtendaji wa neno.’—Yak. 1:22.
4 Kuna faida nyingi za kusali wakati wa funzo. Sala hutuletea baraka za Mungu. (Luka 11:13) Umuhimu wa kujifunza Neno la Mungu hukaziwa tunaposali. Mwanafunzi hujifunza jinsi ya kusali anaposikiliza sala zetu. (Luka 6:40) Zaidi ya hayo, sala zinazotoka katika moyo uliojaa upendo kwa Mungu na shukrani kwa sifa zake zisizo na kifani zinaweza kumsaidia mwanafunzi kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova.
[Maswali ya Funzo]
1. (a) Kwa nini inafaa kuanza na kumalizia funzo la Biblia kwa sala? (b) Tunaweza kutumia maandiko gani ili kumweleza mwanafunzi kwa nini tunapaswa kusali kabla na baada ya funzo?
2. Ni nani anayepaswa kutoa sala ikiwa ndugu aliyebatizwa au mhubiri mwanamume ambaye hajabatizwa anaandamana na dada kwenye funzo la Biblia?
3. Tunaweza kutaja mambo gani tunapotoa sala wakati wa funzo la Biblia?
4. Kuanza na kumalizia funzo la Biblia kwa sala huleta faida gani?