Biblia Itakaziwa Zaidi
1 Toleo la kwanza la gazeti The Golden Age lilichapishwa mnamo Oktoba 1, 1919. Gazeti hilo lilikuwa kifaa bora sana katika kazi ya kuhubiri. Kwa nini? Kwa sababu lilitolewa hasa kwa ajili ya umma. Haikuwa hivyo kuhusu gazeti la Mnara wa Mlinzi, ambalo kwa muda mrefu lilionwa kuwa gazeti la “kundi dogo.” (Luka 12:32) Wahubiri wa Ufalme walisisimuka sana gazeti The Golden Age lilipotolewa, na kwa miaka mingi idadi ya nakala zilizochapwa za The Golden Age ilizidi ile ya Mnara wa Mlinzi.
2 Gazeti The Golden Age lilikusudiwa kuwafahamisha watu kuwa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo ndio suluhisho la kweli la matatizo ya wanadamu nao utawaletea wanadamu maisha bora. Kwa makumi ya miaka iliyofuata, mabadiliko yalifanywa katika gazeti hilo ili lifae hali za watu zilizokuwa zikibadilika. Katika mwaka wa 1937, jina la gazeti hilo lilibadilishwa kuwa Consolation. Kisha, katika mwaka wa 1946 likapewa jina Amkeni!, jina tunalotumia hadi leo.
3 Tangu lilipotolewa, gazeti hilo limetimiza sehemu muhimu katika kazi kubwa ya kuhubiri ambayo imefanywa tangu mwaka wa 1919. (Mt. 24:14) Hata hivyo, kwa kuzingatia wakati mfupi unaobaki, inafaa kufanya mabadiliko mengine katika gazeti la Amkeni!
4 Mamilioni ya watu hupenda kusoma Amkeni! kwa sababu linazungumzia habari nyingi zisizo za kidini kwa njia ya kuvutia. Bila shaka, idadi kubwa ya watu wanaohudhuria Ukumbusho kila mwaka husoma gazeti la Amkeni! Lakini, ili mtu afichwe katika “siku ya hasira ya Yehova,” anahitaji kusaidiwa kufanya mengi zaidi kuliko kusoma tu vichapo vyetu kwa ukawaida.—Sef. 2:3; Ufu. 14:6, 7.
5 Hivyo, kuanzia Januari 2006, Amkeni! litakazia zaidi Ufalme wa Mungu. Litawahimiza waziwazi wasomaji watafute masuluhisho ya matatizo yao katika Biblia, nalo litazungumzia sana jinsi matukio ya siku hizi yanavyotimiza unabii wa Biblia. Kwa njia hiyo, wasomaji watafahamu vizuri zaidi matukio ya siku hizi na huenda mambo wanayosoma yakawachochea wajifunze zaidi kumhusu Yehova.—Zek. 8:23.
6 Amkeni! litaendelea kuzungumzia habari zinazowapendeza watu wengi. Hata hivyo, gazeti hilo litakazia Biblia zaidi. (1 The. 2:13) Kwa kuwa Mnara wa Mlinzi huzungumzia ujumbe wa Biblia kwa undani na Amkeni! litakuwa likizungumzia habari nyingi ya Kimaandiko, hakutakuwa na uhitaji wa kuendelea kuchapisha Amkeni! mara mbili kwa mwezi. Hivyo, kuanzia Januari 2006, Amkeni! litakuwa likitolewa mara moja kwa mwezi. Hatua hiyo itarahisisha kazi ya kutayarisha, kutafsiri, na kusafirisha vichapo vyetu.
7 Amkeni! huchapishwa katika lugha nyingi na badiliko hilo litahusisha asilimia 40 hivi ya lugha hizo. Katika lugha nyingi, tayari Amkeni! huchapishwa mara moja kwa mwezi, au mara nne kwa mwaka. Hakutakuwa na mabadiliko katika uchapishaji wa Mnara wa Mlinzi.
8 Wahubiri watatoa toleo la kila mwezi la Amkeni! pamoja na toleo lolote la Mnara wa Mlinzi la mwezi huohuo. Kwa kuwa wahubiri watatoa toleo lilelile la Amkeni! kwa mwezi mzima, hawatahitaji kubadilisha maelezo yao katikati ya mwezi wanapolitoa kama tunavyofanya leo.
9 Tangu toleo la kwanza katika mwaka wa 1919, gazeti lililoitwa The Golden Age, kisha Consolation, na ambalo sasa linaitwa Amkeni! limesaidia sana katika kazi ya kuhubiri habari njema. Tunatumaini Yehova ataendelea kubariki ugawanyaji wa gazeti hilo ambalo litafanyiwa mabadiliko na kwamba litawasaidia watu wengi zaidi kutoka “mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,” kuuona Ufalme wa Mungu kuwa tumaini lao la pekee.—Ufu. 7:9.
[Maswali ya Funzo]
1. Mwanzoni, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilichapishwa hasa kwa ajili ya nani, na gazeti The Golden Age lilitolewa kwa ajili ya nani?
2. Gazeti The Golden Age linaitwaje leo, lilichapishwa kwa kusudi gani?
3. Gazeti la Amkeni! limekuwa kifaa bora katika kutimiza unabii gani?
4. (a) Mtu anahitaji kufanya nini ili afichwe katika “siku ya hasira ya Yehova”? (b) Kulingana na kitabu cha Ufunuo 14:6, 7, ‘malaika anayeruka katikati ya mbingu’ anawaambia watu wote wafanye nini?
5. (a) Kuanzia Januari 2006, ni habari gani itakayokaziwa katika gazeti la Amkeni!? (b) Huenda wengi wakachochewa kufanya nini, na kwa njia hiyo watatimiza unabii gani?
6, 7. (a) Amkeni! litawasaidiaje wengi watende kupatana na 1 Wathesalonike 2:13? (b) Amkeni! litachapishwa mara ngapi kwa mwezi, na badiliko hilo litahusisha lugha ngapi?
8. Wahubiri watatoa gazeti la Amkeni! pamoja na Mnara wa Mlinzi jinsi gani?
9. Amkeni! litaendelea kufanya nini?