Je, Unaweza Kubadili Ratiba Yako?
1 Tukiwa Wakristo wa kweli, tumekubali mwaliko wa kuwa “wavuvi wa watu.” (Mt. 4:19) Kama wavuvi halisi, huenda tukapata matokeo mazuri zaidi katika kazi hiyo ikiwa tutapanga ratiba ya kuhubiri wakati watu wanapopatikana. Watu wengi hupatikana nyumbani alasiri na jioni. Mara nyingi wao huwa wametulia kiakili na huenda wakapendezwa zaidi kuwapokea wageni wakati huo. Je, unaweza kubadili ratiba yako uhubiri wakati kama huo?—1 Kor. 9:23.
2 Mahubiri ya Jioni: Kupanga kimbele kuhubiri jioni kunaweza kutusaidia kuwafikia watu wengi zaidi kwa habari njema. (Met. 21:5) Vijana wanaweza kuhubiri baada ya shule. Wengine wanaweza kuhubiri baada ya kazi. Mafunzo fulani ya kitabu yanaweza kupanga kuhubiri kwa saa moja kabla ya funzo lao la kila juma.
3 Ikiwa tutahubiri nyumba kwa nyumba wakati wa alasiri na jioni tutaweza kuzungumza na wale ambao kwa kawaida hawapatikani nyumbani. Katika maeneo mengi, mahubiri ya barabarani na mahubiri mengine yanaweza kufanywa jioni. Na wengi huona jioni kuwa wakati bora wa kufanya ziara za kurudia na kuanzisha mafunzo ya Biblia.
4 Utambuzi Unahitajika: Unahitaji kuwa na busara unapohubiri jioni. Mara nyingi inafaa kuhubiri tu mapema jioni, badala ya kuwatembelea wenye nyumba usiku wakati ambapo huenda wakawa wanajitayarisha kulala. (Flp. 4:5) Unapogonga mlango, simama mahali unapoweza kuonekana, na ujitambulishe waziwazi. Eleza haraka kusudi lako. Ukifika wakati usiofaa, kama vile wakati familia inapokula, waambie utawatembelea wakati mwingine. Uwe mwenye ufikirio nyakati zote.—Mt. 7:12.
5 Tunahitaji pia kutambua hatari zinazoweza kutokea. Ikiwa mnahubiri baada ya giza kuingia, ni jambo la hekima kusafiri mkiwa wawili-wawili au katika vikundi. Pitieni kwenye njia zenye mwangaza wa kutosha ambapo pana watu. Hubirini tu maeneo mnayoona kuwa ni salama. Epukeni maeneo ambayo huenda yasiwe salama baada ya giza kuingia.—Met. 22:3.
6 Kuhubiri jioni hutuwezesha kuhubiri pamoja na mapainia-wasaidizi na mapainia wa kawaida. (Rom. 1:12) Je, unaweza kubadili ratiba yako ili ushiriki katika sehemu hii ya utumishi?
[Maswali ya Funzo]
1. Kwa nini tunapaswa kubadili ratiba yetu ya kuhubiri?
2. Tunaweza kutumia njia zipi kuwafikia watu wengi zaidi kwa habari njema?
3. Ni katika njia gani unaweza kuhubiri alasiri na jioni katika eneo lenu?
4. Kwa nini ni muhimu kuwa na utambuzi na ufikirio unapohubiri jioni?
5. Tunaweza kuepukaje hatari zinazoweza kutokea tunapohubiri?
6. Tunaweza kupata faida gani ya ziada kwa kuhubiri jioni?