Sitawisha Upendezi wa Watu Unaowapelekea Magazeti kwa Ukawaida
1 Watu wengi tunaowakuta katika huduma hutukaribisha na kukubali vichapo vyetu, lakini husita kukubali funzo la Biblia la kawaida. Njia moja ya kusitawisha upendezi wao ni kwa kuwapelekea magazeti kwa ukawaida. Unapomwachia mtu magazeti, andika jina na anwani yake, tarehe uliyomtembelea, magazeti aliyochukua, andiko mlilozungumzia, na jambo lingine lolote lililokusaidia kutambua mambo yanayompendeza mtu huyo. Unapopata magazeti mapya, yasome na utafute mambo ambayo yatawavutia wale unaowapelekea magazeti kwa ukawaida, kisha uzungumzie mambo hayo unapowatembelea. (1 Kor. 9:19-23) Baada ya muda, huenda wakavutiwa na jambo fulani katika magazeti yetu na wakataka kujifunza zaidi.
2 Hata hivyo, tunatambua kwamba watu wengi hawatakuwa watumishi wa Yehova kwa kusoma magazeti tu. Kwa kuwa ni muhimu watu wamtafute Yehova sasa, tunaweza kuwasaidiaje wafanye hivyo? (Sef. 2:2, 3; Ufu. 14:6, 7) Tunaweza kusitawisha upendezi wao kwa kusoma nao andiko moja ambalo tumelichagua kwa uangalifu kila wakati tunapowapelekea magazeti.
3 Kuzungumzia Andiko Moja: Fikiria wale unaowapelekea magazeti kwa ukawaida, kisha utayarishe mazungumzo yanayotegemea andiko moja ambalo mtazungumzia na kila mmoja wao ikitegemea mahitaji yake. (Flp. 2:4) Kwa mfano, ikiwa mmoja wao amefiwa na mpendwa wake, unaweza kumrudia mara kadhaa ili mzungumzie yale ambayo Biblia inasema kuhusu hali ya wafu na tumaini la ufufuo. Maelezo yanayopatikana katika kitabu Kutoa Sababu chini ya kichwa “Kifo” na “Ufufuo” yanaweza kutumiwa kutayarisha mazungumzo yanayotegemea andiko moja. Baadaye huenda ikawa rahisi kuendelea na mazungumzo kwa kuzungumzia mambo kama vile kuondolewa kabisa kwa ugonjwa, uzee, na kifo. Nia yetu ni kutafuta jambo linalomvutia mtu na kumwonyesha maoni ya Biblia kulihusu hatua kwa hatua.
4 Wasaidie Waelewe: Ingawa ni vizuri kuwa na mazungumzo mafupi na rahisi, kusoma tu andiko ulilochagua hakutoshi. Shetani amepofusha fikira za watu ili wasielewe habari njema. (2 Kor. 4:3, 4) Hata wale wanaojua mambo fulani katika Biblia wanahitaji kusaidiwa kuielewa. (Mdo. 8:30, 31) Kwa hiyo, fafanua na ueleze andiko hilo vizuri, kama vile ungefanya ikiwa ungekuwa ukitoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. (Mdo. 17:3) Hakikisha kwamba mtu huyo amejua jinsi Neno la Mungu linavyoweza kumnufaisha maishani.
5 Ikiwa mtu huyo anafurahia mambo anayojifunza, hatua kwa hatua ongeza idadi ya maandiko mnayozungumzia kila mara unapomtembelea. Unaweza kuzungumzia maandiko mawili au matatu zaidi. Tafuta fursa ya kuzungumzia broshua Anataka au kitabu Ujuzi. Kwa njia hiyo, mtu huyo ambaye umekuwa ukimpelekea magazeti kwa ukawaida, huenda hatimaye akawa mwanafunzi wa Biblia.
[Maswali ya Funzo]
1. Tunaweza kusitawishaje upendezi wa watu kwa kuwapelekea magazeti kwa ukawaida?
2. Kwa nini ni muhimu watu wamtafute Yehova sasa, nasi tunaweza kuwasaidiaje wafanye hivyo?
3. (a) Tunaweza kutayarishaje mazungumzo yanayotegemea andiko moja? (b) Ni mambo gani yanayowavutia watu katika eneo lenu?
4. Kwa nini ni muhimu kuwasaidia wengine waelewe Maandiko, na tunaweza kufanyaje hivyo?
5. Mtu unayempelekea magazeti kwa ukawaida, anawezaje kuwa mwanafunzi wa Biblia?