Programu Mpya ya Kusanyiko la Pekee
Tukiona au kusikia onyo fulani lakini tusitende kulingana nalo, matokeo yanaweza kuwa mabaya sana. Hata la muhimu zaidi, ni kutenda kulingana na mwelekezo wa kiroho ambao Yehova hutoa. Jambo hilo litakaziwa kwenye programu ya kusanyiko la mwaka ujao wa utumishi. Kichwa chake ni, “Kazieni Uangalifu Jinsi Mnavyosikiliza.”—Luka 8:18.
Katika hotuba yake ya kwanza, msemaji anayezuru atazungumzia jinsi shauri lililo katika sura za kwanza za barua ya Paulo iliyoongozwa na roho ya Mungu kwa Waebrania linavyotuhusu sisi leo. Katika hotuba ya kumalizia, “Sikiliza Daima Mafundisho ya Mungu,” msemaji huyo atatusaidia sote tujichunguze kama kwa kweli tunamsikiliza Yehova, Mwana wake, na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45.
Sehemu kadhaa katika programu zitafaidi hasa familia. Hotuba yenye kichwa “Familia Zinazosikiliza Neno la Mungu Bila Kukengeushwa” itatusaidia tusiruhusu vitu vya ulimwengu virudishe nyuma maendeleo yetu ya kiroho. Itatia ndani mahojiano ya wale ambao wamefanya mabadiliko ili kutanguliza mambo ya kiroho. Hotuba yenye kichwa, “Jinsi Kusikiliza Neno la Mungu kwa Makini Kunavyowaimarisha Vijana Wetu,” itatia ndani mahojiano ya vijana ambao wameushika ukweli shuleni, wakiwa na marika wao, au katika huduma. Hotuba yenye kichwa, “Watoto Wachanga Wanaomsikiliza Mungu na Kujifunza,” itatusaidia tusipuuze uwezo wa kujifunza wa watoto wachanga. Vijana pamoja na wazazi wao wanaohojiwa watatusaidia tuone faida zinazotokana na kuwafunza watoto njia za Yehova tangu wakiwa wachanga.
Huku Shetani ‘akiipotosha dunia nzima inayokaliwa,’ Yehova anaonyesha watumishi wake waaminifu njia wanayopaswa kutembea. (Ufu. 12:9; Isa. 30:21) Kusikiliza kwa makini na kulitii shauri lake katika maisha yetu hutufanya tuwe na hekima na furaha, na huongoza kwenye uzima wa milele.—Met. 8:32-35.