Programu Mpya ya Kusanyiko la Pekee
Jicho limebuniwa kwa njia ya ajabu sana. (Zab. 139:14) Lakini tunaweza kukazia macho kitu kimoja tu kwa wakati mmoja. Ndivyo ilivyo kuhusu macho yetu ya kiroho. Ili macho yetu ya kiroho yakazie kitu kimoja tu, ni lazima tuzingatie kufanya mapenzi ya Mungu. Kwa sababu mambo yenye kukengeusha yanazidi kuongezeka katika ulimwengu wa Shetani, ni jambo linalofaa sana kwamba programu yetu ya kusanyiko la pekee la mwaka wa utumishi wa 2006 itazungumzia kichwa “Uwe na Jicho Rahisi”!—Mt. 6:22.
Tutafanya nini ili Yehova atubariki? (Met. 10:22) Swali hilo litajibiwa katika sehemu yenye kichwa “Baraka za Kuwa na Jicho Rahisi.” Mahojiano yatakazia jinsi tunavyoweza kufaidika kwa kufuata kanuni za Maandiko. Hotuba ya kwanza ya msemaji anayezuru, “Kuwa na Jicho Rahisi Katika Ulimwengu Mwovu,” itatuonya kuhusu mambo yanayoweza kuvuruga maisha yetu na hatimaye kutuzuia tusifanye maendeleo ya kiroho. Pia tutajifunza mambo yanayohusika katika kuchagua “fungu jema.”—Luka 10:42.
Wazazi na wengine wanawezaje kuwahimiza vijana Wakristo wakazie fikira miradi ya kiroho? Katika hotuba “Wazazi Wanaolenga Mishale Yao Vizuri” na “Vijana Wanaofuatia Miradi ya Kiroho,” wazazi na vijana watatoa maelezo kuhusiana na swali hilo muhimu. (Zab. 127:4) Hotuba ya mwisho itakayotolewa na msemaji anayezuru itaonyesha jinsi tunavyoweza kusonga mbele pamoja na tengenezo la Yehova tukiwa mtu mmoja-mmoja, tukiwa familia, na tukiwa kutaniko.
Iwe sisi ni wapya katika kweli au tumemtumikia Yehova kwa miaka mingi, ni muhimu ‘tuwe na jicho rahisi.’ Programu ya kusanyiko la pekee itatusaidia kufanya hivyo.