Ratiba ya Familia—Utumishi wa Shambani wa Familia
1 Yehova hushangilia kuwaona vijana wakilisifu jina lake. (Zab. 148:12, 13) Katika siku za Yesu hata ‘watoto na wanaonyonya walimsifu’ Mungu. (Mt. 21:15, 16) Hivyo ndivyo ilivyo leo. Wazazi, mnaweza kuwasaidiaje watoto wenu wawe watu wanaomsifu Yehova kwa bidii katika huduma ya Kikristo? Kama ilivyokaziwa katika makala iliyo juu, inayozungumzia mikutano ya kutaniko, mfano wenu ni muhimu sana. Baba mmoja alisema jambo ambalo wazazi wengi wamejionea. Alisema hivi: “Watoto hufuata mfano wako wala si maneno yako!”
2 Dada mmoja aliyelelewa na wazazi wanaomcha Mungu anasema hivi: “Hatukuamka kamwe Jumamosi asubuhi na kujiuliza ikiwa tungeenda kwenye huduma. Tulijua kwamba tungeenda.” Ninyi pia, mnaweza kukazia umuhimu wa kazi ya kuhubiri kwa kuhubiri pamoja na familia zenu kwa ukawaida. Hilo haliwawezeshi watoto wenu kuiga mfano wenu tu, bali pia huwawezesha ninyi kuchunguza mtazamo wao, tabia, na maendeleo yao.
3 Kuwazoeza Hatua kwa Hatua: Ili watoto wafurahie utumishi, ni lazima wazoezwe kuhubiri vizuri. Dada aliyenukuliwa mapema alisema hivi: ‘Hatukuandamana tu na wazazi wetu katika kazi yao. Tulijua kuwa tunapaswa kufanya jambo fulani, hata ikiwa ilikuwa tu kubisha mlango na kuacha kikaratasi cha mwaliko. Kwa kutayarishwa vema kabla ya utendaji wa kila mwisho-juma, tulijua kile ambacho tungesema.’ Unaweza kuwazoeza watoto wako kwa kutumia dakika chache kila juma kuwatayarisha kwa ajili ya huduma ya shambani, iwe wakati wa funzo la familia au katika pindi nyingine.
4 Kuhubiri pamoja mkiwa familia huwapa nafasi nyingine ya kuwafundisha watoto wenu kweli. Baba mmoja aliandamana na binti yake alipotembea kilometa 20 (safari ya kwenda na kurudi) ili kuwaachia wanakijiji katika bonde fulani trakti za Biblia. Binti huyo anasema hivi: ‘Baba yangu alikazia kweli moyoni mwangu tulipokuwa tukitembea.’ (Kum. 6:7) Yehova na awabariki kwa kupanga huduma ya shambani katika ratiba ya kila juma ya familia zenu.