Deni Letu kwa Wengine
1 Mtume Paulo alihisi kwamba ana wajibu wa kuwahubiria watu. Alijua kwamba Yehova alikuwa amefungua njia ili watu wa namna zote waokolewe kupitia damu yenye thamani ya Mwanaye. (1 Tim. 2:3-6) Kwa hiyo, Paulo alisema: “Mimi nina deni kwa Wagiriki na kwa Wabaribari pia, kwa wenye hekima na kwa wasio na akili pia.” Alijitahidi sana kulipa deni lake kwa wanadamu wenzake kwa kuwahubiria habari njema.—Rom. 1:14, 15.
2 Kama Paulo, Wakristo leo hujitahidi kuwahubiria majirani wao habari njema katika kila fursa. Tunapaswa kuwatafuta haraka watu wenye mioyo minyoofu kwa sababu “dhiki kubwa” inakaribia upesi. Upendo wa kweli kwa watu na utuchochee kuwa na bidii katika kazi hii ya kuokoa uhai.—Mt. 24:21; Eze. 33:8.
3 Kulipa Deni Letu: Kuhubiri nyumba kwa nyumba ndiyo njia yetu kuu ya kuwafikia watu. Tunaweza kuzungumza na watu wengi ambao kwa kawaida hawapatikani nyumbani tukiweka rekodi sahihi na kurudi nyakati mbalimbali. (1 Kor. 10:33) Tunaweza pia kuwafikia watu kwa kuhubiri katika eneo la biashara, barabarani, katika bustani, kwenye maegesho ya magari, na kupitia simu. Ni vizuri tujiulize, ‘Je, ninajitahidi kutumia njia mbalimbali ili kuwahubiria watu ujumbe wa uzima?’—Mt. 10:11.
4 Dada mmoja painia alihisi ana jukumu kubwa la kuwahubiria watu wote katika eneo lake. Mapazia ya nyumba moja hayakuwa yakifunguliwa, na hakuwa akimpata mtu yeyote nyumbani humo. Hata hivyo, siku moja ambayo painia huyo hakuwa katika utumishi, aliona gari mbele ya nyumba hiyo ambayo kwa kawaida haikuwa na mtu yeyote. Hakutaka kupoteza nafasi hiyo, basi akabisha hodi. Mwanamume alifungua mlango huo, na baada ya ziara ya kwanza, dada huyo na mumewe walimtembelea mtu huyo mara kadhaa. Mwishowe, mtu huyo alikubali funzo la Biblia, na sasa ni ndugu aliyebatizwa. Anashukuru kwamba dada huyo alihisi ana deni au jukumu la kuwahubiria wengine.
5 Mwisho unapokaribia haraka, tunapaswa kulipa deni letu kwa wanadamu wenzetu sasa kwa kujitahidi kabisa katika kazi ya kuhubiri.—2 Kor. 6:1, 2.