Tafuta Nafasi za Kuhubiri
1 Kutaniko la Kikristo lina watu wa hali mbalimbali. Hata hivyo, tumeazimia kumsifu Yehova kwa umoja. (Zab. 79:13) Tunawezaje kutafuta nafasi za kuhubiri ikiwa afya mbaya au matatizo mengine yanatuzuia kuhubiri habari njema kikamili?
2 Katika Shughuli za Kila Siku: Yesu aliwahubiria watu hata alipokuwa katika shughuli zake za kila siku. Alipokuwa akipita nje ya ofisi ya kodi alimhubiria Mathayo, alipokuwa akisafiri akamhubiria Zakayo, na alipokuwa akipumzika akamhubiria mwanamke Msamaria. (Mt. 9:9; Luka 19:1-5; Yoh. 4:6-10) Sisi pia tunaweza kuwahubiria watu tunaokutana nao katika shughuli zetu za kila siku. Tukiwa na Biblia, trakti au broshua karibu, tutakuwa tayari kuzungumza kuhusu tumaini letu.—1 Pet. 3:15.
3 Je, kushindwa kutembea kumekuzuia kwa kadiri fulani kushiriki katika kazi ya nyumba kwa nyumba? Tafuta nafasi za kuwahubiria wahudumu wa afya na watu wengine wanaokutembelea. (Mdo. 28:30, 31) Ikiwa kwa sababu ya hali fulani unakaa nyumbani kwa muda mrefu, je, umejaribu kuhubiri kupitia simu au barua? Dada mmoja huwaandikia barua kwa ukawaida watu wa ukoo ambao si Mashahidi. Yeye hutia ndani Maandiko yenye kutia moyo na mambo aliyoona alipokuwa akihubiri.
4 Kazini au Shuleni: Tamaa yetu ya kumsifu Yehova itatuchochea pia tutafute nafasi za kupanda mbegu za kweli kazini au shuleni. Mhubiri mmoja mwenye umri wa miaka minane aliwaeleza wanadarasa wenzake mambo aliyosoma kwenye gazeti moja la Amkeni! lililokuwa likizungumza kuhusu mwezi. Baada ya kujua chanzo cha habari hiyo, mwalimu wake alianza kuchukua magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa ukawaida. Tukiwa kazini, tunaweza kuweka kitabu Biblia Inafundisha mahali ambapo wengine wanaweza kukiona. Jambo hilo linaweza kuwafanya waulize maswali na kutupa nafasi ya kuwahubiria.
5 Je, unaweza kufikiria njia za kutafuta nafasi ya kuhubiri unapokuwa katika shughuli zako za kila siku? Kwa kutumia kila nafasi tunayopata, na tujitahidi kila siku ‘kumtolea Mungu dhabihu ya sifa.’—Ebr. 13:15.